Mikakati yahitajika katika kukubialiana nazo
NA MWANAJUMA ABDI, DAR ES SALAAM
KILA ifikapo Juni 26 ya kila la mwaka, dunia huadhimisha siku ya kimataifa ya kupambana na dawa za kulevya, ikiwa na lengo la kuongeza uelewa wa jamii na kuhamasisha umma kushiriki katika mapambano dhidi ya matumizi na biashara ya dawa hizo.
Kauli mbiu ya mwaka huu “Tuelimishane juu ya Tatizo la Dawa za Kulevya, Kuokoa Maisha”, ambayo inawafahamisha jamii kujua ukweli juu ya madhara yanayotokana na matumikzi ya dawa za kulevya ili isijingize katika matumizi ya dawa hizo.
Hivi karibuni, Kamishna Jeneral wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Gerald Musabila Kusaya, wakati akizungumza na wandishi wa habari juu ya maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kupambana na dawa hizo yatafanyika katika viwanja vya Nyerere Square Dodoma na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa Majaliwa.
Alisema maadhimisho hayo hufanyika kila ifikapo Juni 26 ya kila mwaka, huadhimishwa duniani kote, kwa lengo la kutoa elimu kwa umma juu ya athari na madhara ya matumizi na kufanya biashara hiyo katika jamii.
Alieleza dawa za kulevya ni kemikali ambazo ziingiapo mwilini huathiri ubongo wa mtumiaji na kumsababisha kuwa na matendo, hisia, fikra na muonekano tofauti na matarajio ya jamii.
Kemikali hizo hutokana na mimea na madini ambayo ni malighafi, muhimu kwa mahitaji mengine ya mwanadamu, ambapo dawa hizo huingia mwilini kwa njia kuu tatu, ikiwemo ya kunywa au kula, kuvuta na kujidunga shindano.
Dawa za kulevya zipo za aina mbali mbali lakini maarufu ni pamoja na Heroin, cocaine, Methamphetamine, bangi, mirungi na nyenginezo.
Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za kulevya imechambua dawa za kulevya aina ya mirungi na bangi, inayotokana na mmea.
Kwa kuanzia ya Mirungi unatokana na mmea unaoitwa “Catha edulis”, ambao una kemikali za cathinone na cathine ambazo huongeza kasi ya utendaji wa mfumo wa fahamu.
Mirungi ilikuwa inatumika tangu enzi za mababu kwenye nchi za pembe ya Afrika hususani Ethiopia, Eritrea, Kenya, Somalia pamoja na rasi ya Arabuni nchini Yemen.
Dawa hiyo hutumiwa zaidi kwenye mikusanyiko ya wanaume ingawa katika miaka ya karibuni wanawake wamejiingiza katika matumizi ya dawa hiyo.
Kwa upande wa Tanzania mirundi hustawi na hupatikana kwa wingi katika mikoa ya Kilimanjaro- Same, Tanga- Lushoto, Manyara na Arusha – Mlima Meru.
Kiasi kikubwa cha mirungi huingizwa nchini isivyo halali kutoka nchi jirani ya Kenya ambako ni zao halali la biashara, ambapo pia hujulikana kwa majina mengine kama gomba, veve, miraa, mogoka, kangeta, giza, bomba, kashamba, mbaga, alenle.