NA TATU MAKAME
OTHMAN Koroka Mayabo (28) mkaazi wa Kombeni Wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja, amepandishwa katika kizimba cha mahakama ya mkoa Vuga, akikabiliwa na kosa la kumtorosha msichana aliye chini ya uangalizi wa wazazi wake.
Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka, kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Shamsi Yasin, mbele ya Hakimu Salum Bakari kuwa, mshitakiwa huyo alitenda kosa hilo Novemba 23 mwaka 2020 majira ya saa 4:00 huko Kombeni.
Alisema mshitakiwa huyo, alitenda kosa la kumtorosha msichana huyo jambo ambalo ni kosa kisheria.
Alisema kosa la pili kumuingilia msichana huyo, kinyume na kifungu cha 133 (a) cha sheria namba 6 cha mwaka 2018 sheria za Zanzibar.
Alisema, baada ya kusomewa kosa hilo mshitakiwa aliomba dhamana ombi ambalo lilikataliwa mahakamani hapo.
Hata hivyo amepelekwa rumande na kutarajiwa kufikishwa tena mahakamani hapo April 29 mwaka huu kesi yake itakapotajwa tena.