NA MAULID YUSSUF, WEMA

WAZIRI wa Habari, Vijana, Utamduni na Michezo Tabia  Maulid Mwita, amesema , bado juhudi zinahitajika ili kuendeleza vipaji vya wabunifu wa sinema nchini.

Akizungunza wakati wa hafla ya usiku wa zawadi wa Tamasha la Kimataifa la filamu Zanzibar, (Zanzibar International Film Festival), ukumbi wa Ngome kongwe, ambapo hutuba yake ilisomwa kwa niaba   na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Simai Mohammed Said.

Alisema kuimarisha tamasha hilo kutasaidia sana kuibua vipaji vya vijana na kuitangaza Zanzibar kiutalii zaidi pamoja na kupelekea jina la Tanzania liendelee kukua nchi za nje.

Aidha alisema akiwa mwenye dhamana ya elimu nchini ata hakikisha anainua vipaji  katika skuli mbalimbali, ili kukuza tamasha hilo kwa kuwa na wabunifu wazalendo.

Mapema Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya ZIFF  Hassan Mitawi alisema tamasha hilo, linaleta  muamko kwa Wazanzibari  katika suala la utunzaji mazingira bila ya kuharibu mila zao.

Alisema tamasha hilo linawakilisha maonesho mbalimbali ambayo yanaelimisha na kuihamasisha jamii juu ya kujilinda na maradhi, kulinda mazingira  na kudumisha mila na tamaduni za kizanzibari hali inayopelekea  Zanzibar kuzidi kujulikana duniani kote na kuwa  kivutio kikubwa cha utalii.

Nae  Mkurungenzi wa ZIFF  Martin Muhando alisema tamasha  la ZIFF linawasilisha utamaduni wa Zanzibar, pamoja na wakaazi wake hasa katika masuala ya utamaduni wao ambapo huwavutia sana wageni wanaokuja kutembelea visiwa vya Zanzibar.

Alisema kutokana na mazingira mazuri na ukarimu  wa watu wa  Zanzibar   imepelekea kuwa na ongezeko la  wadhamini na wadau wengi ambapo pia linaongeza furaha na amani  kwa wageni na wenyeji wa visiwa vya  Zanzibar.

Aidha wameiomba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuendelea kulisimamia  tamasha hilo ili libaki Zanzibar kwani ndio asili ya Tamasha hilo.

Tamasha la 24 la ZIFF limeshirikisha jumla ya filamu 67, ikiwa filamu 11 kati ya hizo zimeonekana kufanya vizuri kwa mwaka huu,  ambapo filamu ya RUPIA imeshinda tunzo ya EMARSON kwa mwaka 2021.

Hafla ya usiku wa zawadi ni miongoni mwa shamrashamra za 24 za tamasha la Zanzibar International Film Festival ambazo hufanyika kila mwaka visiwani Zanzibar.