NA FAT-HIYA MOHAMED

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali yake itaendelea kushirikiana na wadau mbali mbali wa maendeleo, ili kuhakikisha malengo ya uchumi wa buluu yanafikiwa.

Akizungumzia kwa niaba yake, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Simai Mohammed Said, wakati wa sherehe za uwekaji jiwe la msingi na ufunguzi wa majengo ya Skuli ya Assalam iliopo Kizimkazi  Mkoa wa Kusini Unguja,  amesema kufikia malengo  ya maendeleo kunahitaji kushirikiana na kila mdau wa maendeleo hasa katika sekta ya elimu .

Amesema Serikali ya awamu ya nane itaendelea kuwa karibu na wawekezaji  wa maendeleo kwa kuwaelekeza namna ya kufata  miongozo mbalimbali bila ya kuvunja sheria ili kufikia malengo.

Said amesema  Skuli za kijamii nazo ni miongoni mwa vyanzo vizuri vya maendeleo katika jamii,  hivyo Wizara ya elimu itaendelea kuwa pamoja nao kwa kuwapa muongozo ya sera ya elimu ya Zanzibar, ili kwenda sambamba na utoaji wa elimu kwa wote.

Amesema   uongozi wa Assalam umefanya jambo zuri kuhakikisha wanawekeza katika sekta ya elimu  na ujasiriamali vijijini, kitu ambacho kitawapelekea wanakijiji kujiajiri wenyewe kutokana na ujuzi waliopatiwa.

Mkuu wa Wilaya ya Kusini , Rashid Makame Shamsi,  amesema ataendelea kusimamia maendeleo ya Wilaya yake hasa katika sekta ya Elimu, kwani hiyo ni  sekta ambayo huzalisha wataalamu wote duniani.

Nao wamiliki wa skuli hiyo, Sadiki Mohammed Ali na Hatice Colak,  wamesema lengo la kuanzisha Skuli katika kijiji cha Kizimkazi na vijiji jirani ni kuhakikisha wanatoa elimu ya awali na msingi na wanasaidia  wanawake, watoto,wazee pamoja na watu wenye mahitaji maalum.

Wamesema pia wana Taasisi isiyokuwa ya Kiserikali   ambayo inajishughulisha na maswali mbalimbali ya kijamii ikiwemo  uchimbaji wa visima  katika vijiji mbalimbali na kuwasaidia watu walio na hali ngumu kimaisha.

Skuli ya Assalam Community Foundation, imeanzishwa mwaka 2017, ili kutoa taaluma kwa wananchi wa Zanzibar hasa vijijini.