RUKWA
MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo, amemuagiza Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoani humo kuhakikisha anafanya msako wa Kijiji kwa Kijiji kuwasaka na kuwakamata waganga wa kienyeji wanaopiga ramli chonganishi maarufu kama “Lambalamba”.
Hatua hiyo ya Mkuu wa Mkoa inakuja baada ya kundi hilo kuonekana wanafanya makosa ya kuwadanganya wananchi, kuwadhulumu pesa zao na hatimae kuwaacha wakiendelea kuwa masikini.
Aidha, Wangabo amesema kuwa nchi hii haiwezi kuendeshwa kwa Imani za kishirika ambazo zinarudisha nyuma juhudi za wananchi katika kujikwamua na umasikini.
“Hivyo nakuelekeza Kamanda wa Polisi kukiweka chini ya ulinzi Kijiji chochote kitakachoonekana kinawaficha waganga hao ama kutotoa ushirikiano kwa jeshi hilo” alisema Mkuu huyo wa Mkoa.
Amesema kuwa anawashangaa wazazi wanaoshindwa kuwahudumia Watoto wao mahitaji ya shule ili wapate elimu na matokeo yake anatumia pesa hiyo kumpatia mganga huyo ili aweze kumsafishia mji wake.
Alieleza wazazi na wananchi wanaofanya vitendo kama hivyo wamejiroga wenyewe kwa kushindwa kujitambua.
“RPC anzisha msako kamata hawa lambalamba wote, bonde la Ziwa rukwa kuanzia kule chini (Kijiji cha Kasense) mpa kule (Kijiji cha) Kilyamatundu (umbali km 174) kote saka na huku juu saka, kila unayesikia kamata, hatuwezi kuendesha nchi namna hii kwa Imani za kishirikina, haiwezekani, kama kuna kijiji ambacho kinazuia zuia, kama Kijiji chote weka ndani, ninaagiza Kijiji chote kamata weka ndani, hatutaki ujinga, tutakizingira Kijiji hicho hakitoki kitakuwa chini ya ulinzi, tutakiweka chini ya ulinzi juu na chini,”Alisisitiza.
“Mnazidi kuwa masikini mnajiletea umasikini na wao walishajua kuwa ni wajinga haw ana wajinga ndio waliwao, wanakuja huku wanasema leta hela na wewe unatoa hela wakati unamahitaji ya msingi, nyumba yako familia yako umeitelekeza halafu unampelekea lambalamba hazikutoshi wewe, unapaswa hata kuombewa kabisa,” Alisema.
Wangabo ametoa maagizo hayo baada ya mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Dk. Khalfan Haule kutoa taarifa ya matukio hayo katika Kijiji cha Malonje, Kata ya Mollo ambapo llimefanyika tukio la upandaji wa miparachichi 100 katika Shule ya msingi ya Kijiji hicho katika maadhimisho ya undaji wa miti kimkoa ambayo hufanyika kila tarehe 19 ya mwezi wa kwanza.
Wakati akitoa taarifa hiyo Dk. Haule alisema kuwa pamoja na kuwa “Lambalamba” hao hawajafika katika Kijiji hicho cha Malonje, lakini kuna kamati ambazo zimeanza kuundwa kwaajili ya mapokezi ya hao “Lambalamba” pampoja na kuwachangisha fedha wananchi ambao wanatumia fedha zao ambazo zingewafaa kwa ajili ya maendeleo yao na maendeleo ya Kijiji chao.
Katika Maelezo yake hayo Dk. Haule aliongeza kuwa Waganga hao wanapitia kwenye ofisi za Matawi za Chama cha Mapinduzi (CCM) kupitisha fomu zao na kuwasainisha wananchi na kuwachangisha kuanzia Shilingi 10,000/=, 300,000/= hadi Milioni Moja.
“Fedha kwaajili ya maendeleo yao Wananchi kwa mfano kupanda miti, watakwambia hawana lakini fedha kwaajili ya kumleta Lambalamba hapa kila kaya itatafuta, uongo kweli? Watatafuta, kama hana atauza ng’ombe, atauza mbuzi, juzi walipita kule (Kijiji cha) Mawenzusi, Mwenyekiti wa tawi wa Chama cha Mapinduzi, balozi na Mwenyekiti wa kitongoji ndio waliowakaribisha, tuliwakamata” alisema.
Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa Ndg Enos Budodi amesema kuwa hatawapokea wala kuwapa ushirikiano viongozi wote wa CCM watakaojihusisha na kuwapokea “Lambalamba” hao.