NA MAULID YUSSUF,

WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Riziki Pembe Juma, amesema  Wizara hiyo inaendelea kufanya bidii kuhakikisha inazalisha Walimu wazalendo wa masomo ya Sayansi nchini, ili kupata wataalamu wazuri wa baadae.

Akizungumza wakati wa hafla ya kumpongeza Mwalimu wa Somo la hesabati kutoka Skuli ya FEZA ukumbi wa Wizara ya Elimu Mazizini mjini  Unguja, amesema kuwa jitihada ya  kusomesha  Wanafunzi  masomo ya sayansi kwa bidii pia kutasaidia sana  kupata Walimu wa masomo hayo wa baadae.

Riziki amewataka Walimu wa Skuli ya FEZA kuandaa mikutano maalum na Walimu wa Skuli nyengine ili kubadilishana mawazo  yatakayoleta  mabadiliko chanya katika Skuli zote za Zanzibar hasa ya ufaulu wa juu kwa masomo ya Sayansi.

Nae Naibu Katibu Mkuu Utawala na Uendeshaji wa Wizara ya Elimu, Mwalimu Abdullah Mzee Abdullah amesema mashirikiano mazuri baina ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar na Skuli binafsi ni miongoni mwa mafanikio makubwa  katika kuendeleza sekta ya Elimu nchini.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Skuli ya Feza Bwana Ali Nughu amesema  ili kuzidisha ari ya kusomesha  kuna umuhimu kwa Walimu wanaofanya vizuri katika masomo yao kupewa zawadi ili nao wahamasike katika  kutafuta mbinu mbadala za kusomeshea.