NA MARYAM SALUM, PEMBA

KUTOWASILI kwa mashahidi wa kesi inayomkabili aliyekuwa ‘bosi’ wa

Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar ‘ZSTC’ Wilaya ya Mkoani, Seif

Suleiman Kassim, anayekabiliwa na tuhuma za kubaka mwanafunzi,

kumelazimika kuahirisha kwa mara nyingine tena baada ya upande wa

mashtaka kutopokea mashahidi wa shauri hilo.

Akiwa mahakama ya mkoa Chake Chake, Mwendesha mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, Mohamed Ali Juma alidai shauri hilo lipo kwa

ajili ya kusikilizwa, ingawa upande wao hawajapokea mashahidi.

Alidai kuwa kutokana na kutowapokea mashahidi hao, ni  vyema mahakama

hiyo kuliahirisha shauri hilo na kulipangia tarehe nyingine kwa ajili

ya kusikilizwa.

“Mheshimiwa hakimu shauri hili lipo kwa ajili ya kusikilizwa, lakini

kwa upande wetu, hatujakupokea mashahidi, hivyo ni vyema likahirishwa

na kupangiwa tarehe nyengine ingawa mtuhumiwa husika yupo mahakamani

anasubiri mwendelezo wa shauri lake”, alidai.

Hakimu wa shauri hilo, Adull-razak Abdull-kadir Ali, hakuwa na pingamizi

juu ya ombi hilo, na kisha kuliahirisha na kutaka lirudi tena

mahakamani hapo Septemba 15, mwaka huu, kwa ajili ya kusikilizwa.

Mwendesha Mashitaka alidai, shauri la Mtuhumiwa huyo linawakilishwa na

Wakili Abeid Mussa Omar, pamoja na wakili Ali Hamad Mbarouk, ambapo pia

nao waliridhia juu ya kuahirishwa kwa shauri hilo.

Awali ilidaiwa kuwa, mshtakiwa huyo Seif Suleiman Kassim miaka 58 wa

Jiondeni Mkoani, alimtorosha mtoto wa miaka 13 ambae ni mwanafunzi,

katika tarehe isiofahamika mwezi wa Aprili mwaka jana, majira ya saa

6: 00 mchana, eneo la Bandarini Mkoani Pemba.

Ilidaiwa kuwa bila ya halali, alimtorosha mtoto huyo wakati alipokua

anakwenda skuli na kisha kumuingiza kwenye ofisi aliyokuwa akifanyia

kazi ya ‘ZSTC’ iliyopo Bandarini Mkoani.

Hilo ni kosa kinyume kifungu cha 113 (1) (a) cha sheria ya Adhabu

namba 6 ya mwaka 2018, sheria ya Zanzibar.

Kosa la pili linalomkabili, ni la ubakaji wa mtoto huyo huyo, ambapo

kufanya hivyo ni kinyume na kifungu cha 108 (1), (2) (e) na kifungu

cha 109 (1) cha sheria ya Adhabu no 6 ya mwaka 2018, sheria ya

Zanzibar.