NA HAFSA GOLO

SERIKALI imewataka Maofisa  wa Elimu wa Mikoa Zanzibar,  kusimamia vipaumbele vilivyowekwa kwa ajili ya  usimamizi wa mitihani ya majaribio (MOCO) katika kuhakikisha wanafunzi wa kidatu cha nne wanafanya mitihani hiyo kwa uadilifu na kuondokana na vikwazo vitakavyochangia kutofikia malengo ya mtihani huo.

Mkurugenzi Elimu Sekondari Asya  Iddi, alieleza hayo alipokua akizungumza na gazeti hili ofisini kwake Mazizini Unguja, na kuwataka watendaji hao wasimamie majukumu yao kwa ufanisi huku wakizingatia sheria,kanuni na miongozo ya mitihani.

Alisema hatua hizo zitasaidia kufikia azma iliyokusudiwa katika kuwapima wanafunzi  inavyostahiki na kufahamu jinsi walimu wa masomo walivyotekeleza majukumu yao ya kazi.

“Mitihani  hii  ya majaribio ni   kielelezo tosha kinachosaidia kutoa   vipimo   vya  kutambua namna ya   athari na mapungufu yaliojitokeza kwa wanafuzi katika uwelewa wa masomo yao sambamba na hatua gani  ya uwajibikaji kwa walimu hao”,alisema.