KIGALI,RWANDA
MAHAKAMA ya Kati ya Nyarugenge imemuhukumu Robert Nyamvumba kifungo cha miaka sita gerezani baada ya kutiwa hatiani kwa ufisadi.
Nyamvumba ndiye aliyekuwa Meneja wa Idara anayesimamia nishati katika Wizara ya Miundombinu.
Alishtakiwa kwa kujaribu kuomba rushwa yenye thamani ya Rwf7.2 bilioni kutoka kwa mwekezaji wa Uhispania, Javier Elizalde.
Mtuhumiwa ambaye yuko mahabusu katika Gereza la Nyarugenge, Mageragere mawakili wake hawakuwepo Mahakamani wakati wa kutangazwa kwa uamuzi huo.
Akisoma uamuzi huo, jaji kiongozi alisema Mahakama ilitathmini uhalali wa mashitaka na iligundua kuwa kulikuwa na ushahidi wa kutosha kumhukumu Nyamvumba kwa ufisadi.
Kulingana na jaji, faini hiyo iliamuliwa kwa mujibu wa sheria, ambayo inasema kwamba faini kwa mtu yoyote aliyehukumiwa kwa rushwa lazima iwe mara tatu ya pesa inayohusika na shughuli ya ufisadi.
Kulingana na Mashitaka 2019, Elizalde, mwekezaji wa Uhispania, alishinda zabuni yenye thamani ya zaidi ya Rwf72 bilioni kuanzisha taa za barabarani kwenye barabara za Rwanda.
Mwanzoni mwa 2020, zabuni hiyo ilikuwa inasubiri kusainiwa ili kuanza utekelezaji wakati Nyamvumba alipiga simu kwa Mhispania huyo akiomba wakutane Kigali.
Kulingana na upande wa mashitaka,wakati wa mkutano huo, Nyamvumba alimwambia mwekezaji kwamba Ofisa wa juu katika Wizara ya Fedha na Mipango ya Uchumi (MINECOFIN) alitaka tume ya asilimia kumi ya jumla ya thamani ya zabuni ili kuharakisha mambo.
Mwendesha mashtaka alisema hapo awali, walipewa na Elizalde ambaye alitoa malalamiko hayo kwa viongozi wa Rwanda baada ya mkutano wake na Nyamvumba.