NYANZA, RWANDA
MAHAKAMA mjini Nyanza kusini mwa Rwanda imeendelea kusikiliza kesi ya Jean Claude Iyamuremye anayejulikana kwa jina maarufu kama ‘Nzinga’, anayekabiliwa na mauaji ya kimbari.
Hata hivyo mtuhumiwa huyo amekataa kuhusika katika mauaji ya kimbari wala katika mashambulio yaliyofanywa na wanamgambo katika maeneo mbali mbali mjini Kigali na kuomba kuachiliwa huru mara moja.
Mwakili wake hapo jana walipinga hoja za mwendesha mashtaka aliyesema kuwa mshatakiwa alihusika katika mauaji dhidi ya watutsi yaliyofanyika katika maeneo mbali mbali mjini Kigali.

Waliiambia mahakama kuwa kama yeye alikuwa na umri wa miaka 18 tu wakati wa mauaji ya kimbari na pia alikuwa mwanafunzi na hakuwa na uwezo wa kukaa pamoja ama kujadili lolote na vigogo waliopanga na kutekeleza mauaji ya kimbari.
Kadhalika amesisitiza kwamba asingeweza kuwa na nia yoyote ya kuuwa watutsi kwa kile alichoeleza kwamba mama yake alikuwa mtutsi.
Upande wa mashtaka unadai kwamba kulikuwa na ushahidi wa kutosha kwamba Nzinga alikuwa akiendesha gari lililojaa wanamgambo na askari waliotekeleza mauaji katika kambi zilizowahifadhi watutsi.
Kuhusu hoja za mashahidi, Iyamuremye Jean Claude ameiambia mahakama kuwa taarifa za mashahidi zilikuwa zinatofautiana na pengine mashahidi walionekana kujichanganya katika ushahidi walioutoa.