NA HAFSA GOLO

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ, Masoud Ali Mohammed amesema utekelezaji wa agizo la serikali la kutolewa vitambulisho vya ukaazi kwa wananchi lazima lizingatie sheria na taratibu zilizopo.


Alieleza hayo jana katika kikao cha majumuisho ya ziara ya Baraza la Wawakilishi ya Kamati ya kusimamia ofisi za Viongozi Wakuu   kilichofanyika katika ukumbi wa Kikosi cha Valantia (KVZ) Mtoni, wilaya ya Magharibi ‘A’. Unguja.


Alisema agizo hilo halipingi wala kubeza sheria zilizopo, hivyo amesisitiza lazima watendaji wasimamie sheria badala ya kufuata mitazamo mengine.


“Agizo la serikali lisiwe chaka la utoaji wa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi kiholela na hatimae kusababisha kuibua changamoto sizizo na tija katika masuala ya kubeza sheria zilizopo nchini,” alisema.


Hivyo Masoud alizitaka taasisi zinazohusika  na usimamizi wa suala hilo pamoja na ofisi za Wakuu wa Wilaya na Mikoa kuhakikisha watu wanaopatiwa vitambulisho ni watu  wanaostahiki na wenye sifa kwa mujibu wa sheria.

Mbali na hilo katika majumuisho hayo Waziri huyo, alipongeza juhudi zinazochukuliwa na kamati hiyo katika kuibua mambo ya muhimu ambayo yatasaidia kuleta ufanisi wa kiutendaji sambamba na mabadiliko ya maendeleo katika taasisi za serikali.

Aliahidi kufanyia kazi ushauri aliopewa na kamati hiyo hasa ikizingatiwa umedhamiria kusimamia kasi ya maendeleo ya serikali ya awamu ya nane katika kuleta huduma bora za wananchi.

Waziri huyo alisema hatua hiyo itasaidia kuleta ufanisi wa kiutendaji na chachu katika kuleta mabadiliko chanya ya maendeleo na kuimarika kwa uchumi.

Katika hatua nyengine waziri huyo, alisema amekusudia kukaa pamoja na watendaji wake ili kuona njia sahihi ya uwekezaji wa mazingira bora katika soko jipya linalojengwa Kibandamaiti.


Alisema kikao hicho kitatoa uamuzi wa kusitisha ufunguzi wa soko hilo ambao unatarajiwa kufanyia mapema mwezi wa Febuari hadi mapaka ufanyike ujenzi wa miundombinu ya maji ya mvua sambamba na vifaa vya kuwekea bidhaa kwa wafanyabiashara watakaotumia soko hilo ikiwa ni miongoni mwa maombi ya kamati hiyo.

Mapema Kaimu Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa Mjini, Suleiman Mohamed Rashid, alisema ujenzi wa soko utakapokamilika zaidi ya wafanyabiashra wadogo 1,200 wanaofanya biashara zao eneo la Kijangwani na wengine wanaofanya maeneo yasio rasmi wanatarajiwa kufanya shughuli zao katika soko.

Alisema  ujenzi wa soko hilo awali ulikuwa ni wa mabanda 14 lakini kutoka a na ukubwa wa eneo na mahitaji ya wafanyabiashra, mabanda mengine 14 yameongezwa na kuwa na idadi ya mabanda 28 ambayo anaamini yatapunguza changamoto ya ufinyu wa maeneo ya biashara.


Rashid aliongeza kuwa changamoto iliyopo katika soko ni ukosefu wa fedha za kujengea uzio sambamba na miundombonu ya kudhibiti mazingira wakati wa mvua ikiwemo vigae.


Nae Mkuu wa Wilaya ya Magharibii ‘B’, Hamida Mussa Khamis alisema kukamilika kwa soko hilo litamaliza tatizo la kuzagaa kwa wafanyabiashara wadogo katika maeneo mengine ikiwemo Michenzani.


Mwenyekiti wa Kamati hiyo Hassan Khamis  Hafidh, alimtaka Waziri kuhakikisha zinatumika mbinu mbadala zitakazosaidia soko hilo la muda kuwa ni la kisasa na kutoa huduma bila ya kikwazo chochote ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya uingiaji wa maji ya mvua na uzio.

Alisema iwapo soko hilo litafunguliwa bila ya kufanyia mambo hayo litaondoa haiba na mandhari nzuri na kutofikia malengo ya serikali.