• Hekima na busara ndivyo vinavyomsaidia  katika  kazi yake vyenginevyo asingedumu
  • Aliwahi kubambikiwa kesi ya kushirikiana na timu kwa  ushirikina
  • Ataka vyumba vya  wachezaji  Amaan vitengenezwe viwe  vya kisasa.

Na Mwajuma Juma

Juma Makungu Simai (58), anasimulia kazi yake ya  kufunga na kufungua  Uwanja wa  Amaan kila  siku kukiwa  na mechi  au hakuna ikiambatana  na visa  na mikasa.

Anasema   mwanzoni  hakuwa anajua kama kazi hiyo ya kufunga na kufungua milango ya Uwanja wa Amaan ni kazi ambayo inakuwa na utaratibu wake.

Anaeleza kuwa wakati anaaza kuingia katika uwanja huo alikuwa anamuona mtu tu akifanya shughuli yake hiyo na kuchukulia ni jambo la kawaida.

Anasema kwa takriban miaka 10 alikuwa  akifika  katika uwanja huo, lakini hakuweza kutambua lolote linalohusiana na kazi hiyo ilikuwa  ikifanywa  na  marehemu  Mfaume  Mwinyi, aliyefariki  mwaka 2013.

Akizungumza na  gazeti hili  Simai ambae  ni mzaliwai wa Dunga Bweni , Wilaya  ya  Kati Unguja,  anasema  mbali na kufanya majukumu mengine uwanjani hapo lakini kazi yake kubwa ni kutunza vyumba vya wachezaji.

Anasema kuwa kabla ya kuanza na jukumu hilo aliajiriwa ndani ya uwanja huo kama tarishi na baadae akahamishiwa katika bustani na sasa kazi yake ni kushughulikia bustani na kutunza vyumba hivyo vya wachezaji.

Simai anasema alinaza  kazi ya  kufunga  kufua  uwanja  wa Amaan mnamo mwaka 2015 baada ya  Mfaume  Mwinyi kufariki na  ikawa  hakuna  mtu mwengine.

“ Kazi hiyo ya kufunga na kufungua milango niliianza mwaka 2015 baada ya aliyekuwepo Mfaume Mwinyi kufariki dunia”, alifahamisha.

Alieleza kuwa anaipenda  kazi yake hiyo , kwani ndio maisha  yake ingawa  anakabiliana  na changamoto  ambazo anasema  ni sehemu ya  maisha .

“Changamoto nnazopitia kwangu nazichukulia ni za kawaida, wachezaji ni kama watoto wanaharibu vitu, ambapo kwangu naichukulia kuwa ni jambo la kawaida”, alisema.

Alieleza kuwa tokea kuanza kazi hiyo kitu ambacho hatokisahau katika maisha yake, ni baada ya kuambiwa kuwa alimruhusu mchezaji kuingia katika chumba cha timu pinzani kufanya ushirikina jambo ambalo halikuwa kweli.

Alisema tukio hilo lilimsikitisha sana kutokana na kwamba kesi yake ilifikishwa mpaka kwa wakuu wake wa kazi.

“Nakumbuka ilikuwa mwaka jana (2020) siku ya mchezo kati ya Zimamoto na KVZ, nilivumishiwa kwamba Zimamoto waliingia katika chumba cha KVZ, wakati haikuwa kweli na siku hii sitoisahau katika maisha yangu maana kesi ilikuwa kubwa”, alisema.

Hata hivyo, anasema kuwa pamoja na watu wengi kudhania kuwa mara nyingi mshughulikiaji wa  uwanja hasa  vyumba vya  wachezaji,  anatumiwa  kuweka  vitu vya kishirikina siku ya mchezo au kabla, lakini yeye hajawahi kufanya hivyo.

“Sijawahi wala sitowahi maana najua madhara yake, kwani hapo nyuma alikuwepo mzee mmoja ambae ameshafariki alifanya hivyo na alipooza miguu”,alisema.

Alifahamisha kwamba vitendo hivyo vinakuwa vinafanyika hasa kwa wenyewe viongozi wa timu na mara nyingi huvifanya siku ile ile ya mchezo, lakini sio kwa majira ya usiku.

Alisema kuwa wakati mwengine huja labda saa moja kabla ya mchezo au masaa mawili, lakini inakuwa ni siku ya mchezo ambao inakuwa yeye anachukulia kuwa ni muda wake wa kuanza kazi yake.

“Vinafanyika na wala sikutanii kwa hili, lakini wapo wanaokuja kufanya kwa siri na wengine kwa dhahiri ambao hata wewe mwenyewe ukiwa ni mdau mkubwa wa kuingia uwanjani hapa unayaona”, alisema.

Simai aliongeza kwa kusema “Ni  kweli watu huja wakafanya vitendo vya kishirikina na hata baada ya mechi utakuta vitu chumbani kama herizi, vikaratasi vilivyoandikwa maandishi ya Kiarabu na makombe yaliyotapakaa”.

Akizungumza kwa  kujiamini  na  kuonesha  kuijali kazi hiyo,mfanyakazi huyo  alifahamisha kwamba wakati mwengine anapokuta vitu kama hivyo huwaita wenyewe na kuwataka waviondoshe na yeye baadae kufanya kazi yake ya usafi.

Hata hivyo, alisema kuwa pamoja na kuwa vitendo hivyo vinafanyika, lakini hajawahi kutoa taarifa kwa yoyote.

“ Hii  ni  kwa sababu matendo ambayo yanafanyika sio siri maana mengine yanakuwa yanafanyika uwanjani mbele ya hadhara ya watu, ingawa mengine yanafanyika kwa siri”, alibainisha.

“Wengine wanajua ni utani kumuona mtu anamwaga maji, lakini wakati mwengine inakuwa kuna ukweli ndani yake”,aliongeza.

Alisema  mara nyingi vitendo ambavyo hufanyika utakuta mara timu  haiingii vyumbani mpaka atoke mtu mmoja kwanza au wengine hufikia  uwanjani moja kwa moja.

Aidha,  alisema  timu  nyingi zina  imani sana  na ushirikina kiasi kwamba  nyengine hukataa kupitia mlango wa kuingilia wachezaji.

“Kwa hapa kwetu hakuna timu ambazo hazirogi, lakini wengine hawafanyii hapa uwanjani bali huja kumalizia tu na wengine wanazidiana, lakini siwezi kuzitaja kwa majina”, alisema.

Alifahamisha kwamba masula hayo yanafanyika kila kukicha, lakini yeye huacha na kuendelea na kazi yake kwa kuwa mambo hayo huona yeye kama yeye hayamuhusu.

“Kuna matukio hufanywa kwa siri na mengine kwa dhahiri, maana wakati mwengine nimo ndani utasikia kitu kinapigwa ukitoka humuoni mtu au hata kama ukimuona humjui”, alisema.

Changamoto nyengine anayopitia ni ya  kikazi zaidi ambapo  watu hutaka kupita zaidi ya idadi ambayo wanatakiwa na anapowakatalia huonekana mbaya.

“ Kwa utaratibu timu inatakaiwa kupita na watu 37, lakini wakati mwengine huja mpaka na watu 40 au zaidi, jambo ambalo hunipa wakati mgumu”, alifahamisha  Simai akionesha  kukerwa  na ubabe wanaotumia  viongozi wa  timu.

Hata  hivyo,  Simai  anasema kuwa mafanikio ambayo anayapata ni  kupata ushirikiano mzuri na wafanyakazi wenzake pamoja na kupata umaarufu mkubwa kwa viongozi na wachezaji ambao wengi wao humfanya kama babu yao.

Simai  ambae anatarajia kustaafu mwakani (2022),anasema  kuwa pamoja na kuwa ni kazi rahisi, lakini sio hivyo kwa sababu kuna utaratibu wake ambao kama muangalizi unatakiwa kuufata.

“Mwanzoni nilikuwa naiona kazi nyepesi, lakini kumbe sivyo ila kwa sasa nimeizoea na ndio naendelea nayo”, alisema.

Hata hivyo,  kwa  upande  wa ushabiki anasema kuwa yeye ni mpenzi na mshabiki mkubwa wa timu ya Simba na kwa Ulaya  Manchesta United na kwa Zanzibar hana timu ambayo anaishabikia kutokana na mzingira yake anayofanyia kazi.

“Siwezi kuwa na timu hapa na hata kama nnayo, lakini imo ndani ya moyo wangu kwa sababu nikiweka dhahiri kutokana na mzingira ya kazi yangu watu watakuwa na mashaka na mimi siku itakapokuwa inacheza. Kwa hivyo, nimeamua kuwa kimya na timu za hapa”, alisema.

Sambamba na hayo Simai anaiomba   Wizara ya  Habari  kuviangalia upya vyumba vya wachezaji kwa kuvifanyia matengenezo kutokana na kuchakaa na  kuwa katika  hali ya kisasa.

Anasema katika vyumba hivyo kunahitaji matengenezo ili viweze kwenda sambamba na vigezo vya kimataifa.

“Zamani katika vyumba hivyo kulikuwa na mabenchi ya kukalia waalimu, lakini sasa hayapo na badala yake wakati wa mechi za kimataifa hulazimika kuweka viti”, alibainisha.

Hata hivyo, anasema kwa kuwa viongozi ambao wameteuliwa kushika nyadhifa ndani ya wizara hiyo baadhi yao wanalijua hilo, ni imani yake kwamba watalifanyia kazi.

Simai akitoa  ushauri wake  atakapostaafu ansema  mtumishi wa umma ambae atapata nafasi hiyo ashirikiane vyema na wachezaji pamoja na viongozi, ili aweze kwenda nao sambamba.

“Hii sehemu ni ngumu na mtu ambae anawekwa hapa asiwe mkali, atumie busara na hekma hasa kwa mechi za ndani ambapo idadi ya kuingia watu inakuwa inapitiliza kwa kutaka kuingia wengi badala ya 37 ambao ndio kwa mujibu wa kanuni na sheria”, alisema.

Juma Makungu Sima ana mke mmoja na watoto wanne wakiwemo wawili wanawake na wawili wanaume.