• Ni rahisi kufuga baada ya kupata  ushauri wa  wataalamu

  • Yana soko zuri ndani na nje  ya nchi

  • Ni utekelezaji wa Uchumi wa Buluu

     Na Thureya Ghalib, Idara  ya  Habari Maelezo, Pemba

NENO Uchumi wa Buluu lilikuwa geni miongoni mwa wananchi wengi wa Unguja na Pemba. Walikuwa wakifahamu mazingira yaliyowazunguka tu ya bahari na katika bahari kazi kubwa ni uvuvi wa samaki na kidogo ukulima wa mwani.

Katika Awamu hii ya Nane imekuja na Sera ya Uchumi wa Buluu , ambayo ni kutegemea bahari katika kuimarisha uchumi kwa  njia ya uvuvi, mafuta,  ufugaji wa viumbe vya bahari, gesi asilia na  mengi yanayohusiana na bahari.

Hivi sasa neno hilo likitamkwa linaleta faraja kwa kila mwananchi wa Zanzibar, kwani wengi hao wanalitafsiri kama ni ukombozi wa kiuchumi unaotokana na vilivyomo ndani ya bahari.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk, Hussein Ali Mwinyi, ameunda Wizara maalum ya Uchumi wa Buluu, ili kuweza kuwasaidia wananachi wake kuinua uchumi wa wao na Taifa kwa ujumla.

Dhamira  hiyo haina maana kuwa Rais amezitupa taasisi nyengine na kuegemea uchumi wa buluu  pekee  ,lahasha bali lengo lake kubwa ni kuwakomboa wananchi wake katika umasikni kupitia nyanja zote.

Katika kampeni zake za kuwania nafasi ya Urais wa Zanzibar katika kiwanja cha Skuli ya Micheweni, Wilayani humo  Mkoa wa Kaskazini Pemba, alizungumzia maneno haya:

“Nimekuwa nikizungumzia Uchumi wa Buluu katika hotuba zangu nyingi kwa maana ya utalii, uvuvi, mafuta, gesi na viwanda vinavyotumia malighafi za bahari, lakini haina maana tutasahau kilimo. Bado kilimo kitapewa kipaumbele”, alihutubia.

Kwa mukhtadha huo, wananchi wamekuwa wakiunda vikundi mbalimbali vikiwemo  vya ufugaji samaki,majongoo bahari na wakulima wa mwani ikiwa ni muitikio wa Uchumi wa Buluu.

Mwandishi wa Makala haya ameamua kugusia juu ya ufugaji wa majongoo bahari ,ili  kufahamu ni kwa  kiasi gani wananchi wameitikia  na namna  gani wanajikumu kimaisha  kupitia  ufugaji huo.

Mwandishi alililazimika kufanya  safari kufuata kikundi cha ufugaji majongoo, ambacho aliambiwa  ni safari ya  kwenda  kisiwani  kwa kutumia mashua yenye kukabiliana na  mawimbi ya bahari.

Haikuwa  safari rahisi mpaka  kufika  katika kisiwa cha Uvinje, kilichopo Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, ili kupata   kiundani  utaalamu wa  ufugaji wa majongoo ya pwani na namna wana kikundi wanavyofaidika na  changamoto zinazowakabili katika ufugaji wa viumbe  hivyo vya  bahari.

Safari ya Uvinje  kwa  salama  kabisa  tulifika  na  kulakiwa  na wanakikundi  cha Juhudi na Maendeleo  wa  Kisiwa cha Uvinje, chenye wanachama 12 wakiwemo akinamama watano na akinababa saba, ambacho kilianzishwa tarehe 16 Septemba,2019.

Baada  ya kusalimiana  na  kujuana  wanakundi walimueleza  mwandishi wa  makala  haya  kuwa wamehamasika na ufugaji wa majongoo  bahari kwa lengo la kujiongezea kipato, jambo ambalo linawasaidia katika kupiga hatua katika maisha yao ya  kila  siku.

Walieleza kila siku zinapozidikwenda, ndivyo wanavyozidi kuhamasika na  ufugaji wa majongoo hayo ,kwani wamekuwa wakipata ujuzi mpya kwa  waliotangulia katika ufugaji huo.

Akizungumza kwa  niaba ya wanakikundi hao Mwenyekiti wa kikundi hicho Sharif Hamad Haji, alisema  kuwa walihamasishwa na mmoja wa mfugaji wa majongoo kutoka kisiwa cha Kojani , na kuelezewa faida na changamoto zake  ndipo walipoamua kuanza rasmi shughuli hiyo.

Alifahamisha baada ya kupata taaluma hiyo, walianzisha shamba na kuunda kikundi cha watu kumi na mbili na kuanza ufugaji wa majongoo bahari kwa awamu ya kwanza.

Alisema kwa hatua ya mwanzo walipata  kasoro ndogo ndogo katika ufugaji wao, hivyo waliomba msaada kutoka Idara ya Maendeleo ya  Uvuvi wawasaidie kuwaongoza, ili kuondoa kasoro hizo.

“Mbali na kuwa Idara ya Maendeleo ya Uvuvi inachukua jitihada kubwa katika kutupa elimu na kusababisha faida kubwa kwetu,bali tunaomba wazidi kuwepo karibu na sisi kutueleza sheria zao ili tufanye shughuli zetu tukiwa salama,”alieleza mwenyekiti huyo.

Alifahamisha kuwa kwa  vile  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,  inapenda maendeleo kwa wananchi wake,  imechukua jitihada za makusudi kupitia Idara ya Maendeleo ya Uvuvi ikiwa  ni pamoja na    kufika katika  maeneo yetu,  kuona mashamba pamoja na kuyachukua majongoo kupelekwa katika maonesho mbali mbali.

Mwenyekiti huyo alisema kutokana na kuhamasika, uzalishaji ukaongezeka  na kulazimika  kuongeza ukubwa wa shamba  kutoka mita ishirini hadi  kufikia mita ishirini na saba.

“Tumerefusha mita za kinga (kuta) ambazo zitakinga wale wanaotembea tembea katika eneo la shamba, ili wasituharibie takriban mita 20, “alisema Sharif.

Alifahamisha kuwa Jongoo anaefugwa  huchukua muda wa miezi 8 mpaka  12 hadi kukua na kuvunwa kwake, na viumbe  hao hawana chakula chochote wanacholishwa isipokuwa chakula  chao hufyonza mchanga wa bahari ndimo wanapata  chakula.

Alieleza kuna aina nyingi  za majongoo bahari  wanayofugwa, lakini wao wanayo majongoo meupe  au maarufu ‘sandfish’  na walianza na ufugaji wa majongoo 13 na kwa sasa wanao zaidi ya 200.

Akielezea changamoto wananazozipata katika ufugaji huo, mwenyekiti huyo alisema  ni ukosefu wa taaluma kwa ajili ya ufugaji wa majongoo hayo  na wameiomba Serikali iwaletee wataalamu waje wawafundishe.

Alisema  changamoto  nyengine ni kukosa fedha za kujikimu kwa kuendesha  shamba  lao. “Hatuna  nyenzo za kurutubisha vizuri mashamba yetu. Fedha hatuna”, alisema  Sharif.

Akizungumzia Soko la majongoo, alisema lipo vizuri la ndani na nje, kwani jongoo mmoja  huuza  shilingi 5,000  na  kwa  soko la nje kilo moja ni zaid ya shilingi 80,000.

Alisema wao wanauza majongoo yakiwa mabichi, ambapo hadi sasa wanatumia masoko ya ndani tu na hawajawahi kusafirisha nje.

Hata hivyo, alieleza kuwa kwa sasa hawana mpango wa kupanua shamba lao, kwani hakuna mtu ama kiongozi yoyote aliyewasaidia tokea kuanzisha kikundi hicho.

Alifahamisha  kuwa katika  shamba  lao hilo wamewahi kuvuna mara tatu, na pesa walizozipata ziliwasaidia kujikimu kimaisha pamoja na kuendeleza ufugaji wao na kununua nyenzo za kujengea uzio.

“Tumevuna majongoo hayo mara tatu tangu tulipoanzisha  kikundi chetu ,na lile lengo la kujikwamua kimaisha limeweza kufikiwa”, alifahamisha  mwenyekiti Sharif.

Kwa upande wake mmoja wa mwanakikundi hicho Mboja Juma Makam, alisema lengo la kujiunga na kikundi hicho  ni kujikomboa na umaskini.

Alisema tangu ajiunge na kikundi hicho ameweza kufaidika na mambo mengi ikiwemo elimu  pamoja na kufahamu faida mbali mbali za ufugaji wa majongoo hayo.

“Kwa sasa naweza kupata mahitaji yangu ikiwemo kusomesha watoto,kupata chakula na mahitaji mengi ya kijami”, alisema.

Kwa upande wa msimamizi wa shughuli za ufugaji wa mazao ya baharini kutoka Idara ya Maendeleo ya Uvuvi, Mohamed Salim Othman, alisema shughuli hizi za ufugaji hapa Zanzibar zimeaanza katika miaka ya  karibuni na kwa upande wa Pemba tayari wamekwisha kuhamasika .

Alieleza hii ilifanyika mara baada ya kufanyika takwimu na kuonekana rasilimali yetu ya majongoo  baharini imeanza kupotea tofauti na hapo zamani.

Alifahamisha kuwa mara baada ya kuonekana hilo ndipo walipoamua kushajiisha wavuvi ama watu wanaokaa karibu na bahari kuweza kufuga majongoo ili  kuyanusuru yasipotee kabisa.

“Jamb lililosababisha kupotea kwa majongoo ni kutokana na  kuzidi shughuli za  uvuvi baharini ,hivyo tuliwazidi majongoo baharini  na kusababisha kuanza kupotea na ikabidi wanapozaliwa wengi hufa kuliko wanaokuwa hai”, alisema msimamizi huyo.

Msimamizi huyo aliendelea kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, imeamua kuwarahisishia wafugaji kituo cha kuzalisha  vifaranga Beit el Raas, ambapo miongoni mwa vifaranga hivyo ni  majongoo bahari, kaa na samaki wa mwatiko.

Alisema kuna mambo ya kuzingatia kabla ya kuanzishwa kwa ufugaji wa baharini, hivyo kabla ya ufugaji ni muhimu kuonana na mtaalamu ili aweze kuwapa elimu wafugaji.

Hata hivyo, alieleza ni vyema wananchi wakahamasika na ufugaji wa viumbe bahari, ikiwa ni njia nzuri ya kumuunga mkono Rais wetu wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi.