LONDON, England
KLABU ya Arsenal imemsajili kiungo wa Brazil, Willian kwa mkataba wa miaka mitatu, akitokea Chelsea.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 32 mkataba wake na Chelsea, umekamilika na ametua bure Emirates.
‘The Blues’ ilitoa ofa mpya kwa mchezaji huyo, lakini, haikuwa tayari kufikia kile ambacho washika bunduki hao wamekitoa.
“Naamini ni mchezaji ambaye kweli anaweza kutufanyia mabadiliko makubwa”, alisema, kocha wa Arsenal, Mikel Arteta.
“Tulikuwa tumedhamiria kabisa kuimarisha upande wa kushambulia wa kiungo wa kati na nafasi ya winga”.
Willian alishiriki michezo 339 kwa Chelsea baada ya kusajiliwa akitokea klabu ya Anzhi Makhachkala ya Urusi kwa pauni milioni 30 mwaka 2013.
“Ni mchezaji ambaye tunaweza kumbadilisha badilisha, Anaweza kucheza nafasi tatu au nne tofauti,” Arteta, aliongeza.
“Ana tajriba ya kila safu ya uwanja wa soka, lakini, bado ana nia ya kuja hapa kuchangia kuweka klabu katika nafasi inayostahili kuwa.
“Nimefurahishwa na mazungumzo yangu nae na jinsi alivyokuwa anataka kujiunga nasi”.(BBC Sports).