NA HAFSA GOLO

MBUNGE wa Jimbo la Donge, Dk. Khalid Salum Mohamed, amewataka wajasiriamali kutumia vyema   maonesho ya   sabasaba  kwa kubadilishana uzoefu sambamba na kuhakikisha   bidhaa zao zinakuwa  na ubora na viwango vinavyostahiki.

Waziri Khalid ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais ,Sera na Uratibu wa Baraza la Wawakilishi aliyasema hayo  wakati alipokuwa akiwaaga kikundi cha  wajasiriamali wanawake  wa jimbo la Donge kinachoelekea nchini Tanzania Bara katika maonyesho ya saba saba.

Aliwafahamisha kwamba maonesho ya aina hiyo yana umuhimu  katika kuinua biashara ,kupata soko la kuuza biadhaa wanazozalisha,kubadilishana uzoefu miongoni mwa wajasiriamali sambamba na kujenga mtandao wa pamoja.

“Hakikisheni  safari yenu  ni moja ya fursa muhimu ya kuongeza kipato na kuongeza ujuzi katika uwajibikaji wa majukumu yenu ya kila siku”,alisema.

Alisema katika maonesho hayo lazima wawe wabunifu katika kusarifu bidhaa wanazozizalisha, ili ziweze kupata soko zaidi la ndani na nje ya nchi na la utalii kwani   limekuwa sana kutokana na mpango wa serikali  wa kukuza sekta hiyo.

Pamoja na hayo Dk.Khalid aliwafahamisha wajasiriamali hao kwamba maonesho kama  hayo yatawasaidia wao na  wajasiariamali wengine wa Zanzibar kuwajengea uwezo wa kushiriki katika maonesho mengine makubwa yanayofanyika katika nchi mbali mbali jambo la msingi ni kuhakikisha bidhaa zao zinakuwa na sifa na ubora ambao utawavutia wateja mbali mbali .

Hata hivyo, alisema ,serikali ya Mapinduzi Zanzibar imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha wajasiriamali wote  nchini wanaweza kutumia fursa sambamba na kuwajengea mazingira wezeshi ya kupata mitaji kupitia mfuko wa uwezeshaji wananchi.