NA HALIMA JUMA

MKUU wa Wilaya ya Chake Chake, Abdallah Rashid Ali amesema serikali imekusudia kuondoa matabaka, ili kujenga usawa kwa jamii. Aliyaeleza hayo ofisini kwake Chake Chake, wakati akizungumza na watendaji wa Wizara ya Afya kisiwani hapa.

Alifahamisha kuwa  haipendezi kuona baadhi ya watumishi wanatumia vyeo au jina la mkubwa kufanikisha mahitaji yao kinyume na utaratibu. Aliwataka watumishi kuheshimu sheria na kanuni za
utumishi wa umma katika utekelezaji wa majukumu yao, ikiwa ni pamoja na utayari wa mtumishi kufanya kazi popote anapopangiwa.

“Fanyeni kazi kwa kufuata sheria na kanuni za utumishi wa umma wakati mnapotekeleza majukumu yenu, kwani mlipojaza mikataba mlikiri kufanya kazi sehemu yoyote ile,”alisema.

Alisema ni vyema  wizara ya afya kuweka utaratibu wa kusomesha watendaji wao ambao hautoathiri shughuli za kawaida za utoaji  huduma kwa jamii.
Aliwataka wasimamazi wa vituo vya afya kutoa huduma bora kwa wazazi ili kupunguza vifo vya mama na watoto.

Aidha alisema iwapo  vituo vya afya vitawajibika ipasavyo, vitatoa fursa kwa hospitali kubwa kupunguza maradhi yanayosababishwa na mikusanyiko ya watu wengi.

Kwa upande wao madaktari walisema uhaba wa wafanyakazi, vitendea kazi ikiwemo dawa na vifaa tiba, mazingira ambayo sio rafiki kwa kufanyia kazi, ukosefu wa ada za kujilipia masomo, pamoja na ukosefu wa stahiki zao, ni mambo yanayowavunja moyo katika utekelezaji wa majukumu yao.
Hivyo waliutaka uongozi wa wizara ya afya kupitia
katika hospitali na vituo vya afya, kwenda kusikiliza changamoto  za wafanyakazi.