Mchango wa Kihindi katika  lugha  ya Kiswahili

Na Mohamed Mzee Ali(Tere), SUZA

Lugha ya  Kiswahili pamoja  na kutolewa  nadharia  kadhaa kuhusu lugha  hiyo kama Kiswahili ni Kiarabu, Kiswahili ni Kibantu na  Kiswahili hakina  mwenyewe bali ni lugha ya  watu wote, lakini ukweli unabaki kuwa Kiswahili ni lugha  nzuri yenye  kujitegemea  kwa kila  kitu.

Hata  hivyo, kama zilivyo lugha  nyengine  duniani, Kiswahili kinakua na  kupata   baadhi ya  msamiati kutoka  lugha  nyengine kadhaa  za  dunia. Miongoni mwa  msamiati uliomo katika Kiswahili kutoka  lugha  nyengine  ni  ule  wa lugha  ya Kihindi.

Kwa  mujibu wa  historia, msamiati wa  Kihindi katika  lugha  ya  Kiswahili uliingia  baada  ya  kuja  Wahindi wengi Zanzibar kwa  biashara na  hatimaye kufanya  mastakimu yao hapa.

Sultan  wa  mwanzo wa  Zanzibar Seyyid Said Bin  Sultan alipofanya   makaazi yake  ya  kudumu hapa  Zanzibar badala  ya  Oman mnamo mwaka 1832, alimuajiri Muhindi mmoja maarufu aliyeitwa Taaria Topan kuwa  Mkusanyaji Mkuu wa  Kodi katika  biashara zinazofanyika  hapa Zanzibar.

Kufuatia  kuja  kwa  Muhindi huyo,  wahindi wengine  walianza  kuingia  kwa  wingi kwa  madhumuni ya  biashara za  aina  mbali mbali na kisha kufanya  mastakimu yao hapa Zanzibar hasa  katika  eneo la Shangani katika  Mji Mkongwe  wa Zanzibar.

Katika muamala  wa  kibiashara  wahindi wakiwa  na  lugha  yao, msamiati wao mwingi ilibidi kuingia  katika  Kiswahili ili biashara iendelee vizuri na  kujenga  mafahamiano na   Waswahili waliokuwepo wakati huo.Lugha hizo za kihindi ni pamoja  na Urdu, Gujirati, Hindi nk.

Mara nyingi biashara huendeshwa  kwa  sarafu na  ikasadifu kuwa  kwa  vile Zanzibar ni kitovu cha  biashara, sarafu mbali mbali zikaanza  kutumika. Mathalan, wahindi walikuja  na  Rupia ambayo ni sarafu ya  India na  kutumika pia  Zanzibar.

Sarafu ya  Rupia  iliingia  katika lugha  ya  Kiswahili na  ndio maana ukaja  msemo “Penye  Udhia penyeza  Rupia” yaani  udhia  na  matatizo hutatuliwa  zaidi kwa  njia  ya  pesa.

Neno Pesa nalo pia  lina  asili  ya  Kihindi kwa  hapa  kwetu Zanzibar.Mara  nyingi Wahindi walikkuwa  wakisikika wakisema “Peisa Nehi .Chakatarega?” . Maana  ya  kauli hiyo ni kwamba” Sina  pesa . Nifanye nini?”. Kwa maana  hiyo Wahindi ndio walioliingiza  neno hilo katika   Kiswahili.

Wakati biashara Zanzibar wakati huo imeshika  kasi, bandari ya  Zanzibar ilijipatia  umaarufu mkubwa  na kuwa  kituo kikubwa  cha  biashara Afrika  Mashariki.

 Bidhaa mbali mbali ziliiingia na  nyengine kutoka kama vile  karafuu, mbata , pilipili hoho na  viungo, ambapo kuliibuka ajira  ya watu kubeba mizigo bandarini hapo.

Wahindi walikuwa  wanawaita wabeba mizigo hiyo hapo bandarini kwa  jina  la Khuli na  hapo ndio jina  Kuli kwa  maana  ya  wabeba  mizigo bandari likaanza kutumiwa.

Neno hili Kuli limesadifu kuwa na maana  sawa  na maneno kama mpangazi, mchukuzi na  hamala.

Aidha, bila  shaka katika  biashara fedha  ni lazima  ihesabiwe.Wakati huo  ilikuwa  si sana  watu kuhesabu kufikia  milioni, bilioni  na  kadhalika kama  ilivyo sasa. Fedha nyingi ilikuwa  katika Mamia  na Laki.

 Kwa  bahati Wahindi  walihesabu hadi kufikia Lakh . Sasa neno hili likaingia  katika muamla  wa fedha na  kubakia   katika  Kiswahili Laki yaani 100,000. Kiingereza  hakuna  neno Laki.

Vyombo vya  usafiri navyo viliingia  Zanzibar na  miongoni mwa  hivyo ni magari. Gari zilizokuwa  maarufu ni hizi ndogo ambazo kwa  Kiingereza zilifahamika  kwa  car au motor car.

Waswahili  waliviita  vyombo hivi  vya  usafiri kwa  jina  la ‘Mutukari’ au ‘motokaa’. Hata  hivyo, maneno haya hayakushika   kasi sana  labda kutokana  na kutamka kwake  kuwa kugumu kidogo na  kutumika zaidi “car”.

Kwa  vile  wahindi  mara  nyingi hawatamki Kiingereza  sawasawa, bali hutawaliwa  zaidi na matamshi ya  Kihindi , neno ‘car’  wakawa  wanatamka ‘gar’. Kwa  maana  hiyo neno hili likashika  kasi na kuwa  ‘gari’.

Waswahili wana msemo usemao “ usinifanye  punda  wa  dobi”. Msemo huu una maana  kwamba usimbebeshe mzigo mkubwa ukadhani kuwa  ni mwepesi wakati ni mzito.

Msemo huu unatokana  na  kwamba zamani walipokuja  Wahindi kulikuwa  na watu waliokuwa kazi yao kufua  nguo kwa  kibarua  na  kupiga  pasi. Kazi hii ilianzishwa  na  Wahindi wale  ambao kipato chao ni cha  chini.

Wahindi hao walijulikana  kwa  jina  la ‘DOBI’ na  walikuwa  wanawatumia  punda kubeba  nguo  nyingi na  kupeleka sehemu za mafulio kwa  kufuliwa. Hivyo, neno ‘Dobi’ linatokana  na  Kihindi.

Itakumbukwa  kuwa  vazi la  Kanga lilianzishwa  na  Wahindi na  ndio waliokuwa wachapishaji wakubwa  wa vazi hilo. Ukisikiliza  hotuba  ya Marehemu Mzee Karume alisema ‘kuanzia  Mlandege hadi kwa  Hajitumbo kote  kulikuwa  kunauzwa  kanga’.

Wakati huo  na  hadi leo kanga ilikuwa  inauzwa  kwa  pande  mbili na  wahindi waliita ‘Dhoti’. Neno hili lilitumika na  kushika  kasi na kutumika hadi leo kama “Doti”. Na  ndio maana  watu husema  nipe doti moja  ya  kanga.

Aidha ,katika  Kiswahili kuna kivumishi “ Bora”. Neno hili nimeliangalia  sana  na  halimo  katika lugha  za Kibantu wala   Kiarabu. Nilipotafiti zaidi nikagundua  la  Kihindi kwa   kuwa  neno ‘Bora’ linatokana  na lugha  ya  Kihindi na  kusadifu kulisikia  katika filamu za Kihindi.

Kadhalika  nimesadikisha  kuwa  neno hilo ni la  kihindi kwa  kuwa  niliwahi kufanyakazi na  Muhindi mmoja wa  Kampuni ya  Transpapers ya Dar es Salaam nilipokuwa Wakala  wa Uchapaji Zanzibar akiitwa  Mr. Bora.

Kama nilivyotangulia  kusema  kuwa Wahindi walikuwa  ni wafanyabiashara  wakubwa  wakati huo. Waliingia  katika  kila  biashara hata kuku wa  kinyeji. Ilisadifu siku moja mtu mmoja  kutoka  Bambi alimuuzia Muhindi kuku kumbe  ndani yake  mna   matipitipi wengi kuliko kuku wa  kienyeji.

Baada  ya muda  kupita  ulipofika muda  wao watipitipi yakalia na   muhindi kusema “ mshamba  jinga  sana”.

Wahindi pia  kwa  wakati huo  ndio waliokuwa  wafanyabiashara  wakubwa  wa dhahabu na  fedha. Kwa lugha  ya Kihindi wafanyabiashara hiyo walijulikana  kwa  jina la“Sonara” . Jina  hilo moja  kwa  moja likaingia katika  Kiswahili hadi leo.

Kadhalika, wahindi  pia  walikuja  na biashara ya  kudhamini vitu kama  nyumba , mashamba  na  kadhalika huku anaedhaminiwa akilipa ada fulani kwa  muda maalum. Biashara  hii ilijulikana  kwa  jina la “Bhima”.

Neno hili “Bhima” liliingia  katika lugha  ya  Kiswahili ambalo hivi sasa ndio “Bima”, ambayo hukatiwa biashara, vyombo vya moto na  kadhalika.

Hivi sasa watu wengi utawasikia fulani kaandikiwa  Cheki ya  shilingi 500,000. Neno ‘Cheki’ ni la Kiingereza ‘Cheque’, ambayo ni karatasi maalum inayoandikwa kiasi cha  fedha kumlipa  mtu kwa  kuivunja  benki.

Ukweli neno hili si la  Kiswahili, bali neno lililokuwa  linatumika asili ni ‘Hundi’. Neno hili asili yake  ni lugha  ya  Kihindi na likaingia  katika muamala  wa kifedha  katika  lugha  ya Kiswahili.

Zamani wakati  Wahindi wameshika  kila  aina  ya  biashara, kulikuwa  na biashara  ya kuuza  nguo kuukuu pia. Biashara  hii ilijulikana kwa  jina  la “Poni”. Neno hili lilitumika  sana, lakini hivi sasa biashara  hiyo inajulikana  kwa  jina “ mitumba”.

Ukweli ni kwamba lugha  ya  Kihindi  imeliingiza  neno hilo ‘poni’ katika  msamiati wa Kiswahili ingawa siku hizi limepuuzwa.

Katika  Kiswahili watu wanaofanya  hujuma  ya kuwaua wanyama  katika  hifadhi wanajulikana  kama ‘majangili’. Neno hili ‘jangili’ halina  asili ya lugha  za kibantu  wala Kiarabu kama  ambavyo maneno mengi  yanafahamika  etimolojia  yake. Hivyo, neno hili asili yake  ni  Kihindi na  utalisikia  sana  katika Senema  za Kihindi.

Mtu anaenyang’anya  mali za  watu kwa  nguvu na  hata  kutumia  silaha hujulikana  kwa  jina la  ‘jambazi’. Neno hili nalo asili yake  ni Kihindi na  limeingia  katika  msamiati wa Kiswahili baada  ya Wahindi kuishi hapa Unguja  kwa   miaka  kadhaa. Hata  hivyo, neno ‘chori’ kwa  maana  ya  mwizi nalo hutumika   ingawa  si sana.

Kwa  kawaida Waswahili wana  tabia  ya kutandika pahala  pa  kulala. Pahala  hapo hutandikwa  kwa  kifaa kinachoitwa ‘tandiko’. Hapo zamani tandiko hutengenezwa  kwa usufi na  usumba.

Kadiri siku zinavyokwenda  na  mambo hubadilika. Yamekuja  matandiko ya  kisasa yanayojulikana  kwa  jina  la’ magodoro’.

Neno ‘godoro’ halina asili ya Kiswahili, bali ni msamiati unaotokana  na Kihindi  na  kwa  muktadha  huo ‘godoro’  limechukuliwa kuingizwa  katika Kiswahili kutoka  lugha  ya   Kihindi.

Kuna  Waswahili wengine hadi leo wanatumia neno ‘furniture’ wanapotaka  vifaa  vya  nyumbani vinavyotengenezwa  kwa  mbao kama kitanda, kiti , meza, makochi nk.

’Samani’ kwa  maana  ya  vifaa  vilivyotajwa  awali, pamoja  na kutumika  neno hilo, lakini halitokani na lugha  za kibantu, bali   asili yake  hasa  ni Kihindi na  hasa  katika  lugha  ya ‘Urdu” inayozungumzwa  zaidi Pakistan  na Bangladesh.

 Neno hili limeingia katika msamiati wa  Kiswahili kutoka  lugha  hiyo walipokuja  wahindi.

Siku hizi utawasikia  watu hasa wanawake  na  wapambaji harusi kuwa tunataka  ‘shela’ ya  kuburura   katika  nguo ya harusi. Harusi za  Kiswahili hazikuwa  na nguo za  aina  hiyo, bali  zilitosha  kanga  za kisutu.

Hili neno ‘shela’ kwa  maana  ya kipande  cha  juu kinachokuwa  kichwani  katika  nguo za  siku hizi za  harusi, limeingia  katika  msamiati wa Kiswahili kutoka  Lugha  ya  Kihindi.

Zamani manukato au uturi ulikuwa  unapimwa vipimo maalum kabla  ya  hivi sasa kuwemo katika chupa  ndogo ndogo na  za kupuliza. Vipimo hivyo vilijulikana  kwa  jina  la “Tola”. Akinamama  walipimiwa katika  vichupa  vyao walivyokuwa  wakiwasilisha muuzaji.

Hili neno ‘Dukani”  lililomo katika   lugha  ya Kiswahili, nimelikuta  katika lugha kadhaa. Neno hili ukiangalia  katika  lugha  ya  Kiarabu unalikuta halkadhalika katika  Kihindi kwa jina  la’ Dukan’.  Kwa  muktadha  huo neno hili ‘dukani’ linatokana  na lugha  hizo mbili.

Sambamba  na  hilo  neno “Dunia” ambalo limo ndani ya  Kiswahili pia  linapatikana  katika Kihindi’Dun’ya’ na  pia Kiarabu. Sasa  nani mwenyewe neno hili linahitaji utafiti, lakini takriban   lugha  zote  duniani zinategemeana.

Katika mapishi huko ndio usiseme. Kiswahili kimepata msamiati mwingi sana kutoka  lugha  ya  Kihindi. Msamiati huo ni pamoja  na Biriyani, Pilau(pullao), ladu (ladoo), bajia, kachori, achari, chapati(mkate  wa kusukuma) nk.

Pia katika Kiswahili kuna neno ‘pwani”. Neno hili kuna  wasiwasi mkubwa huenda  likawa linatokana  na lugha  ya  Kihindi. Ninasema  hivyo kwa  kuwa katika lugha  ya  Kihindi maji yanaitwa ‘pani’.

Kwa  muktadha  huo inawezekana neno pwani ambako kuna  maji mengi ya  bahari wakaona waite ‘pwani’ kutoka  neno ‘pani’ lenye  maana  ya  maji kwa  Kihindi. Hata  hivyo, utafiti zaidi wa etimolojia  ya  neno  unahitajika.