HATIMAYE ndoa iliyodumu kwa miaka mitatu baina ya mwanamuziki wa kike mwenye vituko na vitimbi, Cardi B na mumewe Offset imevunjika rasmi na hivyo wapenzi hao kila mmoja kuishi kivyake.
Kabla ya kufunga ndoa, Cardi B na aliyekuwa mchumba wake Offset ambaye ni mwanamuziki mwenziwe, walikutana mwaka 2017 baadae wakachumbiana kabla ya kuamua kuingia kwenye maisha ya ndoa.
Mnamo Oktoba 27 mwaka 2017, Cardi B na Offset walichumbiana rasmi na kuvishana pete baada ya kumalizika kwa tamasha la muziki lililopewa jina la Power 99, lililofanyika katika mji wa Philadelphia ambapo wote walialikwa kutumbuiza.
Mnamo Aprili 7 mwaka 2018 kupitia kipindi cha televisheni cha ‘Saturday Night Live’, Cardi B aliueleza umma kwamba amefanikiwa kupata ujauzito, ambapo anajiandaa kumzalia mtoto mumewe Offset na mnamo Julai mwaka 2018, Cardi B alijaaliwa kujifungua mtoto wa kike aliyeitwa Kulture Kiari Cephus.
Taarifa iliyotolewa Septemba ya mwaka 2020 kwamba Cardi B na Offset kuchana sio ya kwanza kutokana na wanamuziki hao kukwaruzana mara kwa mara kwenye mahusiano yao.
Itakumbukwa kuwa mnamo Disemba mwaka 2018 kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Instagram, Cardi B alitangaza kwamba uhusiano wake na Offset umevunjika, lakini siku chache kupita waliamua kurejeana tena.

Mnamo Februari mwaka 2019, wapenzi hao walionekana pamoja wakiongozana kwenye sherehe za utoaji wa tuzo za grammy, huku wakipanda pamoja jukwaani.
Lakini kwanini Cardi B na Offset wamevunja uhusiano wao? Kwa mujibu wa taarifa Cardi B ndiye aliyewasilisha faini la kuvunja ndoa mahakamani kuvunja uhusiano huo kwa kile alichokieleza mumewe huyo hajatulia na mwenye jicho la nje.
Kwa maana nyengine na kwa msemo wa kisasa, Offset ana michepuko ama vimanda nje ya ndoa, jambo ambalo Cardi B, amesema linamsononesha na asingependa kuona mambo mazuri na matam ambayo ni haki yake kugawana na wengine.
Cardi B, ambaye amejizolea umaarufu mkubwa kupitia kibao chake cha ‘Bodak yellow’, alisema ameshamfumania mumewe kwenye mahusiano ya nje ya ndoa zaidi ya mara moja.
“Nadhani imefika pahala inatosha, siwezi kusikiliza samahani zake na hakuna matumaini kwa sasa kama tunaweza kusuluhisha mgogo uliopo”, alisema Cardi B.
Mbali ya Cardi B, kuthibitisha kumfumania mumewe huo zaidi ya mara moja katika maisha yao ya ndoa, jambo jengine lililomuudhi ni hatua ya mumewe huyo kufanya ngono na wanawake hadi kufikia hatua ya kurikodi video.
“Siwezi kuishi na mtu asiye muaminifu, nimeamua kushika njia yangu na yeye afuate yake. Maisha yataanza tena na sio kuumizana roho kiasi hichi”, alisema Cardi B.
“Najijua kama mzuri, mrembo, nina fedha na utajiri, nina kipaji, lakini pia naweza kupata mwanmme yoyote nimtakaye awe mcheza mpira mcheza kikapu, ila sitaki maudhi”, alisema.
Cardi B, aliendelea kutoa povu kwa kumueleza Offset kwamba yeye sio mali yake kwamba anaweza kumchezea anavyotaka, hivyo kama binaadamu angependa sana heshima na sio jambo jengine.
Katika maisha ya sanaa, Cardi B ni mwanamuziki mwenye vituko na viroja na pia ni mtukutu kwa kiasi chake, kwani mwaka 2018, mwanamuziki huyo alidaiwa kuwalewesha wanaume ambao alipanga kufanya nao mapenzi.
Akisimulia stori hiyo, Cardi B, alisema kabla ya kuwa maarufu kwenye muziki akiwa mnenguaji katika kumbi za starehe, kundi la wanaume lilitaka kufanya naye mapenzi, hivyo alichukua hatua ya kuwalewesha na hatimaye kuwaibia fedha zao zote.
Mwanamuziki huyo wa miondoko ya rap alikosolewa baada ya video ya tukio hilo kurushwa mitandaoni ambapo alisema, ”Sijawahi kusema kuwa mimi ni msafi sana au natoka ulimwengu ulio mzuri sana”, alisema.
”Hakuna nilichokua napata. Hakuna,” alisema kwenye video hiyo, kabla ya kuweka wazi kuwa alikua akiwaalika wanaume kwenye hoteli kabla ya kuwanywesha na kuwaibia.
Akijibu shutuma hizo, aliandika kwenye ukurasa wa Instagram alieleza kuwa alikua akizungumza mambo ambayo yalikwishapita mazuri au mabaya ambayo yalinisaidia kuishi”.
Aliongeza:”Mimi ni sehemu ya utamaduni wa hiphop ambapo unaweza kueleza wapi umetoka, na hata mambo mabaya uuliyoyafanya kufika ulipo leo.”
Mshindi wa tuzo za Grammy pia alieleza kuwa kuna wanamuziki ambao wanasifu mauaji, vurumai, dawa za kulevya na wizi”.

Akiwa na umri wa miaka 19, Cardi B alianza kufanya kazi kama mcheza utupu au kujiambua, ambapo anasema alifanya hivyo kuepuka uhusiano wenye unyanyasaji na pia kupata fedha za kwenda chuo kikuu.
“Mara ya kwanza nilipocheza utupu, niliona aibu kubwa sana, nilihisi kama nasikia sauti ya wazazi wangu kichwani mwangu,” ameliambia jarida la ID mnamo 2018.
“Baada ya muda mrefu sikujali tena. Nilikuwa naona pesa ambazo nilihisi singewahi kuziona.” Anasema alipotimia miaka 21, alikuwa ameweka akiba ya takriban dola 20,000.
Lengo lake ilikuwa ni kuachana na kucheza utupu alipotimia miaka 25 na kuweka akiba ya kutosha kununua nyumba halafu aipangishe, hata hivyo aliachana na kazi hiyo ya kujiambua alipotimia miaka 23.
Kuanzia 2015 hadi 2017, Cardi B alikuwa akishiriki katika kipindi cha uhalisia kwenye televisheni kijulikanacho kama ‘Love & Hip Hop: New York, ambapo katika kipindi hicho anazungumzia mpenzi wake ambaye yupo gerezani na kazi yake katika sanaa ya muziki.
Aliachana na tamasha hilo mnamo 2017 kujishughulisha na muziki, alipokuwa akirekodi albamu yake ya ‘Invasion of Privacy’ Cardi aligundua kwamba ni mja mzito. Aliitoa albamu Aprili 6 mwaka 2018, ambapo walifunga ndoa ya siri chumbani mwao mwaka 2017.

Amekuwa rapa wa kwanza mwanamke kuibuka nambari moja katika Billboard Hot 100, katika muda wa miaka 20, lakini pia ameweka historia katika tuzo ya grammy kwa kuibuka msanii wa kwanza mwanamke wa kipekee kushinda tuzo kwa albamu bora ya mtindo wa rap, kwa albamu yake hiyo ‘Invasion of Privacy’.
Jarida la Forbes, limemuelezea Cardi B kama mmoja wa wanamuziki wanawake wenye ushawishi mkubwa kwa wakati wote hasa kutokana na kile anachokiimba kusambaa kwa haraka sana katika mitandao.
Inasemekana Cardi B ana uhasama mkubwa na mwanamuziki mwenziwe Nicki Minaj na wanamuziki hao hawana mafahamiano ya kutosha kiasi kwamba mnamo mwaka 2018 walitaka kuingiana mwilini.
Wanamuziki hao walikutana mjini New York kwenye hafla ya wiki ya mitindo, ambapo Cardi B alidhamiria kumpiga Nick Minaj kwa sababu ya kumzushia uongo aliokuwa anaeneza kuhusu yeye na mtoto wake.
Cardi ambaye hujiita ‘The Empress’ aliamua kuvua viatu vyake na kumvurumushia Nicki, lakini vyote havikumpata rapa huyo anayejiita ‘The Queen’. Katika sakata hilo Cardi B alipata uvimbe usoni baada ya kupigwa kiwiko na mtu ambaye alikuwa karibu na meza ya Nicki Minaj.
Jina lake halisi alilopewa na wazee wake ni Belcalis Marlenis Almánzar, ambapo alizaliwa Oktoba 11 mwaka 1992. Cardi B kama anavyojulikana na wapenzi na mashabiki wa muziki duniani ni mmoja kati ya wanamuziki mashuhuri wa kike nchini Marekani.
Alilelewa katika eneo la Brooklyn mjini New York. Mamake ni raia wa Trinidad na babake ni raia wa Jamhuri ya Dominica. Anasema wakati akikuwa, rafiki zake walikuwa wakimuita Bacardi na alilibadili jina hilo na kuishia kuwa Cardi B.
Cardi B, pamoja na kwamba anajulikana kama mmoja wa wanamuziki watukukutu na mtata, lakini sifa zake hizo kaziondoi uwezo wake mkubwa kwenye muziki hasa kwneye kura, kuandika mashairi na usoshalite kwenye televisheni.