HIVI karibuni wanajeshi wa Korea Kaskazini walifanya gwaride maalum ambapo mgeni rasmi kwenye gwaride hilo lililofanyika mjini Pyongyang, alikuwa kiongozi wa taifa hilo, Kim Jong-un

Madhumuni ya kufanyika kwa gwaride hilo, ilikuwa ni maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 75 ya chama cha wafanyakazi kinachotawala katika taifa hilo liliopo mashariki ya mbali.

Waandishi wakiwa nje ya nchi waliofuatilia hafla hiyo waliripoti kwamba sherehe hiyo iliambatana na maonesho ya makombora ya makubwa ambayo hayakuonekana yalioneshwa.

Hilo lilikuwa gwaride la kwanza na maonesho ya kwanza ya makombora nchini humo katika kipindi cha miaka miwili na inakuja wiki chache kabla ya uchaguzi wa urais wa Marekani.

Korea Kaskazini imejizuia kuonesha makombora ya masafa marefu katika gwaride tangu rais wa Marekani, Donald Trump na kiongozi wa taifa hilo Kim Jong-Un walipofanya mkutano wao wa kwanza mnamo 2018.

Kwa mujibu wa jeshi la Korea Kusini, gwaride hilo lilifanyika kabla ya alfajiri na sababu za kufanyika gwaride hilo muda huo bado hazijafahamika.

Aidha Korea Kusini ilisema kuwa kabla ya kufanyika kwa gawaride hilo, kiongozi wa taifa hilo Kim Jong-un aliitishwa mkutano wa dharura wa baraza la usalama la taifa kujadili suala la silaha za kuoneshwa sambamba na yaliyomo kwenye hotuba ya Kim Jong-un aliyopanga kuitoa.

Katika hafla hiyo ya Pyongyang hakuna vyombo vya habari vya kigeni au wageni waliruhusiwa kuhudhuria, kwa hivyo wachambuzi wanategemea picha zilizopigwa na vyombo vya habari vya ndani ambazo zinatolewa kutathmini gwaride hilo.

Miongoni mwa kombora lililooneshwa ni lile ambalo lilionekana kama la masafa marefu (ICBM) linaloweza kufika katika bara jingine ambalo ni kubwa kuliko kombora lolote la Korea Kaskazini.

Kwanza ilipitishwa kombora lililozinduliwa la nyambizi Pukguksong 4A, ikifuatiwa na kombora kubwa la Intercontinental Ballistic (ICBM) kwenye gari la kurushia na magari aina ya colossal ‘axles’ 11 mapya ambayo haijulikani yamepewa majina gani.

Kombora jengine lililoneshwa katika hafla hiyo ya miaka 75 ya chama cha wafanyakazi, linaonekana kama limefanyiwa mabadiliko ambalo linaweza kufyatuliwa kutoka katika nyambizi.

Wakati baadhi ya wataalamu wanasema   inaweza kuwa ni makombora ya mfano tu ambayo yanaendelea kufanyiwa kazi, kuoneshwa kwao hadharani kunaonesha kuwa Korea kaskazini inaendelea kusogea mbele katika kuimarisha uwezo wake wa silaha.

Wachambuzi waliofuatilia hafla hiyo iliyooneshwa mtandaoni wameona wanajeshi wakiwa na silaha mpya za mashambulizi, pamoja na kile kinachoonekana kama mifumo mpya ya ulinzi wa anga na gari za kivita.

Hata hivyo wanaeleza kuwa kusita kwa mazungumzo baina ya Marekani na taifa hilo, kunaongeza kasi kwa utawala wa Pyongyang kuendelea kutengeneza makombora.

Picha hizo ilimuonesha kiongozi wa taifa hilo, Kim Jong-un akiwa amevaa suti ya kijivu iliyoshonwa kwa mtindo wa magharibi, akipokea maua kutoka kwa watoto.

Katika hotuba, Kim alisema Korea Kaskazini itaendelea na jitihada zake za kujiimarisha kijeshi kwa lengo la kujilinda dhidi ya maadui wa taifa hilo.

Kiongozi huyo wa Korea kaskazini Kim Jong-un alionya  kwamba atatumia uwezo wake wote wa  kinyuklia iwapo atatishiwa  lakini aliepuka  kuikosoa  moja  Marekani.

Alisema pia anashukuru kwamba hakuna wakorea wa Kaskazini walio na maambukizi Covid-19. “Ninawatakia afya njema watu wote ulimwenguni ambao wanapambana na shida za virusi hivi viovu,” alisema.

Licha ya kudai kuwa nchi hiyo haina mgonjwa wa corona, Kim anaendelea kufanya mikutano ya kiwango cha juu kuhakikisha masharti ya kupambana na ugonjwa huo yanatekelezwa ipasavyo.

Wachambuzi wamesema haiwezekani kwamba Korea Kaskazini kuwa haijapata kesi za maambukizi ya virusi vya corona, hata hivyo inawezekana anachofanya kiongozi huyo ni propaganda. Hakukuwa na ishara ya mtu yeyote aliyevaa barakoa wakati wa gwaride.

Akizungumzia suala hilo, wizara ya ulinzi ya Korea Kusini imesema ina wasi wasi juu ya ukweli kwamba Korea Kaskazini imeonesha silaha ikiwa ni pamoja na zile zilizokuwa zinashukiwa kuwa makombora mapya ya masafa marefu.

Taarifa ya wizara iliitaka Korea Kaskazini kuendelea kuwa sehemu ya makubaliano ya pamoja ya Korea ya mwaka 2018 yenye lengo la kupunguza  uadui baina yao.

Wizara ya mambo ya  kigeni  ya  Korea  Kusini imetoa  taarifa tofauti  inayoitaka  Korea  Kaskazini  kurejea  katika  mazungumzo  ili kupiga  hatua  katika  nia yake  thabiti ya  kufikia kutokuwa na silaha za  kinyuklia na  amani  katika  rasi ya  Korea.

Baada  ya mkutano wa  dharura wa  baraza  la  usalama  la  taifa, wajumbe wa baraza hilo  nchini Korea  Kusini  walisema wataendelea  na  kufanya  tathmini mkakati  wa mfumo  wa  silaha wa Korea  Kaskazini  uliooneshwa  na kufanya  mapitio mapya  ya  uwezo wa  ulinzi  wa  Korea  Kusini.

Mahusiano kati ya Korea mbili yanaendelea kuwa  mabaya  huku kukiwa  na  mkwamo  wa  diplomasia  ya  kinyuklia kati ya Pyongyang na  Washington, hali inayoongeza wasi wasi katika eneo hilo.