• Ni Mkaazi wa Manyaga
  • Alikuwa akifikisha hadi pishi 30 kwa siku
  • Kilichomsukuma ni kushindana na wake wenza
  • Amefanikiwa kumiliki shamba la mikarafuu na ng’ombe  kwa  kazi hiyo.

Na Amina Khamis, Maelezo, Pemba

“ MCHUMIA JUANI HULIA KIVULINI”.Usemi huu sio wangu  bali ni wahenga waliokuwa wakikitukuza Kiswahili wenye  maana  ya  kuwa raha  haiji ila baada  ya  kutoka  jasho. Kwa  mana nyengine kuwa  mafanikio hayaji ila baada ya  jitihada  kupita.

Zanzibar  yaani Unguja na Pemba, imejaaliwa  na  kuwa na njia  za kipekee za uchumi wake  moja  wapo wa  njia  hizo ni zao la  karafuu,ambalo linachangia uchumi kwa  nafasi ya  pili baada  ya utalii.

Pemba ambayo maarufu kwa jina  la ‘Jazeratul khadhra’ kwa  maana  ya  kisiwa  cha  kijani, kimejaaliwa  kuwa  na  neema  kubwa  ya zao la  karafuu  kuliko Unguja ambako nazi ndio ilikuwa  zao kubwa zaidi .

Hali hiyo  iliifanya Pemba kufurika  watu wakati wa msimu wa  karafuu kwa  ajili ya  kuchuma  zao hilo na  wengine walikuwa  wakitoka  Unguja, kwa  vile  shughuli za kuvuna karafuu hufanywa kwa mikono.

Kazi ya  kuchuma  karafuu kwa kawaida hufanywa na watu wa  rika zote wakiwemo wanawake na wanaume na wakati mwengine hata watoto wakati wanapokuwa hawendi kusoma.

Mara  nyingi watu hutegemea  sana kibarua  cha  kuchuma karafuu kupata  mahitaji ya  lazima, na  hapo zamani vijana walikuwa  wakiutumia  msimu wa  karafuu kupata  mahari ya  kuoa.

Wengine walitegemea uchumaji wa  karafuu kwa  kujenga nyumba, kusafiri, kusomesha watoto, kuondoa nadhiri, kununua mahitaji mbali mbali kama vile vyombo vya usafiri na kadhalika.

Kihistoria wakati wa msimu wa karafuu watu walikuwa   wakijenga  undugu wa kudumu baina ya watu wa  Unguja  na  Pemba, kwa  kuwa wengine  walipata wake nyakati hizo za msimu wa kuchuma karafuu.

Misimu ya  karafuu ilizidisha  kukua  kwa  biashara  za kuuza  na kununua, kwani mbali ya  ya  waliokuwa  wakija kwa maamuzi yao, lakini pia  serikali ilikuwa  ikishajiisha  watu kwenda Pemba kuokoa  zao hilo.

Marehemu Bambuti na  ngoma  yake ya  Ndanda  kule  Donge  Unguja, alikuwa  akiimba  nyimbo za kushajiisha watu kuokoa zao la  karafuu kwa  kusema “Twendeni Pemba ee! karafuu tukachume…….”

Kwa vile uokoaji wa zao la karafuu kushirikisha watu wote wanawake na wanaume, nilikuwa  na  shauku ya kutaka  kujua namna watu walivyokuwa wanashindana katika uchumaji wa  zao hilo na  zaidi niliguswa  na  jinsi ya  kike.

Nilipouliza  baadhi ya  watu maarufu katika kambi za karafuu, walinidokeza kuwa wapo wanawake  maarufu katika  uchumaji wa zao hilo na wakiwashinda  wanaume.

Udadisi wangu ulizaa  matunda  na  kuambiwa  Wilaya ya  Mkoani kuna  mwanamke mmoja ana  uwezo mkubwa wa  kuchuma  karafuu na kuwashinda  hata  wanaume.

Nilifunga  safari hadi  Manyaga, Wilaya ya Mkoani kuonana na mchumaji karafuu maarufu mwanamke ili kuzungumza nae juu ya ujasiri wake huo wa kuutataga mkarafuu na kupata mavuno mengi tafauti na baadhi ya wanaume.

Ni umbali wa kilomita kadhaa hadi  kufika katika kijiji cha Manyaga, Shehia ya Mbuguani, Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba, lakini yote  ni kufanikisha safari yangu ya kumuona  mwanamke niliyesifiwa  kuwa ni mwanamke  wa shoka katika  uchumaji wa  karafuu.

Nilipofika  kama  kawaida  nilimsabahi na  kumuomba kuzungumza  nae anipe  mengi ya  uchumaji wa karafuu katika  enzi zake, kwani hivi sasa ni mtu mzima.

Nilianza kwa  kumuuliza  enzi zake ilikuwaje katika  uchumaji wake   wa karafuu na  hata akawa  maarufu na  kuwashinda hata  wanaume?

“Nikikumbuka enzi zangu na leo nilivyo kama kuna kuomba nirejeshewe umri fulani inakubaliwa basi mimi ningeliomba nirudi miaka 27 nyuma tokea kuzaliwa”, ni kauli ya  mwanzo ya  mama  huyo, ambae  kwa  sasa ni mtu mzima mama.

Kauli hiyo imetoka kinywani mwa Bi. Heshima Khamis Ali,  mwenye umri wa  miaka  70 sasa , aliyezaliwa Mgagadu, Shehia ya Minazini, katika Wilaya ya Mkoani ,na kwa sasa ni mkaazi wa Manyaga, ambako ameolewa  na mpaka leo hii licha ya kutengana na mume bado anakaa hapo hakuweza kuhama tena.

Bibi huyo kwa sasa ana watoto saba wakiwemo wanaume wawili  na wanawake watano, ambao baadhi yao wameshakuwa wakubwa na wanachuma karafuu, ingawaje hakuna aliyemfikia katika kuchuma karafuu nyingi.

Bi. Heshima  ambaye ni mtoto wa pili kuzaliwa katika familia ya Mzee Khamis kati ya watoto watatu wawili ikiwa ni wa kike,ambapo wenzake walilelewa na bibi na babu kutokana na mapenzi ya wazazi kumsaidia mtoto wao ulezi.

Akielezea kwa upande wa wazazi wake hawakumbuki kuchuma karafuu bali wao walikuwa wanakaa nyumbani kwa ajili ya kushughulikia karafuu tu kwa kuanika, kufuata mahitaji ya vibarua na kuzishafisha karafuu na makonyo yanapokauka kwa sababu zilikuwa zinazaliwa kwa wingi na siku za mvua ushughulikiaji unakuwa mkubwa kuliko kuchuma.

“Wazazi wangu hawakuweza kuchuma wao ilibidi wabakie nyumbani mvua ikiwa kubwa inabidi kazi ya karafuu inakuwa kubwa na uwe mstahamilivu, na kama jua kali inabidi uwepo zinazopasi uondoe ili upate majamvi uanikie tena kwa sababu karafuu zinakuwa nyingi kama hukufanya hivyo zinaharibika zinakuwa mpeta (karafuu nyeupe) unakosa bei”, alisema.

ALIVYOANZA KUCHUMA KARAFUU

WANANCHI wakishiriki katika zoezi la uchambuaji wa zao la Karafuu katika Kambi ya Bw.Said Salim Ali, katika Kijiji cha Bagamoyo Mtambwe Wilaya ya Wete Pemba Mkoa wa Kaskazini Pemba.(Picha na Ikulu)

Akiielezea  jinsi alivyoanza uchumaji wa karafuu alisema akiwa  mdogo wa  miaka  minane wazee wake walikuwa wanamiliki mashamba ya mikarafuu, na  hivyo  alifundishwa na vibarua waliokuwa wanachuma katika mashamba yao namna  ya  kuchuma  karafuu.

“ Kutokana na uzoefu huo niliendelea kuongeza kiwango changu  cha uchumaji siku hadi siku kulingana na umri wangu  ulivyoongezeka hadi kuwa  na  kasi zaidi ya  uchumaji”, alifahamisha  Bi Heshima.

Alisema ujasiri wake wa kuchuma haukuishia kwao alipokuwa mdogo, bali aliendelea nao mpaka pale alipoolewa ambapo alipofika kwa mumewe hali ilizidi kuendelea, kwani huko mikarafuu pia ilikuwepo na kulitokeza ushindani wa uchumaji wa zao hilo katika kijiji hicho.

“Huku nilikoolewa sasa naona ndiko nilipopata ari zaidi, kwani huku nilikutia wake wenza wawili nao pia walikuwa wachumaji kwa hiyo wayajua mambo ya ukewenza kwa hivyo  tulikuwa twashindana haswa”, alisema Bi. Heshima kuonesha kuwa hakutaka  kupitwa  na wake  wenza.

ANAVYOCHUMA KARAFUU

Alisema yeye kwanza  alikuwa hachagui mkarafuu wa kupanda uwe mkubwa ama mdogo, lakini alikuwa anapendelea zaidi kuchuma mikarafuu mikubwa kwa sababu anapopanda juu ya mkarafuu alikuwa ndio amefika, huchukua zana zake zote ikiwemo maji ya kunywa na kipolo cha  kumiminia.

Akizungumzia jinsi alivyoweza kuuchuma mkarafuu, alisema  kwa upande wake yeye alikuwa anauanza kuuchuma chini ambako ndio kugumu mpaka akifikia kati kati.

“Nikifika  hapo katikati inakuwa kwangu kama   kuchukua chakula  nakula wali na mboga kwenye mkeka wa Chole ama busati jipya kwa sasa”, alisema  Bi. Heshima kunasibisha na tamathali hizo za  semi.

“Siku ya mwanzo kuchuma kwenye mashindaoo ya ukewenza nilikwenda kutizama ustarabu (kusoma)wenzangu nguvu zao zikoje”, alisema.

Bi. Heshima (70) aliendelea kusema kwa vile kulikuwa na ushindani wa kuchuma, yeye ilikuwa anachuma mpaka anashindwa kuzichukua mwenyewe, kwa hiyo hupeleka ujumbe nyumbani na  huletwa mtu na mumewe kuja kusaidiwa.

“Huletewa  mtu  hasa kutokana na mabonde na milima katika maeneo tuliokuwa tunachuma. Ama  ataletwa punda au baiskeli kuchukua karafuu nilizozichuma kwa siku”, alisema.

Alifahamisha kuwa zinapofika nyumbani karafuu kwanza hawashughulikii kunyambua, bali huanza kupika, kufanya ibada sala ya alaasiri inawakutia njiani na baadae kula na wanapomaliza sala ya Isha ndio kazi ya kuchambua huanza kwa kusaidiwa na watoto wa mtaani.

Alibainisha kuwa uchambuzi wa karafuu kwa watoto waliupenda na ilikuwa zinamalizika haraka, kwani watoto hao walikuwa hawafuatii karafuu tu ilikuwa kunatolewa na Hadithi za Paukwa Pakawa na vitendawili.

“Wachumaji wa leo sijawasikia kutoa hadithi wala vitendawili na haya hivi sasa hayapo mabibi muda hatuna kwa watoto wetu na wajukuu waache watoto wamjue Zuchu na Daimondi watwambia wenda na wakati”, alisema Bibi huyo mwingi wa  kusema.

Kwa upande wa malipo Bi. Heshima  alisema  kuwa kibarua pishi ilikua inachumwa shilingi ishirini (20. “Ilikuwa  pesa ya noti  rangi ya zambarau  karafuu hazikuwa na pesa enzi hizo si kwa kibarua wala tajiri, lakini hicho kiliokuwa kinalipwa ilikuwa kinakidhi kutokana na mahitaji yaliokuepo, sambamba na mabadiliko ya awamu baada ya  awamu mpaka kufikia leo hii ya pishi shilingi 2000”.

“Mimi muandishi ndio mwanzo nilipokuambia nirejeshwe miaka ya nyuma ningelikubali kwa sababu kwa wakati huu ingelikuwa nnaweza kuchuma kwa CARRY ningelinunua, lakini leo siwezi tena mwanangu, ”alisema.

Kwa upande wa watoto wake ambae amemrithi kwa kuchuma karafuu alisema ni mtoto wa tatu kuzaliwa anaeitwa Suleiman  Mohamed  Ali (33).” Ana uwezo wa kuchuma mpaka pishi 25 kwa sasa”, alisema.

KIPATO ALICHOKIPATA

Alielezea  kuhusu kipato alichokipata kutokana  na kazi yake  hiyo, alisema  ilitegemea na mzao unavyokuwa, ikiwa mzao mkubwa na mambo yanakuwa makubwa na ikiwa mdogo na inakua hivyo hivyo madogo,lakini kulingana na umahiri wa uchumaji wake hakuwa  mkiani katika kipato.

“Bora mwanangu nisikutajie kima ninachokipata, lakini wa mwisho sitokei nikikwambia nitaambiwa najisifu nafikiri kushanielewa”,alisema.

Alisema alikuwa anachuma karafuu mpaka pishi 30 kwa siku, jambo ambalo halikuwa likimpa tabu kuchambua na kurejea tena kuchuma siku ya pili.

Bi. Heshima alisema  kuwa katika uchumaji wake  wa karafuu hakuishia huko tu alikoishi, bali pia  aliwahi kuchuma katika  sehemu nyengine ikiwemo Tironi, Shehia  ya Mbuguani na Kichunjuu, shehia  ya Mtambile zote  katika  wilaya  ya Mkoani.

MAMBO ALIOYAPATA KUTOKANA NA UCHUMAJI WA KARAFUU

Kuhusu maendeleo yake  aliyojifanyia kutoana  na uchumaji wa karafuu , alisema amefanya mambo mengi ya  kumasaidia.

“ Umaarufu wa kujuilikana na watu na nikiongozwa na aliyekuwa  mume wangu  aliniambia sote ni binaadamu tumeumbwa, kwa vile pesa ninayo baada ya kununua mahitaji yangu na kuwapelekea wazee chochote, nitafute kitu cha kuweka raslimali”, alisema.

“Kuanzia hapo  nilianza kununua ng’ombe ambapo ninaendelea nao mpaka leo hii,  nimejenga nyumba yangu, na ninamiliki shamba la mikarafuu ambalo ni la kwangu mwenyewe”, alifahamisha  Bi. Heshima.

Alisema kwa vile alihamasika tokea mapema tokea kwa wazee wake walikuwa na mikarafuu, kwa hiyo nae alijenga ndoto hiyo na yeye amiliki shamba lake la mikarafuu na aliweza kuifikia alinunua ardhi ambayo ilikuwa haina mikarafuu na akaanza kuipanda sasa anafaidika nalo.

TAFAUTI  YA UCHUMAJI WA ZAMANI NA SASA

Akitofautisha  uchumaji wa karafuu wa zamani na hivi sasa, Afisa kutoka Idara ya Makumbusho na Mambo ya Kale Pemba, Maalim Khamis alisema uchumaji wa sasa na zamani unatafautiana, kwani zamani unaweza kulitembea shamba zima bila ya kukuta matawi yaliyokatwa ya mikarafuu.

Alisema  hali hiyo ilionesha jinsi gani mti huu ulivyothaminiwa na waliomiliki na  walijitahidi kuzungumza na wachumaji wao wasiivunje, kwani kufanya hivyo husababisha  kila msimu unapowadia wa mwaka na Vuli uweze kuonekana na pande zote tatu ziweze kufaidika tajiri,mchumaji na kwa upande wa   serikali ndio huduma za kijamii zinavyoimarika.

“Watu walikuwa wanatengeneza ngazi ndefu ambayo imegawika katika sehemu tatu chini, juu ya kati  (matumboni ) na kileleni uchumaji huu unatumiwa na watu walioko nje ya mkarafuu bila kukerana na mwengine  ambae yeye anakuwa ndani ya mkarafuu tofauti na sasa hivi kama unakwenda mabondeni unachanganyikiwa kwa mikarafuu inavyokatwa”, alisema.

      WITO

Akitoa wito kwa jamii amesema katika miaka hii karafuu ilipopanda bei kumekuwa na tabia za ajabu tofauti na zamani, ambapo hivi sasa kunatokea mambo ya ajabu watu kuiba kwa kukata mikarafuu kwa mapanga, udhalilishaji mkubwa wa wanawake na watoto ikiwemo vitendo vya kikatili kudiriki hata watu kuchinjwa.

Aliiomba jamii kurejesha maadili yao ya zamani ya ukarimu kwa kuwakaribisha wageni, kwani ndio humo unamojengwa udugu na ndoa pia zilipatikana katika kipindi hicho.

“Sasa tuna mali kwa mali matajiri wameondoa imani kwa wachumaji wao, kwani kunatokea upoteaji mkubwa wa karafuu zao na baadhi mama wa kike wanadiriki kuzikanusha ndoa zao wanapokuwa mabondeni ili mradi warudi na karafuu”, alisema.

Alieleza  “sijaonapo “Mpeta “ wa pishi tano tumezidi na watoto wakubwa (wari )wanakwenda mabondeni na simu wanaokota kwa mtandao maneno ya vijana”.

Aliiomba  Serikali isaidie kuondosha  wimbi la ukatwaji wa mikarafuu kwa mapanga, ununuaji wa karafuu mbichi mitaani,  wizi unaozidi kuongezeka sambamba na  utorokaji wa wanafunzi maskulini na katika  vyuo vya Kur-ani.

“Katika maeneo ya  ndani kumezidi hata usalama bararani haupo”, alifahamisha.

“Tunaokaa karibu na njia inapoingia asubuhi wanapotoka vibarua kuelekea mikarafuuni na jioni wanaporudi utaona kiwewe gari zinavyojaa na bodaboda moja inachukua watu mpaka watano huwezi kuangalia,”alisema.

Bi. Heshima ni mama amechuma Karafuu katika maeneo mbali mbali katika Mkoa wa Kusini Pemba ikiwemo Tironi Shehia ya Mbuguani na Kichunjuu Shehia ya Mtambile Wilaya ya Mkoani Pemba.