NA ZUHURA JUMA
JUMUIYA ya Maimamu wilaya ya Chake-Chake (JUMAZA) imewataka wazazi na walezi kisiwani Pemba kufanya mambo yao kwa kufuata taratibu na miongozo ya dini ya kiislamu katika kipindi cha sikukuu ya Eid-el-Hajj, ili kuwakinga watoto na udhalilishaji.
Akizungumza
na waandishi wa habari ofisini kwao Chake Chake, Katibu wa Kamati ya Maadili
kutoka JUMAZA, Sheikh Abdalla Mnubi Abas, alisema kamati haimzuii mtu kutembea
lakini cha muhimu ni kuwalinda watoto dhidi ya udhalilishaji.
Alieleza kuwa, kipindi cha sikukuu watoto wengi
hufanyiwa
udhalilishaji, hivyo ni vyema kwa wazazi na
walezi kufuata taratibu na miongozo ya kiislamu ambayo itasaidia kuwalinda
watoto wao na janga hilo.
“Inapomaliza sikukuu tunapata kesi nyingi za
watoto wetu kufanyiwa udhalilishaji, hivyo tutakapofuata taratibu ya dini yetu ya
kiislamu tutawadhibiti,” alisema.
Alisema katika kuwadhibiti watoto hao ni vyema
wakaongozana nao katika viwanja vya kufurahishia watoto, jambo ambalo
litasaidia kwa kiasi kikubwa kuepuka vishawishi.
“Watoto wanatoka peke yao bila usimamizi wa
wazazi, hii ni hatari kubwa kwao, hivyo tukawatembeze watoto wetu,” alieleza.
Aidha aliitaka jamii isifanye mambo yalio nje ya
utaratibu wa dini ya kiislamu na waende
na mfumo ambao hautaathiri jamii.
Kwa upande wake, Naibu Amiri kutoka JUMAZA,
Sheikh Seif Khamis Nassor aliiomba
serikali kuwaruhusu watoto kutembea kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 12:30 jioni, ili kuwaepusha kufanyiwa vitendo
vya udhalilishaji.
“Mara nyingi udhalilishaji hufanyika nyakati za
usiku, hivyo viwanja vya kufurahishia watoto ni vyema tukavifungua asubuhi na
kuvifunga magharibi,” alisema.