NA   ARAFA  MOHAMED

VIJANA wa  Chama cha Mapinduzi CCM Zanzibar, wametakiwa kuachana na  masuala ya makundi, ili kujiepusha na vitendo viovu na badala yake  kushirikiana kwa pamoja na kuonesha uzalendo wa Chama chao.

 Wito huo umetolewa na aliyekuwa Mwakilishi wa  Viti Maalum  (UWT) Mkoa wa Mjini,  Saada Ramadhan  Mwendwa, wakati alipokuwa  akizungumza na vijana hao huko  Baraza la Vijana   (UVCCM) katika ukumbi wa CCM Amaan Mkoa.

Alisema, chama cha  Mapinduzi  kimeanzisha mabaraza   ya  vijana kwa  lengo  la kuweza  kukutanisha   vijana wote  na kuweza  kukisaidia chama,  ili kufikia malengo  yaliyokusudiwa  na chama  hicho .

Alifahamisha kuwa, Vijana ndio nguvu kazi ya Taifa hivyo ni vyema wakawa wazalendo na nchi yao, na kukipenda chama chao  ili kuweza kuleta maendeleo yao binafsi  na taifa kwa ujumla.

Aidha,  Saada  aliwasihi  vijana   kujitokeza  kwa  wingi    kukipigia kura  chama hicho, katika uchaguzi Mkuu na kuhakikisha chama cha mapinduzi    kinapata  ushindi wa kishindo   kwa  mwaka 2020 .