PYONGYANG, KOREA KASKAZINI
KOREA Kaskazini jana imefyatua makombora mawili yaliyoelekezwa baharini ikiwa zimepita siku mbili tangu serikali mjini Pyongyang ilipodai kwamba imefanya majaribo ya makombora mapya ya masafa marefu.
Taarifa iliyotolewa na jeshi la taifa jirani la Korea Kusini,ilisema makombora hayo mawili yalifyetuliwa kutoka katikati mwa Korea Kaskazini na kuelekezwa kwenye bahari ya mashariki inayofahamika pia kama bahari ya Japan.
Korea Kusini ilisema inashirikiana na mamlaka za ujasusi za Marekani kukusanya taarifa za kina kuhusu majaribio hayo ya silaha na kwamba jeshi lake lipo kwenye hali ya tahadhari.
Majaribio ambayo Korea Kaskazini imeyataja kuwa ya kimkakati ni ya kwanza kufanywa katika muda wa miezi sita na huenda yatachochea mvutano mpya kwenye rasi ya Korea.
Chini ya maazimio ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Korea Kaskazini inazuiwa kuunda au kufanya majaribio ya makombora ya masafa marefu lakini mara kadhaa taifa hilo limepuuza marufuku hiyo.