NA MAULID YUSSUF
ALIYEKUWA Mwakilishi wa Viti Maalum Mkoa wa Kaskazini Unguja, Riziki Pembe Juma, amewataka wazazi kushikamana katika kuendelea kuwaelimisha vijana juu ya kukiletea ushindi chama cha Mapinduzi katika chaguzi zao.
Akizungumza wakati alipokabidhi seti ya TV pamoja na kin’gamuzi katika maskani ya wazee huko Donge Pale amesema, vijana ndio nguvu kazi ya Taifa katika kuleta maendeleo katika nchi.
Riziki amesema kukabidhi vifaa hivyo ni utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi, ambapo chama hicho kimekuwa na utaratibu wa kutekeleza yanapangwa.
Aidha Riziki ambae pia ni Waziri wa Elimu Zanzibar amewasisitiza wazazi kushirikiana na Walimu, ili kuhakikisha vijana wanasoma kwa bidii ili kuongeza daraja la ufaulu kwa Mkoa wa Kaskazini Unguja na kurudisha heshima ya Mkoa wao kama iliyokuwepo hapo awali.
Amesema kwa kipindi kirefu Mkoa wa Kaskazini umekuwa nyuma kutokana na watoto wengi kutoshughulikia masomo yao, na hivyo kusababisha kupata watoto wengi wa mitaani wanaofeli masomo yao.