‘’KIPINDI cha mvua wanafunzi hulazimika niwafungie wasije madrasani mpaka zitakapo malizika,’’ hayo ni maneno ya Sada  Khamis  Hamad  mwenye ulemavu wa viungo ambae ni mwalimu wa madrssa.

Alisema ulemavu alionao si kikwazo kwake kwa kuwa anatimiza ndoto zake za kuwa mwalimu wa madrassa.

Hii ni baada ya kuukosa uwalimu wa skuli kutokana na changamoto za kadhaa ila hakukata tamaa kwa sababu hivi sasa ni mwalimu wa madrasa.

“Nilikuwa natamani siku moja niwe darasani nafundisha ila sikubahatika, sikusoma skuli hata darasa moja, kwani ilikuwa iko maeneo ya mbali na siwezi kutembea”, anakumbuka.

Alisema ukosefu wa kiti mwendo kwa wakati huo, na hasa kutokana na ukosefu wa fedha waliokuwa nao wazazi wake, ulimkosesha elimu ya skuli.

Yote hayo ni masikitiko ya Mwalimu wa Madrasa ya Qur-aan Sada Khamis Hamad mwenye ulemavu wa viungo anaeishi katika kijiji cha Shumba Vyamboni Wilaya ya Micheweni Pemba.

Ukhti Saada Khamis Hamad ambae ni mtoto wa sita  katika familia yao, anasema suala la kukata tamaa na yeye lilikuwa mbali mno.

Baada ya miaka kadhaa, alishindwa hakuweza tena kwenda madrasa kutokana na hali yake na kwa vile hana usaidizi wa kigari ambacho chengemuwezesha kumsaidia.

Baada ya kuona anakosa kusoma, ndipo akamua anzishe madrasa yake mwenyewe baada ya kuhitimu kusoma Qur-aan  ili  kuiendeleza  elimu yake.

“Nilisema ijapo kuwa sikuweza tena kwenda  kusoma, lakini   isiwe  sababu  ya  kukaa  tu nyumbani, ndipo  nikamua  nianzishe  madrasa  yangu, ili kuwafundisha watoto”, anaeleza.

Alisema huu ni mwaka wa nne tangu kuanzisha madrasa hiyo, ambapo alianza  na  wanafunzi  wanne wawili wa kike na  wawili  wanaume  na  sasa  ana  wanafunzi 52.

CHANGAMOTO

Ukhti Saada alisema kuwa anakosa nayoiona na kumkosesha usingizi ni ukosefu wa  sehemu  salama  ya  kusomeshea wanafunzi kutokana na mazingira yake.

Kwake mazingira hayo, hayako sio rafiki,  kwani  kwa sasa anatumia kibaraza cha  nyumba  yao kuwafundishia  wanafunzi  wake.

“Nasumbuka sana hususan kipindi cha  mvua barazani panakuwa  hapasomeki  inabidi  wanafunzi  wasije  madarasa mpaka mvua  zikate”, anasema.

Aisema kuwa wanafunzi wamekuwa wakikimbia na kwenda madrssa nyengine kwa kukosa sehemu  salama  za kufundishia.

“Si vyema nguvu zote zikaelekezwa kwenye ujenzi wa miskiti pekee, bali msingi wa dini ya kiislamu, ni uwepo wa madrassa za kisasa na sio kusomea barazani, hivyo nawaomba wale wote watakaogiswa na madrasa hii kutusaidia”, alisema.

WANAFUNZI WAKE

Asha Khamis na Ali Juma wanafunzi wanaosoma madrsa hiyo a ukhti Saada, wanasema hawaridhishwi  na  kitendo cha kusoma  barazani.

“Kwakweli  hatupendi kusoma mazingira haya, kwani  pakiwa na jua hapakaliki, na kukiwa na mvua tunafungiwa kabisa,’’wanasema.

Wanasema kama kweli kuna nia ya dhati kwa wadau wa haki za watu wenye ulemavu na watoto kupata elimu, hakuna budi kuchangiwa na kujenga madrassa ya kisasa.

MAMA MZAZI

Hadia Salim Ameir, anasema  Mungu  amemjaalia  kuzaa  watoto  wanne  wote  wenye  ulemavu  wa viungo  ambapo  mmoja  alifariki.

“Nilikua nawazaa ni wazima lakini mwisho wake wanakua walemavu, na sikuwapeleka Hospital nikajua ni sababu gani ilopelekea  hivyo”, anasema mama huyo.

Aidha alieleza kuwa anaishi katika mazingira magumu yeye na watoto wake kwani  hata nyumba yao wanayoishi ni mbovu na haina hata  huduma rafiki  za  vyoo  kwa  ajili  yao.

“Baba yao ameshafariki huduma zote wananitegemea mimi na sina msaidizi, sina  hata  kazi ya uhakika ya kufanya  maisha  yangu  ni  magumu  nahitaji  msaada”, alieleza.

Alisema viongozi wa majimbo kama Mbunge au Mwakilishi hawajawahi kupita katika familia yao angalau kuangalia changamoto zinazowakabili.

Kwa upande wake Mratibu wa Baraza la Taifa la Watu wenye  ulemavu  Pemba,  Mashavu   Juma  Mabrouk, anasema  wamekua  wakiwasaidia  watu  wenye  ulemavu, ambao  wanajishuhulisha  na  harakati  mbali mbali.

Hata hivyo aliwashauri wazazi wa wanafunzi wanaosoma katika madrassa hiyo, kuonesha mfano kwa  kuanza kuchangishana fedha kwa ajili ya kuanzisha ujenzi wa madrassa ya kisasa.

“Sisi Baraza hatuna mfuko maalumu wa kumsaidia mtu mmoja moja kama huyo, kwani anayoyafanya ni mambo ya kijamii ispokuwa tunawaomba wanajamii kuchangia, ili aweze kujenga madrassa”, alishauri.

UONGOZI WA SHEHIA

Sheha wa shehiya  ya Shumba vyamboni Time  Said   Omar, ameeleza kuwa  mwalimu  huyo anapata shida kwani  anasomeshea  wanafunzi wake  katika baraza  ya  nyumba  yao  na  wakati  mwengine  hukaa kwenye  Muembe.

ALIsema  ameshachukua  jitihada  mbali  mbali  kuhakikisha  anapatiwa msaada  wa kujengewa madrassa  japo  chumba kimoja,  lakini  bado  hajafanikiwa.

“Nimeshawapeleka viongozi wengi ili kumsaidia lakini bado hatujafanikiwa na   hivi sasa nimejipanga niende   kwenye jumuia ya Milele Foundation kungalia uwezekano wa kusaidiwa”, alisema.

Sheha huyo alisema licha ya ulemavu wake lakini mungu amemjalia kipaji cha elimu  ameshafika  Dar-es-salamu  kushiriki mashindano ya qur an, hivyo anahitaji  kuungwa mkono   kwa hali na mali  ili kuendeleza  kipaji chake hicho.

UONGOZI WA WILAYA

Nae Mkuu wa wilaya ya Micheweni Mgeni Khatib Yahya, alisema anelewa changamoto ya mwalimu, huyo ingawa wanaangalia namna ya kumsaidia.

“Hakuna fungu maalum kwa ajili ya kumsaidia mtu  mmoja  mmoja  kwa  ajili  ya  kujengea  nyumba  ama  Madrassa,  lakini kama wakitokezea wahisani tutampekelekea”, anasema.

OFISI YA MUFTI

Msaidizi Katibu ofisi ya Mufti Sheikh Said Ahmad Mohamed, alisema ofisi hiyo ndio msimamizi mkuu wa madrasa zote za Qur-an, ahivyo, aliahidi kuonana naye.

“Nimevutiwa mno kuona kuna mwanamke tena mwenye ulemavu wa viungo ameanzisha mpango wa kuihuisha dini ya kiislamu, na sisi tutaangalia namna ya kumasaidia,” anasema.

KATIBA YA ZANZIBAR YA MWAKA 1984

Kifungu cha 10 (g) kinafafanua ‘kwamba serikali itawekea mazingira rafiki kwa makundi ya wagonjwa, waliojiajiri, wazee, watoto na watu wenye ulemavu’.

Aidha kifungu cha 12 (1) kimefafanua kuwa, ‘watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria’.’

SHERIA YA WATU WENYE ULEMAVU NO 9/2006

Kifungu cha 9, kinaelezea haki ya kupata elimu kwa watu wote wenye ulemavu na mafunzo mengine kama ilivyo kwa raia wengine.