NA MUNIR SHEMWETA, WANMM SIMIYU

NAIBU Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Angeline Mabula, amemuagiza Kamishana Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Simiyu, Essau Mwakatumbula, kuhakikisha unafanyika mchakato wa kupima eneo la maonesho ya Nanenane Nyakabindi wilayani Bariadi mkoani Simiyu na kumilikishwa.

Dk. Mabula, alitoa kauli hiyo alipotembelea Banda la Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi tarehe 6 Agosti 2020 kwenye viwanja vya maonesho vya Nanenane  vilivyopo eneo la Nyakabindi mkoani Simiyu.

Alisema, kwa sasa viwanja vya Nyakabindi Bariadi yanakofanyika maonesho ya nanenane halijamilikishwa kutokana na eneo hilo kutopimwa jambo alilolieleza kuwa linaloikosesha serikali mapato yatokanayo na kodi ya pango la ardhi.

 ‘’ Lazima tumsaidie Rais katika juhudi zake za kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati kwa kuhakikisha tunakusanya kodi ikiwemo ya pango la ardhi, sekta hii ya ardhi ikisimamiwa vizuri hakuna idara itakayoizidi kwa ukusanyaji mapato‘’ alisema Dk Mabula.

Dk. Mabula alisema baada ya maonesho ya nanenane ya mwaka huu jitihada za kumilikishwa eneo la Nyakabindi vilipo viwanja vya maonesho zifanyike ili maonesho yajayo serikali ianze kukusanya kodi ya pango la ardhi.

Kwa upande wake Kamishna Msaidizi wa Ardhi mkoa wa Simiyu Essau Mwakatumbula alisema ofisi yake ilishaanza mazungumzo na wahusika kuangalia na namna ya kumilikisha eneo hilo ili serikali kupitia Wizara ya Ardhi iweze kukukusanya mapato kupitia kodi ya pango la ardhi.

Katika hatua nyingine Dk. Mabuala, aliwataka maafisa wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi wamaoshiriki maonesho ya Nanenane Nyakabindi Bariadi mkoani Simiyu kuhakikisha wanatoa elimu kwa wananchi wanaotembelea banda hilo kuhusiana na sheria mpya iliyopitishwa Bungeni hivi karibuni.

Naibu huyo aliwataka wananchi waliokamilisha taratibu zote za kupatiwa hati ikiwemo kupimiwa eneo kuanza kutozwa kodi ya ardhi hata kama hawajachukua hati.