Matukio ya vitendo vya udhalilishaji yamekuwa yakiendelea kuripotiwa ndani ya jamii zetu  licha ya juhudi kubwa zinazokuchukuliwa na Serikali pamoja na wanaharakari wanaopinga vitendo hivyo huku  waathirika wakubwa wakiwa ni wanawake na watoto.

Zipo sababu nyingi zinazoelezwa kukithiri kwa vitendo hinyo  ambavyo vinawaumiza vichwa wazanzibari hadi kufikia hatua ya kuitwa janga la kitaifa lakini ninavyoamini mimi, ukosefu wa ushahidi ni miongoini mwa chanzo cha masahibu yanayoikumba jamii yetu.

Idadi kubwa ya wahanga wanaofanyiwa ukatili wa kijinsia wamekuwa wakiathirika kimwili na kiakili  hali ambayo inatishia  kupotea kwa taifa letu la baadae  na kukosa nguvukazi imara  itakayosaidia kustawisha ustawi wa jamii yetu na taifa kwa ujumla  .

 Baadhi ya wazazi ambao watoto wao wamekumbwa na kadhia hiyo nao  huamua kunyamaza kimya na  kuficha uovu huo  kwa kuoneana muhali hasa muhusika mkuu wa kitendo hicho anapokuwa ni  mtu wa karibu na familia au mwenye dhamana fulani  huku wakimuacha mtendewa akiendelea kupata madhila yasiyokuwa na hatia .

Hali imekuwa mbaya zaidi katika vituo vya polisi na mahakama  baada ya   kesi nyingi zinazoriotiwa kushindwa kufikia  hukumu  kutokana na kukosekana  kwa ushahidi  hali inayochangiwa na  baadhi ya wananchi  kutokuwa na elimu juu ya umuhimu wa kutoa ushahidi, na wengine kutokuwa tayari kutoa ushahidi kwa kuoneana muhali.

Masuala ya rushwa katika  vituo vya polisi pamoja na  sheria ya ushahidi kuwa na vifungu  dhaifu   ambavyo bado vinahitaji marekebisho nazo ni baaadhi ya changamoto zinazorejesha nyuma juhudi za mapambano ya vita vya adhalilishaji wa kijinsia.  

Udhaifu huo umekuwa ukiendelea kutoa nafasi  kwa wahusika wa vitenzo hivyo kuendelea kudunda mitaani bila ya hofu huku wakidhani kuwa hakuna mkono wa sheria unaoweza kuwabana na kuwachukulia hatua zinazostahiki.  

Wakati Serikali ikiendelea kutafakari namna ya kukabiliana na janga la udhalilishaji Chama Cha Wanahabari Wanawake Tanzania TAMWA kwa upande wa Zanzibar kwa kushirikiana na Shirika la Action Aid Tanzania kupitia mradi wa kupinga vitendo vya ukatili kwa wananawake na watoto imeamua  kutoa elimu inayohusiana na masuala ua ushahidi wa kisheria   kwa wanachi.

 Baadhi ya sheria zilizowasilishwa na wanasheria pamoja na wanaharakati katika mikutano mbalimbali ya wananchi wa mkoa wa kaskazini unguja   ni sheria ya  ushahidi namba 9. Ya mwaka 2016 : ambayo ni  sheria kuu inayotumika katika masuala ya kutoa ushahidi katika Mahkama na polisi pale unapohitajika.

Sheria nyangine ni sheria ya mwenendo ya makosa ya jinai namba 7, ya mwaka 2018  ni sheria  kuu inayotoa muongozo katika kuendesha, kuchunguza na muendelezo wa makosa ya jinai

Sheria hizo na nyenginezo iwapo wananchi watazifahamu na kuzitumia ipasavyo  zitawasaidia  waendesha mashtaka,  Jaji au Hakimu   kutoa hukumu inayostahiki na  kupunguza wimbi la makosa ya  udhalilishaji.

 Kukataa kutoa ushahidi mahakamani unaohusiana na  matukio ya udhalilishaji pia kunapelekea kutokea adhari  mbalimbali za  kisheria , kiuchumi na kijamii ikiwemo kuendelea kwa  vitendo hivyo  na kukosekana kwa haki .

Iwapo mtu atakataa kutoa ushahidi mahakamani chini ya kifungu 115 cha sheria ya makosa ya jinai kinaeleza kuwa ikiwa mshtakiwa atakataa kwenda kutoa ushahidi, mahakama itatoa amri ya kukamatwa kwa kosa la kuidharau mahakama.   

 Kwa mujibu wa Sheria ya ushahidi kifungu 148 (2) kinaeleza kuwa  ikiwa mshtaki atatoa au kuwasilisha ushahidi wa uwongo atalazimika kufunguliwa shtaka au kutozwa faini.  

 Hivyo basi jamii inapaswa kuzingatia Umuhimu wa kutoa ushahidi mahakamani ili kusaidia kupatikana kwa haki ya wanaofanyiwa  udhalilishaji na  hivyo  kupunguza vitendo hivyo  ambavyo vinafanyika kinyume na silka na desturi za wazanzibari.

 Watendaji wa Serikali  na taasisi za kiraia zinazopigania haki za wanawake na watoto waendelee kutoa mashirikiano kwa jaamii kwa kuwapa miongozo ya masuala ya ushahidi sambamba na kuweka vituo maalum katika shehia vya kupokea taarifa za udhalilisaji.