NA MADINA ISSA

MKUU wa Mkoa wa Kusini Unguja, Rashid Hadid Rashid amesisitiza umuhimu wa  walimu kuendeleza   michezo kwa wanafunzi maskulini.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu huyo, mkuu wa wilaya  ya Kusini Unguja Rashid Makame Shamsi,  katika hafla fupi ya  kupokea  makombe ya ushindi kwa wanafunzi walioshinda sherehe za elimu bila malipo zilizofanyika Pemba hivi karibuni.

Alisema suala la michezo  kwa wanafunzi ni muhimu kwani mbali ya kujengeka kiafya na kiakili,  lakini kunawaepusha na kujiingiza  katika  vitendo viovu ikiwemo utumiaji wa dawa za kulevya.

Aidha  aliwapongeza wanafunzi hao  kwa ushindi  walioupata wa kuchukua nafasi  ya tatu  kati ya mikoa mitano ya Zanzibar hali iliyopelekea kuletea sifa mkoa huo.

Sambamba na hayo, aliwasihi kusoma kwa bidii ili kuweza kufanya vizuri katika masomo yao.

Kwa upande wake mratibu wa michezo wilaya ya Kati, Abdulwahad Dau Haji, aliwaomba wazazi na walezi kutoa mashirikiano kwa watoto wao, juu ya kushiriki michezo maskuli na kuondokana na dhana ya kwamba michezo inapelekea kufeli mitihani yao.

Nao wanafunzi walioshiriki michezo hiyo, wamesema mbali ya kupata ushindi lakini pia wamejenga uhusiano na wanafunzi kutoka skuli mbali mbali na kuwataka wanafunzi wenzao kutovificha vipaji vyao kwani michezo itaweza kuwapatia ajira.

Wanafunzi hao wamefanikiwa kupata makombe  saba na  medali 33 zikiwemo dhahabu 14, fedha 11 na shaba  nane, zilizohusisha michezo tofauti ikiwemo mpira wa pete, mpira wa miguu, riadha, ngonjera, utenzi, nyimbo na mashairi.