NA ABDI SULEIMAN
KIKUNDI cha Riziki Haina Mja cha Ole kinachojishughulisha na kilimo cha mboga, kimemshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, kwa kuwajali vijana.
Mwenyekiti wa kikundi hicho, Omar Hamad Aminia, aliyasema hayo wakati akitoa taarifa ya kikundi chao, wakati wa zoezi la uzinduzi wa uvunaji wa tungule kutoka katika green house za kikundi hicho.
Alisema kikundi chao kimepata mafanikio kutokana na juhudi zilizochukuliwa na serikali kupitia program ya vijana hali iliyofanya kujikita zaidi katika sekta ya kilimo.
“Licha ya kuwa na wizara yetu vijana lakini serikali hii ya awamu ya saba imetufanyia mambo makubwa hadi tumefikia hapa tulipo, vijana wenyewe sasa wako mstari wa mbele katika kujituma,” alisema.