Ni Mdau mkubwa  elimu

Mchango wake  ni wa kupigiwa  mfano

Aitaka  serikali kuwathamini walimu

NA LAYLAT KHALFAN

UNAPOKUTANA nae njiani akili haikutumi kuwa ni msomi aliyebobea na aliyepitia nyadhifa mbalimbali na kubwa serikalini.

Unaweza kusema yule ni mtu tu aliyepindwa na maisha katika miaka yake ya  ujana  na sasa anasubiri rehema na msaada kutoka  kwa wanawe.

Na ukimuona kwenye  baraza za  kahawa anapasha tumbo moto, utasema yule mzee labda ndo mpishi wa kahawa kutokana na ucheshi wake na ukarimu uliotukuka.

Nimesema hivyo kutokana na mazingira yake niliyomkuta kijijini kwao Ndaambani, shehia  ya  Dimani, wilaya  ya Magharibi, Unguja.

 Waasifu wake  ana  umbo la  wastani, mrefu kiasi na tayari ameshakuwa mtu mzima anaejiweza,  aliyeng,oa baadhi ya  meno yake  mbele na kwa haraka haraka utasema ni mzee aliyekuwa hajasoma.

Kumbe  umdhaniae siye kumbe  ndiye, ni gwiji wa sayansi hapa  Zanzibar na  mchango wake ni mkubwa sana katika  fani hiyo.

Uvaaji wake wa kanzu, seruni na kofia utasema ni mtu aliyekuwa anacheza ngoma ya kibati, kumbe huvaa tu wakati anapokuwa  katika  mazingira  ya  kwao.

Nimekutana  nae  kwa  mara  ya  kwanza , lakini nimemjua  kuwa ni  mtu anaependa mas-hara kwa watu na anazungumza na kila rika bila ya kujali usomi na elimu aliyokuwa nayo.

Huyo ni  Maalim Ameir Suleiman Haji (Njeketu), ambaye ni mwalimu maarufu sana na aliyefanikiwa kuwasomesha wananfunzi wengi wa  Sayansi hapa  Zanzibar  hasa  masomo ya  Kemia  na Fizikia (Chemistry na  Physics).

Uwezo wake  mkubwa  wa masomo hayo amesaidia  wanafunzi wengi wa  Zanzibar na kupasisha katika ngazi mbali mbali za elimu.

Akizungumza  na makala  haya Maalim Njeketu anasema  kuwa  safari yake  kuwa  mwalimu wa Sayansi ni ndefu na  hakutarajia  kuwa hivyo, lakini alilenga  zaidi kuwa  Mhandisi.

Anasema baada  ya  kumaliza  masomo yake  ya Kidatu cha Sita mwaka 1974, alijiunga  na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa  masomo ya  Sayansi kwa  kuwa  tayari alikuwa  amejikita zaidi katika  masomo ya  Kemia  na Fizikia.

Aidha  anasema  kuwa  moyoni mwake alikuwa  awe Mhandisi, lakini alishajiishwa awe hivyo kuwaq  bingwa  wa  masomo hayo.

Anaeleza kuwa alipomaliza masomo yake Chuo Kikuu cha Dar  es Salaam, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar haikusita haraka  ilimuajiri na kumpeleka Chuo cha Ualimu Nkrumah wakati huo  mwaka 1978 na kusomesha waliokwenda kwa  kozi za Ualimu na  pia Kidatu cha Nne  kwa  wakati huo.

Hata  hivyo, anasema mnamo mwaka 1986 alipata uhamisho na kwenda Skuli ya  Sekondari ya  Benbella kama Mwalimu Mkuu kwa muda wa mwaka mmoja tu, na kupata uhamisho kwenda Sekondari ya  Lumumba  kuendelea  kusomesha somo la Fizikia  na Kemia.

Anasema kwa kuwa alikuwa  mbobezi wa  masomo hayo, alisomesha vizuri na kuipatia sifa skuli ya Lumumba kwa  kufanya  vyema  kitaifa  mara  kadhaa na hadi leo skuli hiyo bado inaendelea kupasisha vizuri siku hadi siku.

“Inawezekana baada ya kufanya vizuri skulini hapo nilibahatika kuchaguliwa kuwa  Mwalimu Mkuu wa skuli hiyo”, alisema Maalim Njeketu akionesha kujivunia heshima  hiyo aliyoipata  kwa  mafanikio.

Anasema  kwa  vile  kazi ya  ualimu ni ya  kuhama hama  haikuchuka  muda  mrefu alihamishiwa tena  Chuo cha Ualimu Nkrumah   na  alidumu kwa muda  wa miaka  mine.

Aidha  anasema  akiwa  katika chuo hicho  ndipo alipojizolea umaarufu zaidi , kwani  alipangiwa kazi na kuwa  Mkuu wa Divisheni ya Sayansi na Teknolojia.

Anasimulia  kuwa kadri siku zilivyokwenda  alikuwa ni mwalimu wa kupigiwa  mfano kioo  kutokana na jitihada zake za ufundishaji na kwa  bahati  Rais  aliyekuwepo madarakani wakati huo  alimpandisha daraja na kuwa Mkurugenzi wa Elimu Zanzibar.

Anaeleza kuwa mnamo 2006 akateuliwa kushika  wadhifa  wa  Mkurugenzi wa Elimu ya Juu Sayansi na Teknolojia katika  Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar.

Kabla ya kustaafu nafasi yake ya mwisho alikuwa Mkurugenzi wa Baraza la Mitihani ya Zanzibar.

Baada ya kufanyakazi zake vizuri katika miaka yote hiyo,Maalim Njeketu anasema  kuwa  hakutarajia kupata  heshima  kubwa  ya  nchi , lakini kumbe  jitihada  zake  zilikuwa zinaonekana.

Anasema  Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi wa Awamu ya Saba, Dk. Ali Mohamed Shein alimtunuku nishati ya utumishi ulitukuka katika  sherehe  maalum wakati wa  sherehe  za  Mapinduzi.

“ Sikutarajia shangwe, nderemo na  vigeregere vilisikika baada ya wakati wa  kukabidhiwa nishani hiyo kuonesha  kuwa kweli jitihhada  zangu zilithaminiwa”, alifahamisha Maalim Njeketu  huku akionesha  kweli alithaminiwa  mchango wake.

Mwalimu Njeketu ameiambia  makala  haya  kuwa  licha ya jitihada na uzoefu mkubwa aliokuwa nao katika fani ya Ualimu, lakini alivunja ukimya na kusema hazikuwa ndoto zake za kusomesha katika maisha yake, lakini serikali ndio iliyomtaka  kujikita na fani hiyo na aliitikia.

“Zamani kazi zilikuwa zinatafuta watu na sio leo watu wanatafuta kazi. Kwa hiyo baada ya kumaliza chuo tu nilipendekezwa niwe mwalimu na sikuweza kupinga na nilifanya hivyo”, aliongeza.

Anasema ndoto zake alikuwa anataka awe injinia na ndio maana alijikita zaidi katika masomo ya sayansi.

“Nilipangiwa kazi hii ya kusomesha na sikua na kipaji nacho na nililazimika kusomesha kwa kuwa serikali iliamua mimi kufanya hivyo”, anasema.

Maalim Njeketu  anasema katika fani yake hiyo ya ufundishaji alibahatika kutembelea nchi mbali mbali kama vile China, Marekani, Ufaransa, Afrika Kusini, Zimbambwe, Uganda, Israel, Pakistan na  kadhalika  kwa lengo la kupata uzoefu wa kusoma na kusomesha pia.

Anasema katika nchi hizo alizotembelea alibahatika kuwasomesha wanafunzi wengi, ambao wengi wapo kwenye serikali katika nafasi kubwa.

Anasema  kwa  hapa  Zanzibar amesomesha wengi ambao wameshika   nyadhifa  mabali mbali zikiwemo za  Ukurugenzi, Ukatibu Mkuu makamanda  wa jeshi, walimu na hata  madaktari wakubwa.

Akiwataja baadhi ya wanafunzi wake aliopasisha kuwa  wakubwa  ni Maryam Abdallah Sadala (Mabodi), ambae ameshika nafasi ya Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Dk.Ota ambae ni daktari bingwa wa watoto.

Wengine ni Hassan Aboud Talib alikuwa TRA, Asya Iddi ambae kwa sasa ni Mkurugenzi wa Elimu Sekondari na wengine ambao hakuweza kuwamaliza kuwataja.

Aidha Maalim Njeketu  hakusita na kuiomba serikali kuendelea  kuwathamani wastaafu hususan walimu kwa kuwatizama kwa jicho la huruma na kuwaweka katika nafasi yao.

“ Walimu katika nchi ndio kila  kitu. Ndio msingi wa fani zote zinazohitajika”, alisisitiza.

Vile vile aliiomba serikali kujitahidi kushughulikia zaidi suala la elimu kwa kuwapatia nyezo walimu na wanafunzi kwa kuwaimarishia maabara za sayansi na lugha, upatikanaji wa vitabu na vitendea kazi vya walimu.

Kwa upande mwengine alisisitiza kwamba masomo ya Sayansi na somo la Hisabati kusomeshwa walimu wengi ili maendeleo ya elimu yaweze kufikiwa.

Maalim Njeketu alizaliwa  mwaka 1953 katika  kijiji cha Dimani, wilaya  ya Magharibi Unguja.

Mnamo mwaka 1961 alijiunga na Skuli ya Msingi Kombeni kuanzia darasa la kwanza hadi Kidato cha Pili.

Mwaka 1971 alibahatika kuingia Skuli ya Sekondari  Lumumba kuanzia Kidato cha Tatu hadi cha Sita na kumaliza masomo yake hapo 1974.

Maalim  Njeketu ana watoto watano wakiume wanaume  watatu na wawili wanawake, huku mwanae mmoja wa kiume akiwa amefuata nyayo zake za Ualimu na anasomesha katika skuli ya Lumumba masomo ya Sayansi.

“Nimestaafu kazi mwaka 2016 hadi leo ndio nipo hapa naishia kwenye vijiwe vya kahawa na kupoteza muda huku serikali ikiwa ndio mama anaeniendeleza kunilea”,anasema.

“Nashkuru wanangu wote wamenifuata mimi nathubutu  kusema wamenipita kielimu, kwani wao wamefikia hadi PhD”, anamalizia Maalim Njeketu, ambaye  ni hazina  kubwa  ya Taaluma  ya  Ualimu.