NA NASRA MANZI,WHVUM

WAZIRI wa Habari,Vijana, Utamaduni na Michezo Tabia Maulid Mwita juzi  amewaongoza viongozi wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo  na  Wizara ya  Elimu katika mapokezi ya wanamichezo walioshiriki mashindano ya Umisseta huko Mtwara.

Mapokezi hayo yaliyoanzia bandarini hadi katika ukumbi wa Sheikh Idrissa  Abdul Wakil kwa kufanyiwa sherehe ya aina yake.

Akizungumza baada ya kuwapokea wanamichezo hao huko bandari ya Zanzibar Malindi ,waziri huyo alisema serikali kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo   itaendelea kuimarisha na kurejesha haiba ya  michezo ili kuibua vipaji sambamba na  kuipatia sifa Zanzibar  katika michezo mbali mbali.

Alisema michezo  ndio nembo ya nchi,hivyo   ni vyema vijana kutumia  michezo na sanaa kwani ndio chachu ya maendeleo katika maisha yao.

Aidha alisema ubingwa walioupata katika michezo mbali mbali ya Umisseta ni kuunga mkono jitihada za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwinyi katika kuinua  na kuimarisha michezo.

Tabia aliwataka wanamichezo kusoma kwa bidii ili kuwajenga katika michezo kwa lengo la kuibua vipaji vyao.

Aliwapongeza wanamichezo hao kwa jitihada walizozionesha kwani wameitangaza Zanzibar kuwa bado vipaji vipo na vinaendelezwa.

Kaimu Mkuu wa Divisheni ya Michezo Idara ya Michezo Wizra ya Elimu Mussa Abdulrabi Fadhil, amesema katika kuhakikisha michezo wanaimarisha mwakani ameomba kuongezwa wachezaji kutoka  kisiwani Pemba ili kufikia malengo zaidi.

Nae Mratibu Idara ya  ya Michezo na Utamaduni Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali  Pemba  Mzee Ali Abdalla ameiomba Wizara ya Elimu kuzidi kusimamia sera ya elimu kupitia Idara ya michezo ili kusudi kuimarisha sekta ya michezo maskulini kwa vitendo na nadharia.

Kwa upande wa wanamichezo hao Kanda ya Unguja na Pemba wameipongeza  Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo pamoja na Wizara ya Elimu kwa kuwaunga mkono Vijana wao kwani imewapa ari na nguvu ya kuendeleza vipaji vyao.