NA MWAJUMA JUMA
TIMU ya soka ya KMKM wameshindwa kutamba uwanja wao wa nyumbani kwa kuruhusu kufungwa mabao 2-0, na Altihad katika mchezo wa awali wa klabu bingwa Afrika uliochezwa jana uwanja wa Amaan saa 8:00 mchana.
Katika mchezo huo miamba hiyo ilicheza kwa kuogopana na kila mmoja kucheza kwa umakini ili kutoruhusu bao langoni mwake.
Al-tihad ambao wapo ugenini walionekana kucheza kiufundi zaidi walipata bao la kuongoza dakika ya 45 kupitia kwa Muad Eisay, bao ambalo likitokana na uzembe wa walinzi wa KMKM.
Kipindi cha pili kilianza na pande zote mbili kucheza kwa kufuata vyema maelekezo ya makocha wao,ambao walikuwa hawatulii katika sehemu zao za kukaa kuwaelekeza.
Katika Kipindi hicho mchezo ulionekana kuwa na kasi tofauti na dakika 45 za awali, ambazo walizitumia kwa kulengeana mashambulizi ya kushtukiza.
Hata hivyo KMKM watapaswa kujilaumu sana kutokana na kukosa nafasi nyingi za wazi hasa katika vipindi vyote, huku kipindi cha pili walikosa zaidi ya mabao matano.
Mabadiliko yalifanyika kwa timu zote mbili kwa nyakati tofauti ambapo KMKM waliwatoa Abrahman Othman Ali “Chinga’ na Is-haka Said Mwinyi ‘Babui’ na kuwaingiza Faki Mwalimu Sharif na Ibrahim Abdalla ‘Edo’.