PORT-AU-PRINCE, HAITI
IDADI ya waliofariki kutokana na tetemeko kubwa la ardhi katika taifa la kisiwa cha Caribbean la Haiti imeongezeka na kuzidi 1,200.
Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.2 kipimo cha Richter lilitokea magharibi mwa Haiti, na kuharibu nyumba na majengo mengine katika eneo kubwa.
Serikali ya Haiti ilisema kwamba imethibitisha watu 1,297 wamefariki katika tetemeko hilo, huku takriban wengine 5,700 wakiripotiwa kujeruhiwa.
Serikali ilitangaza hali ya dharura na inafanya kazi kusaidia manusura licha ya machafuko ya kisiasa yaliyotokea baada ya mauaji ya Rais Jovenel Moise mwezi uliopita.
Serikali ya Merekani iliamua kutuma timu ya utafutaji na uokoaji huko Haiti. Mnamo mwaka 2010, zaidi ya watu 300,000 waliuawa Haiti lilipotokea tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.0 kipimo cha Richter.