ZASPOTI
BINGWA mara sita, Serena Williams, alipambana kutoka mwanzo wa polepole kumchapa Mmarekani mwenzake, Sloane Stephens na kutinga hatua ya 16 bora ya michuano ya wazi ya Marekani.
Mwanadada huyo anayeshika nafasi ya tatu kwa ubora ulimwenguni mwenye umri wa miaka 38, alikuwa mvivu katika seti ya ufunguzi kabla ya kuongeza nguvu yake kushinda 2-6 6-2 6-2 dhidi ya mpinzani wake aliyepo nafasi ya 26 huko jijini New York.
Williams, anayelenga rekodi ya 24 ya Grand Slam, atakabiliana na Mgiriki Maria Sakkari ambaye yupo kwenye nafasi ya 15 kwa ubora.
Sakkari (25), alimshinda Williams katika seti tatu kwenye michuano ya Western and Southern Open wiki iliyopita.
Williams alijitathmini mwenyewe baada ya kushindwa na Sakkari, akisema kulikuwa ‘hakuna visingizio’ baada ya kuruhusu seti na kuongozwa kwenye mechi hiyo.
Sasa ana nafasi ya kulipiza kisasi haraka baada ya kuonyesha sifa zake za kupigana dhidi ya bingwa wa 2017, Stephens.
Wakati mchezo wa Williams bado haujafika karibu na viwango vya kuangamiza ambavyo vilishinda mataji yake 23 makuu, dhamira aliyoonyesha katika kubadili gia dhidi ya Stephens itakuwa imetuma ujumbe kwa uwanja wote.
“Katika seti hiyo ya kwanza sidhani alifanya makosa yoyote, alikuwa akicheza safi sana,” alisema Williams.
“Nilisema tu sitaki kupoteza kwa seti sawa, kwa sababu alikuwa akicheza vizuri,” alisema Williams, ambaye mara ya mwisho alishinda taji huko Flushing Meadows mnamo 2014.(BBC Sports).