NA NASRA MANZI
KATIBU Mtendaji Baraza la Sanaa, Sensa, Filamu na Utamaduni Dk. Omar Abdalla Adam, amewataka wanavikundi binafsi vya Sanaa ikiwemo uchongaji Ufumaji, uchoraji , kujisajili kwa lengo la kulirahisishia Baraza kupata takwimu sahihi.
Akizungumza na Zanzibar leo ofisini kwake Mwanakwerekwe Unguja alisema kuwa na takwimu kutasaidia kujua idadi na mahitaji ya wasanii hao, kwa kuwaweka katika makundi kwa kuwasaidia na kuwahudumia kwa mujibu wa makundi yao.
Pia alisema takwimu zitasaidia wasanii kupata huduma bora kwa kila hali itakaporuhusu kwa ajili ya kuendeleza na kuinua Sanaa wanazozifanya.
Hata hivyo alisema usajili huo kwa wasanii binafsi utawaongoza kupata hati ya usajili , pamoja na wasanii waliosajili kwa vikundi, hivyo ni vyema vikundi kufuata utaratibu ulioekwa.
“Lengo letu baraza kuimarisha Sanaa kwa vikundi mbali mbali na kuwapatia maelekezo wasanii kwa mujibu wa sheria yetu ya baraza, lakini usajili katika vikundi vyao utawawezesha kufanya kazi kwa utulivu bila ya kubughudhiwa” alisema.