KAMA kuna zawadi kubwa na muhimu kabisa tuliyopatiwa na Mwenyezi Mungu sisi watu wa Zanzibar, Tanzania, Afrika Mashariki na Kati ni tunu ya kipekee ya lugha ya Kiswahili.
Wageni walipo tawala sehemu mbalimbali duniani walilazimisha kuzungumzwa kwa lugha zao, ndio maana hatushangani maeneo mengi duniani yamekuwa yakizungumzwa lugha za kikoloni hadi leo.
Na kwa jinsi wakoloni walivyokuwa washindani, ambapo hivi sasa huitwa mataifa makubwa wakazivisha hadhi lugha zao na kuziita lugha za kimataifa, ambapo kila mkutano muhimu duniani mawasiliano ni kupitia lugha zao.
Kwa jinsi walivyozitukuza lugha zao, wametulazimisha na kutuaminisha kuwa ufasaha wa kuzitumia lugha zao kwenye kuzungumza na kuandika ndio upeo wa utaalamu.
Pamoja na kwamba sehemu ya mwambao wa Afrika Mashariki ilitawaliwa na wakoloni kwa miaka kadhaa, lakini watu wa eneo hili hawakuweza kusahau lugha ya Kiswahili waliyozaliwa nayo.
Kiasili hasa lugha hii ilianzia pwani ya Afrika Mashariki na kusambaa katika nchi kadhaa zilizokaribu na pwani hiyo hadi kuelekea sehemu za bara arabu na duniani kote.
Viko vyuo vikuu kutoka nchi mbalimbali duniani vinafundisha lugha ya kiswahili baada ya kutanabahi umuhimu wa lugha hiyo, ambapo baadhi ya vyuo hivyo vinatoa shahada za juu kabisa.
Aidha vipo vyombo vya habari vya kimataifa hasa redio zinazo peperusha matangazo yao kwa kutumia lugha ya Kiswahili, mafanao wa redio hizo ni kutoka nchi za China, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani, Japani, Uturuki, Iran na kadhalika.
Hata hivyo ukweli ni kwamba Kiswahili hivi sasa kinapita kwenye wakati mgumu, ambapo nyumbani kwao ndio kimeanza kupoteza hadhi katika nyanja mbalimbali.
Kwa mfano, wazungumzaji wa Kiswahili hivi sasa tunawazungumzia wa hapa Zanzibar ambapo inaamika lugha hii ndio kwao, wameanza kutamka sivyo baadhi ya misamiati.