NA HAFSA GOLO

SERIKALI imetangaza dhamira yake ya kuwapatia makaazi familia tatu zilizopata athari za mvua masika zilizonyesha mwaka 2020, katika kijiji cha Kidombo Mkwajuni.

Waziri    wa Nchi  Ofisi  ya Makamu  wa Pili  Rais  Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi, Dk. Khalid Salum  Mohamed, ameyasema  hayo,  Mkwajuni  Uyagu,  mara baada ya kufanya ziara ya kuwatembelea wananchi walioathirika na mvua  za masika za mwaka 2020.

Alisema kuwa serikali ya awamu  ya nane imejiweka karibu na wananchi   kwa kuwasikiliza shida zao, kwani ndio walio wachagua na kwaweka madarakani.

“Serikali inaendelea kusimamia kwa vitendo dhamira ya muasisi wa Mapinduzi  ya Zanzibar ya mwaka 1964 Mzee Abeid Amani Karume katika kuwapatiwa huduma bora wananchi ikiwemo makaazi bora ya kudumu”,alisema.

Aidha,   alisema kuwa ni vyema wananchi kujiepusha na kujenga sehemu ambazo zinakaa maji  ambayo hupelekea maafa na kusababisha athari mbali mbali  kwa wananchi ikiwemo kupoteza mali na kuhatarisha usalama wao pale wanapoingiliwa na maji ya mvua.

Sambamba na hilo, Dk. Khalid alisema serikali inampango wa kujenga mtaro wa maji na kuweka kalvati, ili kuepusha  changamoto ya uingiaji wa maji katika makaazi ya watu na waweze  kufanya shughuli zao za kijamii bila ya kikwazo.

Akielezea athari zilizo jitikeza katika eneo hilo sheha wa shehia ya Mkwajuni Uyagu,  Hussein Haji Kesi, alisema kuwa   jumla ya nyumba 28  ziliharibiwa na mvua  na kupelekea wananchi wengi kukosa  makaazi ya uhakika.