NA MWANDISHI WETU

ALIYEKUWA Rais wa kwanza wa Zanzibar, Hayati  Sheikh  Abeid Amani Karume, bado ataendelea kuwa ni  kielelezo cha ushujaa kwa Wazanzibari kutokana na  matendo yake yaliobaki kuwa tafsiri halisi ya uzalendo na maendeleo. 

Kiongozi huyo licha ya kuwa shujaa na mwana Afrika halisi, alipigania maslahi ya  wananchi wanyonge na masikini, bila kuchoka hadi pale uhuru kamili wa Zanzibar ulipopatikana Januari 12, mwaka 1964.

Hayo yameelezwa jana na Waziri  wa zamani wa Mambo  ya Ndani ya Nchi, Mzee Ali Ameir  Mohamed, akiwa kijijini kwake huko Donge Kichavyani kisiwani Unguja katika mahojiano maalum ya kumbukumbu ya miaka 49 tokea kuawa kwa Rais huyo  wa kwanza April  7, mwaa 1972.

Mzee Ameir,  alisema viongozi wengi  katika bara la Afrika wamekuwa na tabia ya kutoa misimamo mingi inayohusu utetezi wa maslahi ya watu wote wanapokuwa nje ya madaraka, na pale wanapokalia viti vya utawala hujisahau na  kutenda kinyume na ahadi zao.

Alisema ahadi za chama cha ASP  kupitia Manifesto yake ya kwanza ya uchaguzi toka  mwaka 1957, na ahadi za Rais Mzee Karume ilisimamiwa ipasavyo katika utekelezaji ulioleta manufaa chanya yenye tija  kwa wananchi na maendeleo ya nchi yao.
“Nathubutu kusema kinagaubaga Hayati  sheikh Abeid Amani Karume ameuawa akiwa kielelezo cha ushujaa kutokana matendo yake mema .Utekelezaji wa ahadi  zake kwani dhana ya uzalendo na maendeleo amezitekeleza na aliyaahidi ametenda na alioyaacha yamebaki kuwa alama ya maendeleo” Alisema Mzee Ameir.

Waziri  huyo wa zamani akimzumgumzia hayati  Mzee Karume ,amelitaja  jina lake halitachakaa na kusahaulika kwa kuwa alijitolea maisha yake  yote kuhakikisha Zanzibar inafika mbali kimaendeleo katika kujenga  ustawi wa maisha ya watu chini ya umoja, amani alipinga ubaguzi ,ukabila na udini. 

Aidha, Mzee Ameir amesema, kabla ya kuingia madarakani chama chake ASP kuliweka msimamo wake bayana na kusema  kikifanikiwa kushika  madaraka kitavunja matabaka ya ubwana na utwana ,kukomesha ubaguzi na kuhimiza watu kushirikiana na kufanyakazi za kimaendeleo. 

“Mzee wetu Karume aliamini katika msimamo uliowataka wananchi kufanyakazi kwa bidii,huthaminiwa kwa utu na heshima ya kila mmoja .Hakutaka uzembe,  uvivu na porojo .Hakusita wala kuogopa kusema kweli hivyo amekufa akiwa shujaa wa kweli na mzalendo kwa Zanzibar na Afrika “Alisksitiza 

Mwanasias huyo,  aliyewahi pia kuwa Waziri  wa Nchi  Ofisi ya Waziri Mkuu Sera na Habari, alisisitiza na kutaka kizazi kipya kuisoma historia ya nchi yao mahali ilipotoka, ilifikaje mahali walipo na kuona jinsi watakavyoilinda nchi yao bila kupotoshwa.