NA HAFSA GOLO

CHANGAMOTO ya kupasuka kwa kuta za baadhi ya madarasa skuli ya Jang’ombe Msingi  na kukosekana uzio zimeleta hofu kwa walimu  ya kuhatarisha usalama wa wanafunzi.

Mwalimu  Mkuu wa Skuli ya Jang’ombe”B” Msingi, Jabiri Mzee Mikidadi, alieleza hayo wakati alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofisini kwake skulini hapo.

Alisema  hofu hiyo imekuja   kufuatia kukatika kwa viwambaza vya jengo  lenye madarasa sita ambayo wanasomea wanafunzi 600 kwa siku.

Aidha alisema miongoni mwa vyanzo vilivyochangia  kupasuka kwa madarasa hayo ni pamoja na ukosefu wa kutokidhi  viwango vya ujenzi wa madarasa hayo, ambayo yalijengwa kupitia nguvu za wananchi pamoja na kutuama kwa maji ya mvua katika jengo hilo yaliosababisha mmomonyoko wa ardhi eneo hilo.

“Mvua kubwa zinaponyesha maji hutuama katika kiwambaza cha jengo hilo kutokana na hayana kwa kwenda baada ya kuzibwa kwa mtaro katika eneo hilo”,alisema.

Alisema ukosefu wa uzio skulini hapo ni tatizo sugu lililodumu muda mrefu na linaendelea kuleta athari ikiwemo ajali holela za wanafunzi zinazotokea ndani ya skuli.

Alifahamisha moja ya changamoto zinazojitokeza kutokana na  ukosefu wa uzio na zinaleta  wakati mgumu kwa walimu wa skuli hiyo alisema, wanafunzi  zaidi ya  wawili kwa mwezi  hugongwa na wenye bodaboda wakiwa katika mazingira ya skuli.

“Bodaboda zinapita ndani ya maeneo ya skuli na zinaendelea kuleta athari huu mwezi uliopita watoto wawili waligongwa tukawapeleka hospitali  hivyo tumewaita viongozi wa jimbo tukakaa nao nao wakaahidi kutatua kero hizo ikiwemo kuweka kifusi katika eneo linalotuama maji”,alisema.