NA LUTFIA CHUM {MUM}

WATU wawili wamekamatwa wakiwa na nyaraka bandia za serikali vikiwemo vyeti pamoja na mashine za kutengezea nyaraka hizo.

Kamanda wa Polisi  wa Mkoa wa Mjini Maghribi, Awadhi Juma Haij, aliyasema hayo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari huko ofisini kwake Mwembemadema Mjini Unguja.

Kamanda Awadh alisema watu hao wamekamatwa na askari wa JKU Agosti 25, 2021 majira ya saa 4:00 asubuhi , wakiwa na nyaraka hizo pamoja na mihuri mbali mbali ya serikali.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni  Hassan Fumu Simai miaka 50 ,  ambae ni mvuvi  mkaazi wa Mtoni  Mazurui na  Shaaban  Ali  Suleiman  mwenye miaka 50 mfanyabiashara  mkaazi wa Mwanakwerekwe.

Aidha, Kamanda  Awadhi amesema kuwa , chanzo cha kubaini  tukio hilo ni mara baada ya waombaji wa ajira ya kazi ya kujiunga na Jeshi la Polisi Tanzania iliyotangazwa  hivi  karibuni katika kambi ya JKU na JKT.

Usajili huo, Kamanda Awadh alisema, Makao Makuu ya JKU walibainika kati ya waombaji hao walikuwa na vyeti feki,  na baada ya kulifanyia kazi suala hilo walibaini kuwapo kwa mtandao uliojihusisha na vitendo hivyo.

Alisema katika kulifuatilia suala hilo pia walikamata mihuri 251, kutoka katika taasisi mbali mbali za serikali zenye nembo tofauti, ikiwemo mashine za Printer tatu, Laptop moja, Vyeti 271 vya kughushi na  Vibati vya kugongea Mihuri ( stamp) sita  vyote  vikiwa vya kugushi .

Kamanda Awadhi amesema, watuhumiwa hao  mara baada ya kukamatwa walikabidhiwa kwa Jeshi la Polisi mkoa wa Mjini Maghribi, kwa hatua zaidi za kisheria  na watafikishwa mahakamani  upelelezi utakapo kamilika .

Wakati huo huo, katika operesheni hiyo, wamefanikiwa kukamata watu wawili  wakijihusha na kufanya biashara ya dawa za kulevya kwa kuuza na kutumia dawa hizo.

Tukio hilo alisema lilitokea Agosti 30, 2021,  majira ya saa 7: 00  mchana  huko  Mahonda, askari walimkamata  Michael  Willbert John  miaka 30 mkaazi wa Mahonda,  akiwa ma kete 560 za dawa za kulevya aina ya Heroin, akiwa amezificha ndani ya Choo katika nyumba yake anayoishi.

Aidha,  Kamanda Awadhi amesema,  katika siku hiyo majira ya  saa 4:00 asubuhi huko Kwaalinato  Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Maghribi,  askari walifanikiwa kumkamata  Asya Abdalla  Juma, mwenye miaka 21,  akiwa  na Dawa za kulevya  aina ya Heroin  Gram 20  jambo ambalo ni kosa kisheria.