• Kuna mabadiliko makubwa
  • Huduma zote muhimu za jamii zote zinapatikana
  • Sasa wanajenga mji mpya
  • Kipindupindu sasa basi wanajenga na kutumia vyoo

Amina  Ahmed  , Maelezo, Pemba  

NI Takriban dakika 15 kwa mwendo wa miguu na dakika tano kwa usafiri wa daladala  au wa binafsi kutoka Madenjani   hadi kufika katika barabara kuu iendayo   bandari ya Likoni kuelekea kisiwa cha Kojani .

Eneo la Madenjani ni lango kuu la kuingilia na kutoka  katika miji maarufu   ya Kisiwa cha Pemba kama vile  Chake Chake, Wete na Micheweni,  ambapo barabara hiyo ndiyo ya  kuelekea kisiwani humo.

SAFARI YA KOJANI

Ukiwa hapo  Madenjani utaacha njia zote na kufuata barabara iendayo Micheweni,  ndipo utakutana na bango kubwa linalokuashiria njia  ya ndani ya kuelekea kisiwa cha Kojani.

Ni umbali wa dakika 10 hadi 20 kutoka bandari ya Likoni   hadi kufika ndani ya kisiwa cha Kojani kwa kutumia   vivuko vya majini ambavyo ni  Ngalawa , Mashua, Dau au boti za kisasa za Faiba(fibres) , ambazo zote  hazitumii mashine.

Kisiwa cha Kojani kipo nje kidogo na mji wa Wete, mkoa wa Kaskazini Pemba na ni maarufu kwa shughuli za uvuvi na  utamaduni wa kipekee  wa  watu wake wajulikanao kwa  jina  la “Wakojani”.

Ukiwa katika kivuko kuelekea kisiwa cha Kojani kwa fikira za haraka unaweza kuhisi  kuwa kisiwa hicho hakina wakaazi wengi ndani yake , lakini kumbe  ukweli haupo hivyo.

Muonekano unaokukaribisha kisiwani Kojani ni wa  tofauti kutokana na  baadhi ya  nyumba  nyingi za makaazi ya watu kuwa  tafauti na  kwengineko kisiwani Pemba.

Nyumba hizo zinaonesha haiba  na muonekano wa kipekee  katika ramani  unayoiona na  hasa  kushonana sana na  chochoro  kama vile mji mkongwe  wa  Zanzibar, ila wao  nyumba  zao ni za  chini.

Mandhari ya ujenzi wa kisiwa hicho unaweza ukadhani kwamba ni  nyumba hizo  zimehamwa au hazina uwezo wa kuhimili kukaa familia zaidi ya moja, lakini upekee wa wakaazi wa kisiwa hicho  ni wa kushangaza.

Kwa vile nilikuwa na shauku na hamu ya kutaka kujua hali ya kisiwa cha Kojani na asili yake nilianza udadisi wangu kabla sijateremka kwenye chombo nilichopanda.

Kwa mujibu wa wenyeji  wa  kisiwa hicho walinisimulia kuwa asili ya jina la   Kojani limetokana na neno “Kujini “  ambalo chanzo chake lilianza na mahojiano maalum kati ya wageni hao wa mwanzo ambao walikuwa peke yao  kisiwani humo.

Watu wa mwanzo waliofika katika kisiwa cha Kojani nilisimuliwa kuwa waliwaona majini ndani ya kisiwa hicho na kujaribu kuzungumza nao kwa lugha zao, kwa   majini kuuliza watu hao KUJINI  wakiwa na maana ya kuwa“mumekuja kufanya nini “  na majini hao wakajibu “tujitukaa “wakiwa na maana ya kuwa tumekuja kukaa (kuishi) .

Kwa mujibu wa simulizi inaelezwa  kuwa watu wa mwanzo walioingia ndani ya Kisiwa cha Kojani walikuwa ni wageni  waliotokea sehemu za Iran, ambao idadi yao ilikuwa ni wanaume wawili waliojulikana kwa jina la Shah  Kombo na Shah Simai.

Kwa vile wageni hao waliendelea kuishi katika kisiwa hicho walikuwa peke yao walilazimika kutafuta wanawake katika maeneo mbali mbali ikiwemo Kenya na kuja nao katika kisiwa hicho na kuanza kuzaa na kuzaana.

Vizazi hivyo  viliendelea   na wengine kujitokeza kutoka maeneo mbali mbali  katika mwambao wa Pwani ya Afrika Mashariki ndipo walianza kubadilisha neno KUJINI mpaka kutamkwa ‘Kojani’.

Kisiwa hicho kwa sasa  kina wakaazi zaidi ya elfu kumi  na tatu (13,000), ambapo wapo wale ambao hawaishi katika kisiwa hicho  wamehama kutokana na harakati za kimaisha, lakini  ni zao la asili na ni  ‘Wakojani’.

Kutokana na kukua kwa mji huo Serikali iliamua kufanya kisiwa cha Kojani kuwa ni wilaya ndogo   ambayo huduma zote muhimu za kijamii zinapatikana katika  kisiwa hicho, ambacho kwa ujumla kina shehia mbili shehia ya Kojani na shehia ya Mpambani .

WAKOJANI NA UCHUMI WA BULUU

MWANDISHI wa makala haya akizungumza na mmoja wa wazee wa Kojani alipofika kisiwani humo kufanya mahojiano juu ya kisiwa hicho.

Harakati kubwa za wakaazi wa kisiwa hicho kwa upande wa akina baba ni uvuvi, lakini kwa upande wa kina mama ni kilimo cha aina mbali mbali kama vile mpunga, mihogo, mtama na kadhalika kwa ajili ya chakula na sio biashara na ususi wa mikoba, mikeka, vipepeo  na makawa  kwa ajili ya biashara.

Kijana Bakari  Hassan  Bakari   mwenye umri miaka 31, aliyezaliwa na kukua  katika kisiwa cha Kojani , anasema  tokea   kuwa na fahamu zake yeye anajishughulisha na  uvuvi    wa samaki katika bahari ya Hindi  na kazi hiyo alijikuta anairithi kutoka kwa baba yake mzazi.

“Mimi ni mvuvi  na nimekulia katika shughuli hizi ambazo nimezirithi kidogo kidogo kutoka kwa baba yangu mzazi, nilipokuwa mdogo nilikuwa  namfuata baharini   mpaka  nilipokuwa na mimi nishakuwa mzoefu hadi wakati huu  sina harakati nyengine isipokuwa uvuvi”,alieleza .

Hata hivyo, Bakari  anasema shughuli ya uvuvi kwa sasa   zimekuwa na ugumu kutokana na  kukosa nyenzo  za kisasa za kuvulia, kwani kama unataka kupata samaki wenye kuingia sokoni lazima ufike kwenye bahari kuu ambako kuna hitaji zana za kisasa.

“Tangu awali mimi nakumbuka nilikuwa navua kupitia vyandarua  nyavu za matundu madogo , mishipi ya ndoana  na tulikuwa tunavua popote  palipokuwa na bahari,lakini kwa sasa  hali imebadilika  ukivua kutumia nyavu ushakuwa na ugomvi na serikali kuna maeneo ukivua ushaingia mipaka ya hifadhi. Kwa kweli uvuvi sisi wakaazi wa Kojani kwa sasa umekuwa mgumu tunafanya kwa hayo hatuna kazi nyengine tu”, alisema.

Baadhi ya wazee ambao bado wanaendeleza harakati zao za kimaisha, kupitia makala haya wameiomba serikali kuwaandalia mazingira  mazuri yatakayowasaidia  wavuvi ambao hawatumii uvuvi  wa bahari kuu,  kuweza kufaidika na bahari kwa kuwasaidia na kuwapa  elimu na mbinu za uvuvi  unaotakiwa na serikali, ili kuendana na sera ya Uchumi wa Buluu.

“Sisi watu wa Kojani asili yetu  ni uvuvi  na serikali isione kwamba tukivua tunakosea ikatufunga au tukaanza kuwa mahasimu  watutafute wavuvi  wazungumze na sie,   kama  sisi tumefanya kazi ya uvuvi kwa urithi watupe izo mbinu  za kisasa,  lakini wanatoa maagizo tu hawatufiki wakatupa elimu  na ndio maana ugomvi na serikali juu ya  uvuvi  haumalizi ‘’, alisema   Mzee Mbarouk Hassan (Maarufu mzee makuti).

“Uchumi wa buluu  sidhani kama  umetuangalia  sisi watu wa Kojani kwa sababu  wavuvi wengi  tunatumia bahari ya Hindi   kuvua, leo serikali imewaza  bahari kuu   kwa hiyo  si wote ambao harakati za uvuvi wanatumia bahari kuu,” alifahamisha akitamani kushirikishwa  katika uvuvi wa kisasa.

Aidha aliongeza “Serikali kupitia Wizara ya Uchumi wa Buluu watuwekee  Mkojani mwenye uzoefu na uvuvi  kwa sababu  wakazi wa Kojani ndio wavuvi, tumetapakaa  ulimwengu nzima ambapo hata wazungu wanaiga tu kwa  Mkojani,  mbinu na  uzoefu unaotusaidia ni kuonekana thamani ya mvuvi Tanzania mzima , lakini asiyejua  uchungu na uvuvi, sifikirii kama  kuna atakaeona umuhimu wa mvuvi ,’’.

Aliendelea kusema uvuvi hautaki kompyuta, bali   unataka uzoefu kwa maana mtu  akilala  na kuamka  akisikia mlio wa maji tu  anajua leo baharini kunaendeka au hakuendeki, wakati   kompyuta hazina akili za uvuvi kama  uzoefu wa watu wa Kojani.

‘’ Serikali tunaiomba ije Kojani isikilize kilio chetu wavuvi wenye uzoefu, kama kweli imedhamiria kuenda kwenye uchumi huo wa buluu”, alisema Yussuf  Salim Bakari.

Baadhi ya akina mama ambao wanajishughulisha na ususi  wa mikoba mikeka na makawa  walisema   kazi hiyo na wao walirithi kutoka kwa wazazi wao .

“Mama yangu alikuwa ni mpakasaji maarufu wa mikeka na mikoba, na baba yangu ndio alikuwa muuzaji wake huichukua mikoba na mikeka kuvuka kwa kidau kuenda nayo mijini  kuiuza  na mimi kwa sasa naendeleza kazi hiyo ingawa mume wangu kuchukua kuenda kuuza haendi nalazimika kuchukua mimi mwenyewe  kuenda nayo,” alisema Bi Time Mwiyaka wa Kojani.

Anasema kwa vile hana muuzaji wa uhakika sio mara nyingi kuenda nayo nje ya kisiwa cha Kojani, ila inanibidi ashone na kuiuza humo humo ndani,  jambo ambalo linampunguzia soko.

Akizungumzia Soko la uhakika la kuuza bidhaa zao  hizo wanazozalisha kwa  mikono yao, anasema ndio limekuwa tatizo kwa sababu  walianzishiwa kikundi hapo Kojani na aliegombea  urais  wa Zanzibar kupitia chama cha NRA.

Alisema  aliwaahidi kuwawezesha, lakini hakuwawezesha na wao  uwezo wa kujiwezesha hawana kwa maana hiyo kikundi  kikashindwa kuendelea kikafa mpaka leo.

Bi Time anawaomba wadau pamoja na  serikali na wadau wa harakati za wanawake  wawaangalie wanawake wa kisiwa hicho kwa kuwasaidia upatikanaji wa soko  la biashara zao.

LAHAJA  YA KIKOJANI

Baadhi  ya Lafudhi  halisi ya kisiwa cha Kojani  kwa  asieyekuwa mkaazi wa huko  inataka umakini kuelewa ni kama zilivyo lafudhi nyengine za visiwa vidogo vidogo ikiwemo Tumbatu na maeneo mengine kama  vile Micheweni.

Wakaazi wa kisiwa cha Kojani wana Lafudhi kama hizo ni kama unaweza ukasikia   maneno kama ‘Kufisa’ ikiwa na maana ya kumsindikiza mgeni, ‘Kubauwa’ ikiwa na maana ya kujisaidia haja ndogo, ‘Kukeleshi’ ikiwa maana yake ni  kukaa kitako.

Nyengine ‘Kudaukia’ hii nayo ikiwa na maana ya kujulia hali majirani,’

‘Kutongoa’ maana yake ni kuzungumza, na mengi mengineyo.

Hata hivyo, inasemekana wakaazi waliowengi katika kisiwa cha Kojani wana asili ya Kenya na Mombasa (Wagunya) kutokana na wale wanawake wa kwanza waliohamia  walichukuliwa huko na ndio walioanzisha kizazi  mpaka leo. Na hadi leo  Wakojani hupendelea kufanya shughuli za uvuvi wakiwa huko nchini Kenya.

Aidha, utamkwaji wa lugha za mwambao kwa vizazi vilivyozaliwa kisiwani hapo na watu hao wa mwanzo zimekuwa ni maneno ya kujirudia rudia kwa vile ndio usuli wao.

KOJANI YA SASA

Zamani ukitaja neno Kojani wengi walikuwa walifahamu vyengine. Walikuwa na  fikra kuwa wakaazi wa huko ni wakaidi na  wasiopenda kubadilika.

Ni kweli ilikuwa hivyo, lakini Kojani ya leo sivyo ilivyokuwa  miaka kadhaa iliyopita. Kumekuwa  na mabadiliko makubwa na kuendena  na  cheo ilichopewa kisiwa hicho cha kuwa  wilaya  ndogo.

Katika kutembea yangu kisiwani humo nimegundua kuwa kisiwa  hicho kina sehemu ya  kale na  ya  sasa. Sehemu ya  kale kuna  nyumba  zilizoshonana  na  chochoro na  nyingi zimeezekwa  makuti na   ni nyumba  duni zikionesha hali ya umasikini.

Hata  hivyo, hali sio ilivyo hivi sasa, bali  kuna mji wa  kisasa unaojengwa  kwa  mpango na  nyumba  zake  ni za  matofali ya jasi zenye  vyoo na  pia vyumba  vya ‘self contain’.

Kojani niliyokuwa  nahadithiwa  na  nilivyoikuta ni tafauti kwa  hivi sasa. Mara  kadhaa kisiwa  hicho kilikuwa kikikumbwa  na maradhi ya Kipindupindu kutokana  na  wakaazi wake kujisaidia  pwani na mazingira  machafu, lakini hivi sasa wakaazi wana  mwamko wa kujenga  vyoo na  kuvitumia na  kuondokana  na tabia ya  zamani.Hata hivyo, matambara ya  watoto kukoshwa  pwani.

Hata  hivyo, suala  la taka  bado linasumbua wananchi, kwa  vile hakujakuwa  na mpango madhubuti wa  kudhibiti taka yaani ‘garbage  management’.

Nilipowasogelea  akina mama, niligundua kuwa  wanafuraha hivi sasa kwa  kuwepo Kituo chao cha Afya, ambacho huduma  zote hivi sasa  zikiwemo za kujifungulia wanapata  hapo.

“zamani ilikuwa tunavuka tunaenda Likoni na   Madenjani kwa huduma nyingi ikiwemo afya. Wengi tulikuwa tukijifungulia nyumbani”, alibainisha mwanamke mmoja huku akimuonea  haya mwandishi wa makala  haya.

Taarifa nilizozipata ni kwamba kituo chao hicho cha Afya kina madakatari wawili wanaokaa hapo na  wengine wanakuja  na  kurudi na  kwamba kimepunguza  sana shida iliyokuwepo zamani ya  kwenda Chwale.

Taratibu mwandishi wa makala haya alizunguka huku na  kule  na kujionea huduma  nyengine muhimu zilizozmo katika kisiwa hicho, ambazo ni maji na  umeme.

Kisiwa  hicho  hivi sasa kina umeme wa  uhakika  na  pia  maji safi na  salama, vyote  hivyo vimetoka  nchi kavu na  kwa kiasi kikubwa  vimewaondolea usumbufu na  dhiki kubwa   wakaazi wa kisiwa  hicho.

“Safari ya kuvuka kwenda Likoni na Madenjani kutafuta maji sasa hazipo. Twapata  maji  na  umeme hapa hapa”, alifahamisha msichana  mmoja.

Pitapita yangu kiswani humo nikakuta wakaazi wengi hivi sasa wana  mawasiliano ya simu za mikononi, tafauti ilivyokuwa hapo nyuma, na nilipotupa  macho huku na  kule nikaona minara  ya  ya mawasiliano ya  simu imejengwa  kiswani na  hakuna shida  ya mtandao(network).

Huduma  hii ya  mawasiliano ya  simu pia imesaidia sana  kwa  wakaazi wa kisiwa hicho, kupata  huduma  za kifedha kwa  kupitia hiyo tafauti na  hapo zamani.

Kuhusu usafiri wa  kwenda  na  kurudi  kisiwani humo, hivi sasa suala  hilo halina usumbufu tena. Kuna  usafiri wa  kutosha  na  wa kisasa kwa  kutumia  boti za  mashine na kuondokana  na kutumia tanga.

Nilipodadisi  zaidi  usafiri nikaelezwa kuwa  unatarajiwa  kuimarika zaisi kwa  kuwepo usafiri wa kisasa zaidi siku zijazo kwa  kuletwa  boti kubwa  na ya  kisasa. “Nasikia visiwa  vyote  vitapatiwa  usafiri huo”, alidokeza sheha.

Suala la uzazi salama  na mpango katika kisiwa  hicho, nilidokezwa kuwa  uzazi salama upo, kwani wengi wanajifungulia kituo cha afya hivi sasa.

Hata hivyo, uzazi wa mpango bado ni mtihani, kwani wanawake wanabeba mimba hata kabala yamuda wa kuachisha wa miaka miwili na uthibitisho ni kushuhudia watoto wa papo kwa papo tele.

Aidha, mabadiliko mengine kwa wanakojani hasa wanawake pia yapo husasan katika uvaaji wa nguo, kwani zamani ilikuwa zaidi kanga ya kifua kwa watu wazima na watoto kanga  ya  shingo, lakini kwa  sasa wanajitanda vizuri na  pia kuvaa  mashungi.

Wa zamani waliosema jana haiwi leo hawakukosea, kwani katika kisiwa cha Kojani taratibu vijana wanabadilika na kuona mila  na  desturi za  zamani zimepitwa  na  wakati,ambapo mila  ya mwaka  wa Kikojani hivi sasa hauna   nguvu sana  kama zamani.

“Vijana wanaona mambo haya yamepitwa  na  wakati na  wa zamani ndio wanatoweka, basi ni hatari. Kilichobaki  kwa sasa ni kuheshimu wakubwa. Hilo lipo hadi leo”, alisimulia sheha.

Kadhalika ngoma  za  asili nazo kisiwani humo nyingi zimekufa na  vijana wanashuhgulika zaidi na muziki wa kisasa katika  simu zao.

Juu ya  hali wanawake  wajane  katika kisiwa  hicho, mkaazi mmoja  alidokeza kuwa mwanamke akiachika miiko yao haruhusiki kuishi katika nyumba peke  yake ikiwa ni kuchelea  kuingia  katika maovu.

“Akiachika ntu nke hakai pekee bali arudi kwao na kukaa na watu. Si ruhusa kukaa pekee”, alifahamisha kijana mmoja.

CHANGAMOTO

Mara nyingi ndo za utotoni ni tatizo kwa jamii hasa katika jamii za vijijini. Suala hili kwa wakaazi wa Kojani limekuwa ni tatizo na bado hakujakuwa na mwamko wa kuleta mabadiliko.

Nilipodadisi ndoa za mapema nilielezwa kuwa tatizo hili lipo la wasichana kuozeshwa mapema. Jamii ya Wakojani inaamini kuwa msichana akifika miaka 15 aolewe, kwani ni umri muafaka na yasije yakatokea mengine.

Wanakojani wanaamini kuwa msichana akifika miaka 21 hajaolewa inakuwa ni nuhsi na kupata mikosi hapo baadae ya kukosa kuolewa.

“Mtoto wa kike akifika miaka 15 anastahiki kuposwa na kuolewa, ikizidi miaka 21 hajaolewa ni kama anaitia mikosi familia”, alisema bwana mmoja mzee.

Wazawa wa Kojani wametapakaa sehemu nyingi ikiwemo Kenya, Bara na Unguja. Hata hivyo, wana sifa kubwa ya kuthamini kwao na mara nyingi kuna baadhi ya misimu kurudi kwa wingi.