Jamii haipaswi kuwa na dhana, mitazamo finyu juu ya chanjo
NA BAKAR MUSSA, PEMBA. (Kwa msaada wa Mtandao)
KINGA ni bora kuliko tiba, hivyo ndivyo wahenga na wataalamu wa Afya wanavyosisitiza.
Bilas haka hili halina wasiwasi kwa sababu watu wote ni mashahaidi kwa njia moja au nyengine juu ya faida zinazopatikana kwenye kujikinga na hasara zinazoambatana na kutibu.
Linapokuja suala la chanjo usemi huu imekuwa rahisi kusahaulika hasa hapa katika visiwa vya Unguja na Pemba, na mara nyengine nchi nyengine za Bara la Afrika.
Imekuwa ni jambo la kawaida unapokuja wakati wa kutoa chanjo hasa ile inayowahusu watu wengi kwa pamoja hutokeza watu ambao huamua kupinga chanjo husika pengine kwa hoja dhaifu huku wenyewe wakiwa hawana ujuzi wowote kuhusu chanjo.
Wala inavyotengenezwa, wala inavyofanyakazi pamoja na taratibu zinazopitia hadi kukubalika kwake kuwa zitumike kwa maisha ya binaadamu.
Kwa wale wanaofuatilia mambo ya hapa kwetu ni mashahidi wa hili, kuna wale wanaopinga kuanzia chanjo wanazopatiwa watoto kukingwa na maradhi mbali mbali kama vili surua, polio, kifua kikuu, pepopunda na mengineyo na wanaopinga chanjo zinazokuja baada ya watoto kukua.
Tumeyashuhudia haya wakati wa chanjo za kukinga wasichana na saratani za kizazi, tulishuhudia wakati wa Utoaji wa matone ya Vitamin A, tumeshuhudia wakati wa Utoaji wa chanjo ya Kipindu pindu nakadhalika.
Maneno haya ya kupinga chanjo yamejitokeza pia katika wakati huu ambao dunia inahangaika kuwakinga wanaadamu na janga la Ugonjwa wa Corona.
Ugonjwa ambao hadi mwanzo mwa mwezi huu wa Julai tayari umeshachukua maisha ya watu takriban milioni nne (4,000,000).
Wapingaji hawa hutumia maneno na vishawishi mbali mbali na vitisho ili kuwavunja moyo wale ambao wanadhani wanaweza kutumia chanjo husika.
Maneno kama vile chanjo imelenga kupunguza idadi ya watu, inakusudia kupunguza uwezo wa watu kuzaliana, inapunguza nguvu za kiume/za kike ni maarufu kila inapotokezea msimu wa chanjo.
Maneno haya husemwa mara nyingi, na kurudiwa na kuenezwa kiasi kwamba huwafanya baadhi ya watu ama kuamini moja kwa moja au kubakia njia panda iwapo watumie au wasitumie chanjo flani.
Jambo hili hupunguza ufanisi kwa sababu kinga kamili katika jamii hupatikana pale ambapo walengwa wote wamepata chanjo husika.
Nadhani ni Mashahidi jinsi Dunia ilivyohangaika kutokomeza kabisa ugonjwa wa polio kwa sababu kila jitihada za kuhakikisha kwamba watoto wote duniani wamechanjwa basi hutokezea nchi ambazo kuna watoto ambao hawakuchanjwa kwa sababu mbali mbali zikiwemo za migogoro na vita ama zile za kupinga kama zinavyojitokeza miongoni mwa wenzetu.
Katika wakati huu ambapo dunia inapambana na ugonjwa wa Corona au Virusi vya COVID-19 chanjo imekuwa tena nia suala muhimu.
Ni takriban mwaka wa pili sasa tokea ugonjwa huu ulipoanza kugundulika lakini hakuna matibabu yake, Wataalamu wamehangaika kutafuta njia ya kunusuru maisha na sasa angalau kuna Chanjo.
Mataifa mbali mbali yanajaribu kutengeneza chanjo zao lakini kwa sasa angalau chanjo tatu zinatumika zaidi hizi pamoja Oxford Astrazaneca, Pfizer na Johson and Johson najua pia kuna nchi kama Cuba ina chanjo yake ya Abdalla na Russia pia.
Tafauti na magonjwa mengine ambayo huathiri nchi zinazoendelea kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko nchi zilizoendelea ugonjwa wa Corona umeleta athari sawa bila kuchaguwa iwapo ni taifa linaloendelea au lililoendelea.
Na mara nyengine tumeshuhudia mataifa yanayoendelea yakiwa na unafuu kidogo kuliko yaliyoendelea, kwa mfano Mataifa kama vile Ujerumani, Italy, Uingereza na Marekani yaliathiriwa zaidi na tatizo hili hata kuliko baadhi ya Mataifa masikini ya Afrika na Asia.
Jambo hili lilileta tofauti pia katika upatikanaji na mgawanyo wa Chanjo, ilipelekea dunia kushuhudia kiwango kikubwa cha chanjo (zaidi ya asilimia 90) kikibakia katika mataifa yaliyoendelea na asilimia ndogo ikielekezwa katika nchi zinazoendelea zikiwemo nchi zetu za bara la Afrika.
Wakati hali ikiendelea kuleta matumaini katika mataifa yaliyoendelea kuna kila dalili kwamba nasi tulioko katika nchi zinazoendelea ambazo kimsingi bado zinakabiliwa na kitisho cha wimbi la tatu la Corona huenda nasi tukapata mgao wa chanjo hizo.
Shukrani nyingi ziende kwa Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) ambalo limekuwa likipiga kelele bila kuchoka umuhimu wa kuhakikisha pia kwamba chanjo zinagawanywa kwa usawa bila kujali taifa, eneo au hali ya kiuchumi.
Jambo hili linaashiria kwamba japo kwa kuchelewa kidogo lakini nasisi huenda tukapaata chanjo hapa kwetu.
Serikali zetu zote mbili zimekuwa wazi juu ya hili, kwamba chanjo ya Corona itakuwa ni hiari lakini itahakikishwa kwamba inapatikana na wale wataopenda kutumia watumie.
Shirika la Afya ulimwenguni, limekuwa likikaririwa na msimamo huo kwamba chanjo ya Corona ni hiari lakini linashauri watu wachanje kutokana na kuwa na faida kubwa zaidi kwa kukinga gonjwa hili.
Kwa mfano takwimu za hivi karibu zinaonesha kuwa wakati wa kabla ya chanjo mtu 1 kati ya 10 waliopata ugonjwa wa Corona alilazwa hospitali lakini kwa wale waliopata chanjo ni mtu 1 tu kati ya 50 ndio ataishia kulazwa hospitali kwa hiyo ni faida kubwa.
Kwa hivyo wakati tukiamini kwamba ndani ya muda mfupi ujao kutakuwa na uwezekano wa kupata chanjo ya Corona ndani ya Tanzania na ndani ya Zanzibar nimeonelea ni muhimu kuelezana kidogo kuhusu suala la chanjo hasa chanjo ya Corona.
UMUHIMU WA CHANJO YA CORONA
Kuelezana huko hakuna lengo la kuwataka watu waende kuchanja au kuwazuia wasiende kuchanja bali kuna madhumuni ya kusaidiana kupanua ufahamu juu ya Chanjo.
Ili yule ambae ataenda kuchanja na hata ambae ataamua kutokwenda kuchanja awe na uelewa juu ya maamuzi yake na pengine athari nzuri au mbaya za maamuzi yake.
Angalizo ni kwamba mwandishi wa Makala hii si mwanasayansi wa chanjo, wala si daktari wa chanjo ispokuwa amesaidia kukusanya taarifa hizi kutoka vyanzo vya kuaminika sana Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) ili zisaidie ufahamu wa wanajamii wenziwe.
NINI CHANJO.
Chanjo zinajumuisha vipande vidogovidogo vya vijiumbe vinavyosababisha magonjwa au chembe chembe zinazounda vipande hivyo vidogo vidogo.
Pia zina viungo vya kusaidia chanjo kuwa na ufanisi na kuwa salama, hivi vinajumuishwa katika chanjo nyingi na vimekuwa kuwa vikitumika kwa miongo kadhaa katika mabilioni ya dozi za chanjo.
Kila kiungo cha chanjo hutumika kwa kusudi maalum na kila kiungo hujaribiwa katika mchakato wa utengenezaji na viungo vyote hufanyiwa majaribio kwa sababu za usalama.
KWA NINI IWEPO CHANJO?.
Ili kukomesha magonjwa haya, kunahitaji kutumia njia zote za kuzuia, chanjo ni moja wapo ya njia bora zaidi ya kulinda afya na kuzuia magonjwa, hufanya kazi na kinga asili ya mwili ili uwe tayari kupambana na virusi.
Hatua zingine, kama kuvaa kinyago kinachofunika pua na mdomo na kukaa mbali miguu 6 kutoka kwa watu wengine ambao hauishi nao, pia husaidia kuzuia kuenea kwa COVID-19, uchunguzi unaonyesha kuwa chanjo ya COVID-19 inafaa sana kukuzuia kukuambukiza ugonjwa huo.
Wataalam wanafikiria kupata chanjo ya COVID-19 inaweza kusaidia kuzuia kutabaanika hata ikiwa umepata COVID-19, chanjo hizi haziwezi kukupa ugonjwa
USALAMA WAKE UKOJE ?
Mfumo wa usalama wa chanjo Marekani inahakikisha kuwa chanjo zote ziko salama iwezekanavyo, kwani hizo Chanjo zote zinatumiwa zimepitia vipimo sawa vya usalama na kufikia viwango sawa na chanjo zingine zozote zilizotumiwa kwa muda mrefu.
Zina mifumo iliowekwa kote Duniani ambayo inaruhusu CDC kuangalia maswali ya usalama na kuhakikisha kuwa chanjo zinakaa salama.
CHANJO GANI ZINAPATIKANA?.
Ziko aina tofauti za chanjo za COVID-19 zitapatikana, ambazo hutolewa kwa sindano ya aina mbili, moja kwa wakati na nyengine wakati mwengine.

Sindano ya kwanza inauandaa mwili, ya pili inatolewa nyuma ya wiki tatu baadaye ili kuhakikisha mwili una ulinzi kamili.
Ikiwa mtu ameambiwa anahitaji sindano mbili, ahakikishe unapata zote mbili, zinaweza kufanya kazi kwa njia tofauti, lakini aina zote za chanjo zinasaidia kujikinga.
NDANI YA CHANJO MUNAVITU GANI
NA VINAMSAADA NINI.
ANTIGENI
Kila chanjo ina kitu kinachoitwa Antigeni ambacho husaidia kinga ya mwili kufanyakazi dhidi ya magonjwa na antigeni inaweza kuwa ni sehemu ndogo ya vijiumbe vinavyosababisha magonjwa (Bakteria, Virusi, pollen) kama vile protini au sukari, au inaweza kuwa ni kijiumbe kizima katika muundo ambao umedhoofika au haufanyikazi.
VIHIFADHI
Vihifadhi huzuia chanjo kutoharibika au kuchafuliwa mara baada ya kufunguliwa kizibo au kifuniko kama itatumika kuchanja mtu zaidi ya mmoja.
Chanjo zingine hazina vihifadhi kwa sababu zinawekwa kwenye kasha ya dozi au kipimo kimoja kwa ajili ya mtu mmoja na kasha hutupwa baada kipimo hicho kimoja cha chanjo kutumika.
Kihifadhi kinachotumika sana ni 2-phenoxyethanol na imekuwa ikitumika kwa miaka mingi katika chanjo kadhaa, imekuwa ikitumika katika bidhaa mbalimbali za Watoto nani salama kutumika katika chanjo kwani sumu yake kwa binadamu ni ndogo sana.
VIDHIBITI
Vidhibiti huzuia athari za kemikali kutokea ndani ya chanjo na vinafanya sehemu ya chanjo hiyo kutoshikamana na makasha ya chanjo hiyo na vifuniko.
Vidhibiti vinaweza kuwa ni sukari (lactose, sucrose), tindikali ya amino(glycine) na protini ya kwenye mwili wa binadamu inayotokana na hamira au chachu.
SURFACTANTS
Surfactants au chembe mtungo inaweka viungo vyote kwenye chanjo pamoja, zinasaidia na kutulia na kutogongana kwa vitu ambavyo viko katika mfumo wa maji ya chanjo pia mara nyingi hutumika katika vyakula kama barafu (ice cream).
MABAKI
Mabaki ni kiasi kidogo cha vitu anuai ambavyo vinatumika wakati wa utengenezaji au uzalishaji wa chanjo ambazo sio viungo hai katika chanjo iliyokamilishwa.
Vitu vinatofautiana kulingana na mchakato wa utengenezaji uliotumiwa na vinaweza kujumuisha protini za mayai, hamira au viuatilifu.
Athari za mabaki ya vitu hivi ambavyo vinaweza kuwapo kwenye chanjo ni ndogo sana.
KIMIMINIKA
Kimiminika ni maji yanayotumika kulainisha chanjo kuwa katika hali sahihi inayohitajika mara moja kabla ya matumizi, na kinachotumiwa zaidi ni maji safi.
VISAIDIZI
Baadhi ya chanjo zinakuwa na visaidizi, vinaimarisha kinga ya kuhimili chanjo, wakati mwingine kuweza kuifanya sindano ya chanjo ikae inapochomwa kwa muda mrefu au kwa kuamsha chembe chembe za kinga.
Visaidizi hivyo vinaweza kuwa ni kiwango kidogo cha chumvi kama vile (like aluminium phosphate, aluminium hydroxide au potassium aluminium sulphate).
Aluminium imedhihirisha kutosababisha matatizo yoyote ya muda mrefu ya kiafya na binadamu wamekuwa wakijipa kiwango cha aluminium kwa kula na kunywa.
CHANJO ZINATENGENEZWAJE?
Chanjo nyingi zimekuwa zikitumika kwa miongo sasa na mamilioni ya watu wamekuwa wakipatiwa chanjo hizo salama kila mwaka.
Kama ilivyo kwa dawa zote kila chanjo lazima ipitie majaribio ya kina ili kuhakikisha ni salama kabla haijaanza kutolewa kwenye mipango ya nchi zao.
Kila chanjo ambayo inatengenezwa lazima kwanza ifanyiwe uchunguzi na tathimini ili kubaini ni antigen gani inapaswa kutumika ili kuamsha kinga.
Awamu hii ya awali hufanyika bila kujaribiwa kwa binadamu.
Chanjo ya majaribio hujaribiwa kwanza kwa wanyama ili kutathimini usalama wake na uwezo wake wa kuzuia magonjwa.
Ikiwa chanjo inaleta mwitikio wa kinga, basi hapo hujaribiwa kwa binadamu katika awamu tatu.
AWAMU YA 1
Chanjo hutolewa kwa idadi ndogo ya watu waliojitolea kutathimini usalama wake, kuthibitisha kuwa inatoa hakikisho la kinga na kuamua kipimo sahihi.
Kwa ujumla katika awamu hii chanjo zinajaribiwa kwa vijana, watu wazima wenye afya njema waliojitolea.
AWAMU YA 2
Katika awamu hii hutolewa kwa mamia kadhaa ya watu waliojitolea ili kutathimini zaidi usalama na uwezo wake wa kujenga kinga.
Washiriki katika awamu hii wanakuwa na sifa sawa (kama vile umri, jinsia) kama ilivyo kwa watu waliokusudiwa, na kwa kawaida kuna majaribio mengi katika awamu hii kutathimini makundi ya umri mbalimbali na michanganyiko tofauti ya chanjo.
Kundi ambalo halikupata chanjo kwa kawaida hujumuishwa katika awamu kama kikundi cha kulinganisha ili kubaini ikiwa mabadiliko katika kikundi kilichochanjwa yametokana na chanjo au yametokea kwa bahati.
AWAMU YA 3
Katika awamu hii hupewa maelfu ya watu waliojitolea huku wakilinganishwa na kundi kama hilo la wale ambao hawakupata chanjo lakini walipokea bidhaa za kulinganisha, kubaini ikiwa chanjo hiyo ni bora dhidi ya ugonjwa ambao imetengenezwa kulinda na kubaini usalama wake katika kundi kubwa la watu.
Majaribio mengine ya awamu ya tatu hufanywa katika nchi nyingi na sehemu nyingi ndani ya nchi ili kuwa na uhakika wa utendaji wa chanjo hiyo unaonekana kwa watu wengi tofauti.
Wakati wa majaribio ya awamu ya pili naya tatu waliojitolea na wanasayansi wanaoendesha utafiti huwa wanafichwa kujua ni kina nani waliopewa chanjo au waliopokea bidhaa za kulinganisha.
Hii inaitwa “kupofusha” na inapaswa kuhakikishwa kuwa waliojitolea au wanasanyansi wanaofanya utafiti hawaathiriwi katika tathimini yao ya usalama au ufanisi wa kujua ni nani aliye na bidhaa gani.
Baada ya majaribio kumalizika na matokeo yote kukamilika waliojitolea na wanasayansi walioendesha majaribio wanaarifiwa ni nani aliyepata chanjo hiyo nani aliyepewa bidhaa kulingana na matokeo hayo.
Wakati matokeo yote ya majaribio ya kliniki yanapopatikana hatua kadhaa zinahitajika zikiwemo tathimini ya uhakiki wa ufanisi na usalama kwa idhini ya sera za afya ya umma.
Maafisa katika kila nchi hutathimini kwa kina takwimu za majaribio na kuamua endapo waidhinishe chanjo hiyo kwa matumizi.
Chanjo lazima ithibitishwe kuwa salama na yenye ufanisi kwa idadi kubwa ya watu kabla ya kuidhinishwa na kuingizwa kwenye programu za kitaifa za chanjo.
VIPI ITAJUILIKANA UFANISI WA CHANJO?.
Kizuizi cha usalama na ufanisi wa chanjo ni kikubwa sana, kwa kutambua kwamba hupewa watu ambao wana afya njema na hasa ambao hawana maradhi au sio wagonjwa.
Ufuatiliaji zaidi unafanyika kwa njia ya kuendelea baada ya chanjo kutolewa, kuna mifumo ya kufuatilia usalama na ufanisi wa chanjo zote.
Hii inawawezesha wanasayansi kufuatilia athari za chanjo na usalama hata kama zinatumiwa kwa idadi kubwa ya watu kwa muda mfrefu.
Takwimu hizi hutumiwa kurekebisha sera za matumizi ya chanjo ili kuongeza athari nzuri za chanjo hizo na pia kuruhusu chanjo hiyo kufuatiliwa kwa usalama katika wakati wote wa matumizi yake.
Wakati chanjo inapoanza kutumika lazima ifuatiliwe kila wakati ili kuhakikisha inaendelea kuwa salama.
NI MAMBO GANI UNAYOWEZA KUFAHAMU
CHANJO YA COVID 19 NI SALAMA?.
Chanjo ya COVID-19 imethibitishwa kuwa salama na yenye ufanisi, nchini Marekani, hatua nyingi zimewekwa ili kuhakikisha kuwa chanjo zinapitia hatuwa mbali mbali zilizoelezwa .
Taarifa na takwimu kutoka kwenye majaribio zinakaguliwa kwa kutegemea na wanasayansi, wataalamu wa tiba, na wataalam wa afya ya umma kabla ya kupewa chanjo.
Vituo vya kudhibiti Magonjwa (CDC) vimeunda zana mpya ya kugundua haraka maswala yoyote ya usalama kuhusiana na chanjo za COVID-19, “V-safe” ni zana mpya inayotumika kwenye simu mahiri, ya kukagua afya baada ya chanjo.
Itatolewa kwa watu wakati watakapokuwa wanapokea chanjo ya COVID-19, chanjo ya COVID 19 itasaidia kujikinga kutokana na kupata COVID-19.
DOZI NGAPI ZINAHITAJIKA KUJIKINGA NA COVID 19.
Unahitaji dozi 2 za chanjo ya sasa ya COVID-19 ili kupata kinga kubwa zaidi dhidi ya ugonjwa huu mbaya.
Hivi sasa kuna usambazaji mdogo wa chanjo ya COVID-19 nchini Marekani, lakini usambazaji utaongezeka katika wiki na miezi ijayo.
Kila mtu ataweza kupata chanjo dhidi ya COVID-19 mara tu idadi kubwa ya kutosha ya chanjo itakapopatikana, ikishapatikana kwa wingi, kutakuwa na watoaji wa chanjo maelfu kadhaa.
Mnamo tarehe 13 Disemba 2020, ACIP ilitoa mapendekezo ya matumizi ya chanjo ya COVID-19 ya PfizerBiotech ili kuzuia COVID-19, mnamo tarehe 20 Disemba 2020, ACIP ilitoa mapendekezo ya matumizi ya chanjo ya COVID-19 ya Moderna ili kuzuia COVID-19.
Ukosefu wa fedha za kulipa, hali ya uhamiaji, au ukosefu wa bima havitazuia kupata chanjo dhidi ya COVID-19, dozi za chanjo zitatolewa kwa watu bila malipo bila kujali hali ya uhamiaji au ikiwa wana bima au la.
Watoaji wa chanjo wanaweza kutoza ada za usimamizi wa kutoa chanjo, watoaji wa chanjo wanaweza kulipwa ada hii na kampuni ya bima ya umma au ya binafsi ya anayepokea chanjo.
KUNA ATHARI GANI BAADA YA KUPATA CHANJO?
Baada ya chanjo ya COVID-19, unaweza kupatwa na athari za kawaida, hii ni ishara kwamba mwili umejenga kinga, athari ni dalili kwamba chanjo inafanya kazi, athari zinaweza kuwa kama homa na zinaweza hata kuathiri uwezo wa kufanya shughuli za kila siku, lakini zinaweza kuondoka baada ya siku ya chache.