NA FATUMA KITIMA ,DAR ES SALAAM
WAZIRI wa Habari ,Utamaduni, Sanaa na Michezo Innocent Bashungwa, amesema kuwa lengo la Serikali kuweka mazingira wezeshi ili vyombo vya habari vikue na kuendelea kutoa mchango chanya kwa nchi.
Aliyasema hayo jana jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa kati ya TCRA Wamiliki wa Vyombo vya Habari , wamiliki wa Visimbuzi, Bodi ya Filamu, Cosota pamoja na Basata.
Bashungwa alitoa wito kwa vyombo vya habari kuendelea kusimamia sheria, kanuni ,Sera, mila ,desturi na tamaduni.
“Mkifanya hivyo kila mmoja wetu kwa nafasi yake hamtosikia Serikali inafungia chombo chochote kwasababu lengo ni kujenga ustawi na sio kubomoa”alisema
Pia alisema kupitia tasnia ya Sanaa inaweza kuongeza pato la taifa na kukuza uchumi wa ndani ya nchi.
Bashungwa alisema Serikali imetambua kuwa tasnia hiyo ina uwezo wa kuchagua kipato na ajira kwa vijana.
Alibainisha kuwa utekelezaji huo ni moja ya kuunga mkono serikali ya awamu ya tano katika kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi ya uchumi wa kati wa viwanda.
Hata hivyo, alieleza kuwa katika tasnia hiyo kuna vipengele vingi ikiwemo, Habari, Utamaduni pamoja na sanaa ambazo zote ni uwekezaji mkubwa nchini..