NA ASYA HASSAN

MKUU wa Mkoa wa Kusini Unguja, Rashid Hadid Rashid, amewasisitiza   madaktari na wauguzi wa vituo vya afya kufuata sheria na taratibu za kiutendaji wa kazi zao kwa lengo la kutoa  huduma bora kwa wananchi.

Alisema lengo la serikali ni kuimarisha huduma za afya hasa za mama na mtoto, ni kuona wananchi wanapata huduma zinazostahiki bila ya usumbufu.

Mkuu huyo, alifahamisha kwamba si jambo la busara kuona baadhi ya wahudumu wanakwenda kinyume na sheria na maadili ya kiutendaji hali ambayo inapelekea kuleta malalamiko na kuitia doa serikali.

Aliyasema hayo wakati alipofanya ziara  ya kushtukiza katika vituo  vya Uzini, Bambi na Umbuji, ili kuona utolewaji wa huduma kwa wananchi pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili  watendaji wa vituo hivyo.

Akizungumzia kuhusu suala la wafanyakazi kufunga kituo cha afya Bambi,  alisema serikali  haikuridhishwa  na  suala hilo na kuzitaka mamlaka zinazohusika  kuwachukulia hatua  za kisheria  wahusika wa suala hilo.

Kwa upande wa baadhi ya  wahudumu na madaktari wa vituo hivyo walisema wanakabiliwa na  uhaba wa wafanya kazi pamoja na posho la likizo  na kutopata huduma ya  maji hasa katika vituo  vinavyotoa huduma  za mama na mtoto.

Mkurugenzi wa Baraza la Mji Kati, Mohammed Salum Mohammed, aliwashauri wakuu wa vituo kuwa changamoto zinazojitokeza katika utendaji wao isiwe  ni kigezo kukwamisha upatikanaji wa huduma  kwa wananchi.