NA NASRA MANZI, WHVUM

WAZIRI wa Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo Tabia Maulid Mwita  amepokea shilingi 10,000,000 kwa ajili ya ufadhili wa ligi kuu Zanzibar.

Hafla hiyo ilifanyika ukumbi wa wizara hiyo Migombani, ambapo Katibu Mkuu mstaafu wa wizara hiyo  Omar Hassan ‘King’, alimkabidhi  waziri Tabia kiasi hicho cha fedha.

Akizungumza mara baada ya kupokea fedha hizo Tabia  alisema ni vyema wahisani na wapenda michezo kuendelea kushirikiana na wizara  ili kurudisha hadhi ya soka kama zamani.

Alisema Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo itahakikisha misingi,kanuni na sheria za mpira zinafuatwa ili mpira wa Zanzibar upige hatua.

Alimshukuru katibu huyo mstaafu kwa jitihada alizozichukua yeye binafsi pamoja na uongozi wa skuli ya Glorious kwa kutoa fedha hizo ili kuhakikisha ligi kuu inaimarika.

Katibu Mkuu Wizara ya Habari,Vijana Utamaduni na Michezo Fatma Hamad Rajab alisema wizara itaendelea kushirikiana na wadau,wafadhili na wadhamini katika kuleta mafanikio ya mpira ili kupiga hatua ya kimaendeleo.

Nae Katibu Mkuu Mstaafu hiyo Omar Hassan ‘King’ ameipongeza wizara kwa kazi ya kukuza na kusimamia taasisi za  michezo ili kuleta mabadiliko ya michezo katika nchi.

Aidha ameziomba klabu za michezo pamoja na vyama vya michezo kushirikiana pamoja, jambo ambalo litaleta ushindani  na kupeleka soka mbele.