NA   LUTFIA   CHUM (MUM)

Wafanyabiashara wa Ukindu  katika maeneo ya Saateni  Mkoa wa Mji  Magharibi Unguja,  wameiomba  serikali kuwaangalia kwa jicho la huruma  katika biashara ya ukindu, kwa kuwapatia  masoko, ili kuweza  kuondokana na changamoto zinazowakabili   kwa mda mrefu  sasa.

Wakizungumza na Zanzibar Leo, wamesema  ,  wengi wao hawana misingi mizuri  ya kuendesha  biashara hiyo, kufanya hivyo kutasaidia  na kuboresha mazingira wanayofanyia kazi  kila siku, ili kujiinuwa kimaisha .

Wafanyabiashara hao wamesema, biashara ya ukindu kwa sasa ni ngumu, kwani hakuna wanunuzi wa uhakika , hali inayopelekea kukaa kutwa nzima bila  kuuza,  jambo ambalo  linaogeza ugumu wa maisha.

Wamesema  kuwa,  bado wanakabiliwa na changamoto nyingi katika biashara ya ukindu,   kwani mazingira wanayo fanyiabiashara ni changamoto pia,  ingawa wapo katika eneo hilo kwa zaidi ya miaka 20 sasa, lakini bado mazingira hayajawa rafiki kwao.

Wakizungumzia  kwa upande wa ushuru wamesema, kila wiki wanalipa elfu saba kwa ajili ya usafi, lakini ni  jambo la kushangaza  hakuna usafi unaofanywa  hali inayowalazimu   kufanya wao wenyewe,  ili kuona mazingira yanayowazunguka yanakuwa katika usafi.

Wafanya biashara hao, wameiomba serikali, kwa  kuwatafutia masoko ya ndani na nje  ya Zanzibar,   kwani kufanya hiyo kutainua biashara ya ukindu  hapa Zanzibar, na  kupelekea kuongezeka kwa mapato   serikalini  pia kwa mtu mmoja mmoja.

Aidha wafanya biashara hao   wamesema ni vyema serikali  kuwapatia mikopo ,  kwa lengo la  kukuza mitaji yao,   ili kuboresha  zaidi,  ambayo bado haijawa ya uhakika.

Ofisa Uhusiano  wa Baraza la Manispaa Mkoa wa Mjini, Magharib  Seif Ali Seif,  amesema muongozo wa serikali ni kulipa kila mwezi  na siyo  kila wiki kwani Kaya , Maduka , Magodauni na Stoo vyote vinatozwa  kwa mwezi na hakuna malipo ya usafi yanayofanywa kwa kila wiki.