SEHEMU YA PILI

Na Mohamed Mzee Ali, SUZA.

Ahlan  wasahalan. Bado nipo na  wanahabari kuhakikisha  kuwa tunaiva  katika chungu kimoja, ili kuepuka makosa  wanayoyafanya  katika lugha  ya  Kiswahili.

Huwa  nachukizwa  na  makosa  hayo, lakini sitachoka kuwasaidia wenzangu hao na  kutaka  waelewe kuwa  Kiswahili ni tunu kubwa kwao na  wanapaswa kukikienzi, kukipenda  na kukilinda.

Nikianza na kufuatilia  makosa   yanayofanywa  na  wanahabari wenzangu niliwasikia wakisema “ watu watano wamekamatwa  katika  msitu wa  hifadhi wakichana  mbao”.

Kiswahili fasaha na  sahihi mbao haichanwi bali hupasuliwa . Hii inatokana  na  kwamba mbao zinatokana  na magogo na  kawaida  magogo hupasuliwa na  kupatikana  mbao hizo.

Zamani kulikuwa  na  wimbo unaosema ‘seremala nipasulie  mbao walia kweche msumeno”. Kwa  maana  hiyo usahihi wa kauli iliyotolewa  na  wanahabari hapo awali ni kusema”watu watano wamekamatwa katika  msitu wa  hifadhi wakipasua  mbao”.

Nilimsikia  mwanahabari mmoja akisema” kwa  jina  naitwa Fulani bin Fulani”. Si sahihi katika  lugha  ya  Kiswahili kusema “kwa  jina naitwa”, bali mwanahabari huyo alitakuwa kusema “ jina  langu Fulani bin Fulani” au “naitwa  Fulani bin Fulani”.

Aidha, nilimsikia mwanahabari mwengine  akisema” kwa  majina naitwa Fulani bin Fulani”. Si sahihi kusema  hivyo hata  kidogo. Usahihi ni kusema “ naitwa Fulani bin Fulani”.

Waswahili wengi siku hizi wanaiga  tu kama kasuku wakiwemo wanahabari. Nilimsikia  mwanahabari mmoja anasema “mwisho wa  siku”. Katika  Kiswahili hatuna “mwisho wa  siku”. Kalima hii imechukuliwa katika   Kiingereza ambayo ni “at the  end of the  day”.

Kiswahili kina  hazina kubwa ya maneno na  wala si kama wanavyodhani baadhi ya  watu. Si vyema kutumia  maneno ya  wenzetu wakati ya  kwetu yapo. Hivyo, si vyema  kutumia  “mwisho wa  siku” na  badala  yake watumie “ hatimaye” au  “mwishowe”.

Nimemsikia  mtangazaji mmoja katika  redio ya  Taifa na  wala  sio FM akisema “Habari ya  wewe”. Niliguna na  kujisemea leo Mswahili anainanga lugha  yake  kama hivi? Si sahihi hata  kidogo kutamka alivyosema.

Kauli kama  hiyo ilinikumbusha nilipokuwa  nasoma Khartoum miaka  hiyo nilikuwa na  wenzangu kutoka  Uganda kama Hassan  Delu, Suleiman  Kisule, Suleiman Kasuja, Mudathir Ajotia nk. Hawa kwao ilikuwa  ni kusema  “habari ya  wewe” au “habari ya  kwako”.

Inashangaza kwa  mzawa  wa lugha tamu ya  Kiswahili kusema  hivyo kama  walivyokuwa  wakisema  marafiki zangu wa Kiganda. Jee ! kuna shida  gani kusema “ habari gani” au  hata “habari yako”?.

Imekuwa ni jambo la  kawaida  sasa kusikia  katika  ZBC na  redio nyengine kutamka  majina  ya  pahala  kwa  mfumo wa Kiingereza. Kwa  kweli inakirihisha.Mathalan, nilimsikia  mtangazaji akitangaza tangazo la  kifo kwa  kusema” kilichotokea Mnazimmoja  Hospitali”

Kutamka hivyo si sahihi katika  lugha  ya Kiswahili, bali alitakiwa  aseme “kilichotokea  Hospitali ya Mnazimmoja”. Sambamba na  hilo kuna wanaosema “Bububu Skuli” badala  ya “Skuli ya Bububu”  na  kadhalika.

Hivi sasa inaonekana  kuzoeleka kuwasikia baadhi ya  wanahabari wakitamka neno “mida” badala  ya  “muda”. Kwa  mfano  nilimsikia mtangazaji mmoja  akisema” kunako mida  ya saa sita tutakuwa  tena  hewani”.

Jamani Kiswahili kina  wenyewe. Hakuna katika  lugha  hiyo matumizi ya  neno “mida”. Neno linalotumika ni “muda” nalo ni kupima  urefu wa wakati. Mathalan, mtihani huu utakuwa  muda  wa  saa moja.

Mwengine kwenye FM fulani nilimsikia  akisema “lisaa moja iliyobaki”. Nikajiuliza huyu mtu wa  kabila  gani na  anazungumza lugha  gani?. Kama  Kiswahili hakisewmi hivyo, bali huwa  tunasema” saa moja  iliyobaki”.

Aidha,  mtangazaji utamsikia  akisema” zimebaki dakika 20 kutimia saa sita” au hivi sasa zimebaki dakika 20 kuendea saa sita”. Hiki si Kiswahili fasaha hata  kidogo. Usahihi wa  kutaja  wakati ni kusema “ Hivi sasa ni saa sita kasoro dakika 20”.

Salaale! Makubwa hivi sasa watangazaji na  waandishi wa  habari wamefikia  hadi kusema na  kutumia neno’ kuboa”. Neno hili si la  Kiswahili. Ni neno la  Kiingereza “Boring” au “bore” au “boredom”.

Neno hili maana  yake  ni “kuchosha” kwa  Kiswahili, lakini leo wanahabari wanasema “ anatuboa” badala  ya “anatuchosha”. Hivi karibuni nilisoma  gazeti la  Mwanaspoti liliandika “Simba haipoi wala  haiboi”. Hii ni hatari kwa  ufisadi huu unaofanywa  katika  lugha  ya Kiswahili.

Nililazimka kucheka. Kicheko si cha furaha, kwani sio kila kicheko ni cha  furaha bali chengine  huwa  cha  msiba na  fadhaa. Nilimsikia  mtangazaji mmoja  akisema” nilikuwepo sipo”. Si sahihi kusema  hivyo, bali alipaswa kusema  “sikuwepo”.

Mkabala  na kauli hiyo kuna  wengine utawasikia wakisema “nilipofika  nilimkuta  hayupo”. Hapa alitakiwa  kusema”nilipofika sikumkuta” au “nilipofika hayupo”.

Kadhalika  nilimsikia mtangazaji mmoja  wa FM moja akisema” alikuwepo hajui”. La haula! Kwanini asiseme “ alikuwa  hajui”.

Mpaka  nimefika umri huu au ni kwa  kuwa  ni mshamba, sijasikia  walionitangulia wakisema “Mdada”. Mdada kwa  lugha  ya watangazaji wa  siku hizi ni “dada”. Je kuna uzito gani kutamka “dada”. Utamsikia mtangazaji anasema” mdada wa  kazi” badala  wa “dada wa  kazi”. Pia  wengine husema “wamama” badala  ya “mama”.

Nimesikia  redio  moja katika kipindi chake cha michezo mtangazaji anasema”Timu A na  timu B  zimesare”. Kiswahili hatusemi hivyo, bali alipaswa kusema “Timu A na  Timu B zimetoka  sare”.

Kwa  upande  wa  matamshi ndio hatari. Wanahabari  wengi wajui lugha yao na  ni hatari sana kwa  mustakbali wa Kiswahili. Mara kadhaa huwa  nawasikia  watangazaji na  waandishi wakisema” salasini” badala  ya “thalathini”, “samanini” badala  ya “thamanini”.

Aidha, nimeona maneno yameandikwa katika magazeti kama “kudhorota” badala  ya “kuzorota”,”hafla”   badala  ya “ghafla”. Mfano  Makamu wa Pili wa Rais alifanya ziara  ya “hafla” ZRB badala  ya “ghafla”. Pia wengine  kuandika “gafla” badala  ya “ghafla”.

Neno “hafla” ni sherehe  maalum. Mfano hafla  ya kutunuku  vyeti. Na “ghafla” ni tukio la  kuzuka lisilotarajiwa. Mfano alifariki ghafla.

Kuna msamiati umezuka  hivi karibuni katika tasnia  ya  michezo ambao ni “ amecheza sivyo ndivyo au ndivyo sivyo”. Kiswahili hakina msamiati huo bali ni kusema  tu “amecheza sivyo”.

Maneno mengine niliyowasikia  wanahabari wakivuruga  ni “Haizuru”badala  ya “haidhuru”, “haina  zara” badala  ya “haina dhara” na  “amevaa zahabu” badala  ya “amevaa dhahabu”.

Aidha , nilimsikia mtangazaji mmoja anasema” amejipamba kwa  dhahabu kedekede”. Matamshi kama  haya si sahihi bali alipaswa kusema” amejipamba  kwa  dhahabu kochokocho”.

Nimegundua  kuwa waandishi na watangazaji wanafanya  makosa  makubwa katika  matumizi ya maneno mawili ambayo ni “baada” na  “badala”. Mara  nyingi pahala  pa badala hutumia  baada na kinyume  chake.

Mathalan, watangazaji wa mpira “ ameingia mchezaji Khamis Ndemla baada  ya Joash Onyango”. Hapa alitakiwa atumie  neno badala na  sio baada.

Nimesoma  gazeti moja litolewalo nchini limeandika”ngono ni haki ya faraha baina  ya mke  na  mume”. Kauli kama hii ni makosa  makubwa  katika Kiswahili, bali  alipaswa kuandika”Ngono ni haki ya  faragha baina  ya  mke  na mume”. Kwa  maana  hiyo Kiswahili ni faragha  na wala  si faraha.

Cha  ajabu na  ni ajabu. Nilimsikia  mtangazaji mmoja anatamka “vyupa” ikiwa  ni wingi wa “chupa”. Jee! Mtangazaji kama  huyu anafaa kuwa mwanahabari  wa kuuelimisha  umma wakati uwezo wake  wa lugha  ni hafifu? .Hasara.

Matamshi mabovu kwa  watangazaji hayakuishia kwa  yaliyotangulia, bali nimewasikia  pia wakitamka “zana” badala  ya  “dhana”, “zarau” badala  ya  “dharau”, “samani” badala  ya “thamani” na  kadhalika.

Cha  kushangaza  zaidi mwanahabari mmoja nilimsikia  akitamka  neno “hadisi” badala  ya “hadithi” huku akiwa  hana  habari kabisa kuwa  anakiuka  maadili ya  nchi kwa  kutukana. Yote hayo ni kwa  kuwa  masikini hajui lugha. Lakini , alipaswa kuutumia msemo “kama huyajui uliza  wenzio”.

Nilisoma gazeti moja  nalo mhariri hakuwa makini kutoa  makosa. Aliliacha  neno “tene” badala ya “tena”. Maneno haya yana  tafauti kubwa baina  ya mbingu na  ardhi. Kwa  hakika neno “ tene” siliwezi kulitamka mbele za  watu au kuliandika. Hivyo, wanahabari kaeni na wataalamu wa lugha  kujifunza  kwao.

Erevuka  na shairi lifuatalo:

                   LUGHA BWANA !

Ukitaka ufaidi                     Lugha uwe ni mweledi

Usifanye ukaidi                   Tuliza yako fuadi

Maana hujijadidi                         Na neno likashitadi

Lugha bwana !

Karibuni mukale                 Musidhani kufaidi

Musidhani wali tele             Kitoweo na kadidi

Ila jalasa ukale                   Ubarizi makusudi

Lugha bwana!

Na mchele upotele              Usidhani wafaidi

Kwamba madukani tele       Kumbe kwao ubaidi

Kauli hiyo kelele                  Njaa imepiga hodi

Lugha bwana!

Karibu kwetu Uzini              Si kufanya ufisadi

Ni kijiji cha Uzini                 Ndio hasa makusudi

Si tendo la kishetani           Adhabu yake ni hadi

Lugha bwana!

Kusema ‘nnavitako’             Si shutuma na inadi

Bali apita uliko                    Ufahamu makusudi

Kikae kwao ni huko             Kusini ni yao jadi

Lugha bwana!

Hili neno kusokota              Si kamba ilo jadidi

Wala sembe kusokota         Kuwana kwa makusudi

Mwanamke kukamata         Kinguvu na hana budi

Lugha bwana!

Pia kupiga ukotwa              Nguvu sheti ishadidi

Mwanamke husokotwa        Ridhaa kwake baidi

Ni kubaka kwa kuitwa                 Lugha iliyojadidi

Lugha bwana!

Mohamed Mzee Ali (Tere), SUZA.

Mwisho.