NA TATU MAKAME

MKUU wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Ayoub Mohamed Mahmoud amewahimiza masheha wa mkoa huo  kushirikiana  na watendaji wa  Idara ya uhamiaji kuwatambua wahamiaji haramu ili kuimarisha ulinzi na usalaama ndani ya mkoa.

Akizungumza katika semina kwa masheha wa mkoa wa Kaskazini  huko  Mkokotoni,  Ayuob  alisema   kuna taarifa za kuwepo kwa wahamiaji haramu  wanaofanya shughuli za kiuchumi  na kuishi bila ya kufuata sheria za uhamiaji ndani ya mkoa bila kuwepo taarifa za watu hao.

Hivyo aliwataka   masheha kuwatafuta watu hao na kutoa taarifa za watu wanaoingia ndani ya mkoa huo katika ofisi za uhamiaji ili kuchukuliwa za kisheria.

Alisema kwa kila shehia kuna wajumbe wanaomsaidia sheha lakini  wanashindwa kuwatambua watu wanaoingia  na kuwatoe taarifa ofisi husika.

Alisema wajumbe hao kushindwa kutoa taarifa kwa ofisi za uhamiaji ndani ya shehia zao miongoni mwa  upungufu wa uwajibikaji kwa sheha  hivyo  elimu waliyoipata itawasaidia wao na wasaidizi wao kuwabaini wahamiaji haramu ndani ya shehia zao.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhamiaji  Zanzibar,  Mussa  Masoud  Haji   akizungumza kwa niaba ya Kamishna Mkuu  wa Idara ya uhamiaji Zanzibar, alisema  utoaji wa  elimu ya uhamiaji ni mwendelezo  wa mafunzo yaliyoratibiwa na idara ya uhamiaji Zanzibar  yenye lengo la kuwajengea uwezo masheha wa kutambua masuala ya uhamiaji ili kuimarisha usalama wa nchi.

Nao masheha walisema wahamiaji haramu wanaingia  kupitia  bandari bubu hivyo elimu hiyo itawasaidia  kutekeleza wajibu wao wa  kuwabaini  wahamiaji hao.